Jumatano, 29 Aprili 2015

“Watakiwa kuwacha kuwabeba Viongozi” Waride.

Viongozi wa Chama Cha Mapinduzi wametakiwa kuacha kuwabeba viongozi wanaowania nafasi za uongozi katika Majimbo kwani muda wa kufanya hivyo haujafika.

 Akizungumza na Viongozi wa wanachama wa CCM katika Majimbo ya Fuoni, Dimani, Kiembesamaki na Mwakaje Unguja, Katibu wa Idara ya Itikadi na Uenezi ya Kamati Maalum ya CCM Waride Bakari Jabu alisema ni makosa kwa kiongozi wa Chama kumbeba, kumtangaza au kumtembeza kwa wanachama.

Aliendelea na kusema kuwa Chama hakijatangaza wakati wa kufanya kampeni kwa wagombea kwani muda ukifika watajulishwa kwa kupewa taarifa katika maeneo yote.

Aliwataka Viongozi na Wanachama kuendelea kusimamia na kutekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika miradi ya maendeleo kwa maslahi ya wananchi.

 Aidha aliwataka wanachama kujipanga vizuri na kuhakikisha kuwa CCM inashinda Majimbo yote katika Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2015.