Jumamosi, 2 Desemba 2017

DK.SHEIN AWATAKA VIONGOZI WANAOCHAGULIWA NDANI YA CCM KUWA KARIBU NA WANANCHI


Na Is-haka Omar, Picha na Abeid Machano Kh - Zanzibar.
         

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi(CCM),Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein amewataka viongozi watakaochaguliwa kupitia Mkutano Mkuu wa Chama katika Mkoa wa Kusini Unguja, kuwa karibu na wananchi kwa kufuatilia na kushughulikia matatizo yanayoikabili jamii.


Pia,amefafanua kuwa kila mwanachama anayepata nafasi ya uongozi ndani ya CCM ni lazima awe na sifa ya kufuatilia masuala mbalimbali hususan kero zinazowakabili wananchi ili ziweze kutafutiwa ufumbuzi wa kudumu na mamlaka husika.

 Rai hiyo aliitoa jana wakati akifungua Mkutano Mkuu maalum wa Uchaguzi wa CCM, katika Mkoa huo, uliofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Coconut Tree huko Marumbi Wilaya ya Kati Unguja.

Amewambia  wanachama wa Chama Cha Mapinduzi kuwa wanatakiwa kuwachagua viongozi wabunifu ambao watanzisha miradi ya maendeleo itakayoongeza nguvu za kiuchumi ndani ya Chama na kutoa ajira za kudumu kwa wananchi. 

Dk.Shein ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, amewasisitiza  wajumbe wa mkutano huo kutumia vizuri haki yao ya kikatiba kwa kuchagua viongozi imara wenye misimamo isiyoyumba katika kusimamia Sera za Chama na serikali kwa maslahi ya wanachi wote.

“CCM ina uzoefu mkubwa katika kufanya mageuzi ya kisera, kifikra, kiitikadi pamoja na kimkamkati kulingana na mabadiliko ya nyakati yanavyokwenda. 

Ameongeza  kuwa ndio maana hivi karibuni chama kimefanya mabadiliko makubwa katika Katiba ya Chama ili miongozo ya kikanuni iendane na mahitaji ya wananchi ambao ndio wapiga kura wa kuiweka CCM madarakani kwa kila uchaguzi mkuu. 

Katika maelezo yake amesema  viongozi watakaopewa dhamana ya kuongoza kwa kipindi cha miaka mitano wanatakiwa kutambua kuwa wao ni miongoni mwa wapiganaji wanaounda jeshi la CCM litakalofanikisha ushindi katika mwaka 2020.

 Akitoa nasaha kwa wanachama wanaogombea na watakaoshindwa kupata nafasi za uongozi katika ngazi mbalimbali amewasihi wasivunjike moyo bali washirikiane na wenzao walioshinda na kwamba CCM ni Chama cha watu wote.

 Mbali na hilo, amesema  hali ya kisiasa nchini imeendelea kuwa na mvuto wa kipekee kwa wananchi na ushahidi wa jambo hilo ni ushindi uliopatikana katika uchaguzi mdogo wa madiwani Tanzania bara ambapo CCM kimeshinda kata 42 kati ya 43. 

 Amesema  CCM sio Chama cha mtu mmoja kama ilivyo kwa baadhi ya vyama vingine vya kisiasa nchini vilivyopoteza muelekeo kwa kupokonyana nafasi za uongozi. 

 “ Viongozi mtakaochaguliwa kemeeni makundi ya kuhatarisha uhai wa chama pamoja na rushwa ili kuendeleza misingi imara ya ukombozi iliyofanywa na waasisi wa ASP wakiongozwa na aliyekuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar Marehemu Mzee Abeid Amani Karume aliyepigania wanyonge wa Zanzibar kupitia mapinduzi ya mwaka 1964.”, alieleza Makamu Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar. 

Akizungumzia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM katika Mkoa huo, amesifu juhudi za viongozi mbalimbali wa Chama na serikali katika kusimamia vizuri upatikanaji wa huduma za kijamii ikiwemo kuimarika kwa sekta za elimu, afya, miundombinu ya maji safi na salama pamoja na barabara. 

 Dk.Shein amesema  kupitia mradi wa Ras Al – Khaimah unaodhamini uchimbaji wa visima vya maji safi na salama, Serikali ya SMZ imejidhatiti kumaliza kero ya ukosefu wa huduma hiyo kwa wananchi wa Mkoa huo kwa kipindi kifupi kijacho.

 Ameeleza  kwamba utoaji wa huduma bora za kijamii na kiuchumi ndio kipimo muhimu cha kuipima serikali na kukitathimini Chama cha Mapinduzi kama kimetekeleza kwa ufanisi mambo kilichoyaahidi kwa wananchi. 

 “ Ni wajibu wa kila kiongozi ndani ya chama na Serikali kufanya kazi kwa kujituma na kwa bidii kubwa, ili wananchi wanapotutathimini na kutuhoji waridhike na majibu yetu kwani yatakuwa yanaendana kile tulichoahidi katika kampeni za uchaguzi uliopita”, amesisitiza Dk.Shein. 

 kwa upande wake Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan,ameeleza matarajio yake katika uchaguzi huo ni kuchaguliwa kwa viongozi makini na watakaoivusha salama CCM kwa kila jambo linalotakiwa kutekelezwa kwa maslahi ya Chama.

Samia ambaye ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa, amesema  viongozi hao ambao watachaguliwa wataisaidia kuondoa utendaji wa mazoea visiwani humo na kwamba kuleta mabadiliko ya kimaendeleo kwenye nyanja mbalimbali. 

Naye Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Zanzibar Dk. Abdulla Juma Mabodi amesema  uchaguzi wa Chama Cha Mapinduzi na jumuia zake kuanzia ngazi za mashina hadi Mikoa umeendelea kufanyika vizuri na kwa kufuata matakwa ya miongozo ya kanuni za uchaguzi. 

Ameeleza kuwa  kupitia uwezo na uzoefu wa viongozi wanaochaguliwa katika Uchaguzi huo kuna matumaini makubwa ya Chama cha Mapinduzi kupata ushindi wa kihistoria katika uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020.

 “Kupitia uchaguzi huu Chama kimefanya kazi ya ziada kuhakikisha viongozi wote wanaoteuliwa kugombea nafasi za uongozi hawana sifa chafu za makundi ya usaliti,rushwa na kupanga safu za wagombea uongozi.” ameeleza  Dk.Mabodi.

Katika uchaguzi huo nafasi zinazogombewa  katika Mkoa huo ni nafasi za Mwenyekiti, Katibu wa Siasa na Uenezi, Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Mkoa nafasi tano(5) kutoka kusini pamoja na nafasi tano(5) kutoka kati.
MJUMBE wa Kamati Kuu ya CCM Taifa ambaye pia ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan akizungumza katika mkutano huo.

NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Mabodi akizungumza katika mkutano Mkuu huo uliofanyika katika hoteli ya Coconut Tree Marumbi  Mkoa wa Kusini Unguja.

MAKAMU Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk.Ali Mohamed Shein(kushoto)akimkabidhi taarifa ya utekelezaji ya miaka mitano ya Mkoa huo, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Mabodi.
MAKAMU Mwenyekiti wa CCM Zanzibar akimkabidhi taarifa ya utekelezaji ya miaka mitano ya Mkoa huo pamoja na nyaraka mbali mbali za Chama, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania . Mhe. Samia Suluhu Hassan.
WAJUMBE wa Kamati ya siasa ya Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Kusini waliomaliza muda wao wa uongozi kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita.


MAKAMU Mwenyekiti wa CCM Zanzibar  Dk. Ali Mohamed Shein akipiga kura ya kuwachagua viongozi wa ngazi hiyo akiwa ni miongoni mwa wajumbe wa mkutano huo.

MJUMBE wa Kamati Kuu ya CCM Taifa ambaye pia ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan akipiga kura ya kuwachagua viongozi mbali mbali wa CCM Mkoa wa Kusini Unguja.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni