Jumapili, 29 Aprili 2018

KISONGE YAPATA VIONGOZI WAPYA


 Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Amani Abdi Ali Mzee ‘Mrope’ (anayezungumza wa pili kulia) akifungua mkutano wa uchaguzi wa viongozi wa maskani ya Kisonge.

 Baadhi ya wajumbe wa mkutano huo wa uchaguzi wakifuatilia matukio mbali mbali yanayoendelea kabla ya uchaguzi kufanyika.

 Mgombea wa nafasi ya Mwenyekiti wa maskani ya CCM Kisonge Juma Raja Juma akipiga kura katika uchaguzi wa viongozi wa maskani hiyo kabla ya kushinda nafasi hiyo.









MASKANI ya Kisonge ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar imempata Mwenyekiti wao mpya,Juma Rajab Juma baada ya kuchaguliwa katika uchaguzi uliofanyika jana,ukumbi wa Nasari ya matumbaku Miembeni.

Uchaguzi huo ulikuwa ni wa ushindani mkubwa ambapo Mwenyekiti huyo aliibuka kidedea baada ya kupata kura 93 kati ya 198 huku kuura 6 ziliharibika.

Wagombea wengine wa waliogombea nafasi hiyo ni Mohamed Haji Dau aliyepata kura 3,Mwanangasama Mohamed aliyepata kura 66.

Akizungumza na wajumbe wa mkutano huo Mwenyekiti huyo mpya,Juma, aliwashukru  wanachama hao kwa kumuamini na kumchagua ambapo ameahidi kushirikiana nao kwa lengo la kuiletea maendeleo Kisonge.

Mapema akifungua Mkutano wa uchaguzi wa maskani hiyo , Mwenyekiti wa CCM Wilaya Amani  Abdi Ali Mzee ‘Mrope’ amewataka wajumbe wa mkutano huo kutochaguana kwa urafiki na kwamba wachaguane kwa uwezo wa kiutendaji na watakaounganisha wana CCM.

Aidha, Mwenyekiti huyo amewasisitiza viongozi watakaochaguliwa kupitia uchaguzi huo kutokubali kuharibiwa heshima ya maskani hiyo ambayo imekuwa na historia ya ukomavu wa kisiasa.

“ Baadhi ya watu wasioipenda CCM wakisikia maskani ya Kisonge ina mpasuko basi wao wanafurahi na kuendeleza mbinu chafu za kuihujumu, kwani hata uchaguzi huu najua kuna watu nje huko hawakupenda ufanyike lakini ndo sasa ushakuwa endeleeni na mapambano ya kukilinda na kukitetea Chama Cha Mapinduzi.

"Kisonge haiwezi kusimama bila ya umoja na mshikamano kwani wazee wetu walioasisi CCM na kuikomboa Zanzibar walikuwa na umoja wakipendana na kutumia vikao halali kusuluhisha migogoro iliokuwa ikijitokeza katika kuwagawa hivyo na sisi tunatakiwa kuweka fikra zetu katika  utamaduni huo na kuachana na misuguano isiyokuwa ya lazima na yenye kubomoa chama,"alisema Mwenyekiti huyo wa Wilaya

Alisema ni wakati wa kila mwana- CCM kuelekeza nguvu zake katika kujiandaa na ushindi wa uchaguzi wa mwaka 2020 na kupoteza muda katika kurumbana wenyewe kwa wenyewe katika mambo yasiyokuwa na tija.

Mwenyekiti huyo wa Wilaya ya mjini  Mrope, alitoa wito kwa wagombea ambao kura zao hazitotosha wasinune na badala yake washirikiane katika kushauri viongozi watakaochaguliwa ili kuendelea kuwa wakomavu wa kidemokrasia.

Kwa mujibu wa katiba na kanuni viongozi mbali mbali waliochaguliwa katika maskani hiyo wataongoza kwa kipindi cha miaka mitano.


Pia, kwa upande wa wagombea wa nafasi ya wajumbe wa kamati ya uongozi ya maskani hiyo ambao ni wajumbe wanne lakini walijitokeza ni 12, ambapo jumla ya kura zilizopigwa ni 168 huku zilizoharibika ni 13.

Walioshinda nafasi ya wajumbe wa kamati hiyo ni ni Dauwat Saleh kwa kura 70, Omar Mohamed Suleiman kura 84, Suwaila Masoud Mohamed kura 96 na Mbaraka Haji Vuai kwa kura 85.

Kupitia uchaguzi huo uongozi mpya wa Kisonge ulimteuwa mjumbe mmoja ambaye ni Suwaila Masoud Mohamed kuwa Katibu wa maskani hiyo kati ya wanne waliochaguliwa katika uchaguzi huo.


Ijumaa, 20 Aprili 2018

CCM YAWATAKA WANANCHI KUFUATA MAELEKEZO YA SMZ

KATIBU wa NEC, Idara ya Organazesheni Bakari Hamad Khamis(kulia) akizungumza na uongozi wa CCM Mkoa wa Mjini chini ya Mwenyekiti wa Mkoa huo ndugu Talib Ali Talib (wa pili kushoto), kabla ya kuanza ziara ya kuwafariji wananchi waliopata maafa yaliyotokana na mvua.

 VIONGOZI wa CCM wakiongozwa na Katibu wa NEC, Idara ya organazesheni ndugu Bakari wakiangalia nyumba za wananchi wa shehia ya Sebleni zilizovamiwa na maji ya mvua yaliyojaa katika bwawa lililopo katika maeneo hayo.

 NYUMBA  ya mkaazi wa sebleni Masoud Issa iliyopo katikati ya maji katika eneo hilo.
 SHEHA wa shehia ya Kwa wazee Khalfan Salum akitoa maelezo juu ya nyumba za wananchi zilizopata maafa ya mvua katika eneo la shehia yake.

 NYUMBA za wananchi wa maeneo ya Kwa wazee zilizoingiliwa na maji ya mvua za masika.

 MTAA wa mtumwa jeni Jimbo la magomeni lililoathiwa na maji ya mvua kutokana na baadhi ya wananchi kujenga katika njia za kusafirisha maji ya mvua.

 KATIBU wa NEC, Idara ya Organazesheni Bakari Hamad Khamis(kulia)akizungumza na Mwenyekiti wa CCM jimbo la Magomeni Mahmoud Juma Ali katika ziara ya kuwafariji wananchi waliopata maafa jimboni humo.

 DARI ya nyumba ya mzee Ali Haji Makame iliyoharibika kutokana na mnazi kuangukia nyumba yake huko Pwani mchangani.

 NYUMBA ya Bi. Jina Makame Hamdu iliyoanguka kutokana na mvua zinazonyesha nchini huko Chaani kubwa Wilaya ya Kaskazini 'A' Unguja.

 MMOJA wa wanafamilia ya Bi. Jina akitoa maelezo juu ya athari walizopata katika maafa hayo.


 NYUMBA ya Juma Khamis Mohamed iliyoporomoka kwa mvua huko Chaani kubwa Wilaya ya Kaskazini Unguja.



 KATIBU wa NEC, Idara ya Organazesheni Bakari Hamad Khamis kimfariji mkaazi wa shehia ya Mkwajuni ndugu Kero Chumu Juma ambaye ukuta wa nyumba yake umeanguka kutokana na mvua.



 KATIBU wa NEC, Idara ya Organazesheni Bakari Hamad Khamis akizungumza na bi.Maua Vuai Ame mkaazi wa shehia ya Kiwengwa ambaye nyumba yake imeezuka kutokana na maafa hayo.


 KATIBU wa NEC, Idara ya Organazesheni Bakari Hamad Khamis na msafara wake wakiwa katika eneo la shughuli za uvuvi huko Mwanga pwani Wilaya ya Kaskazini 'B' Unguja, kwa ajili ya kuwafariji wananchi ambao boti sita zimeharibiwa na maafa hayo

 BOTI aina ya ngwanda iliyoharibika kutokana na mvua zinazonyesha huko mwanga pwani.

 JOPO la viongozi wa CCM wakisikiliza maelezo kutoka kwa wakaazi wa maeneo hayo ya mwanga pwani.

 BOTI iliyoharibika kutokana na maafa hayo katika eneo la mwanga pwani.



CHAMA Cha Mapinduzi(CCM) kimewataka wananchi kufuata maelekezo na ushauri wa Serikali juu ya kujikinga na maafa yanayotokana na mvua za masika.

Rai hiyo imetolewa na Katibu wa Idara ya Organazesheni CCM Zanzibar Bakar Hamad Khamis, alipotembelea maeneo mbali mbali yaliyoathiriwa na mvua katika Mikoa ya Mjini na Kaskazini Unguja.

Alisema kila mwananchi anatakiwa kuchukua tahadhari kwa kufuata maelekezo ya Serikali hasa  kuepuka kujenga katika maeneo hatarishi kwa lengo la kujikinga na madhara hayo yanayosababishwa na mvua za masika zinazonyesha kila mwaka nchini.

Bakari alisema lengo la ziara hiyo ni kuwafariji wananchi wote waliopata majanga sambamba na kuitaka serikali kupitia mfuko wa maafa iharakishe misaada kwa wananchi ambao nyumba zao zimebomolewa na mvua hizo.

Akizungumza Katibu wa Wilaya ya Mjini Fatma Shomari, alisema katika Wilaya hiyo jumla ya nyumba 68 zimeathiriwa na mvua hizo pamoja na kusababisha kifo cha mtoto Ramadhan Juma Khamis (4) katika shehiya ya Sebleni.

“Bado tunaendelea kukusanya taarifa za wananchi mbali mbali waliopata maafa katika Wilaya yetu ili tuziwasilishe kwa serikali kwa ajili ya hatua stahiki za misaada”, alisema Katibu huyo.

Kwa upande wake sheha wa shehia ya Kwa wazee Khalfan Salum alieleza kuwa jumla ya nyumba 130 zenye wakaazi wanaokisiwa kufikia 1300 zimeathiriwa na mvua hizo na wananchi wa maeneo hayo wamehama na kutafuta hifadhi kwa majirani waliopo katika maeneo salama.

Akizungumza mkaazi wa eneo hilo Haji Makame ‘London’ aliiomba serikali kupitia Manispaa ya mjini kuharakisha mradi wa ujenzi wa mtaro mkubwa utakaokuwa ukisafirisha maji yanayotwaama katika maeneo hayo ambayo kwa sasa ni makaazi ya kudumu kwa wananchi.

Aidha Katibu wa CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja, Mulla Othaman Zubeir alisema zaidi ya nyumba 18 na boti sita za uvuvi aina ya mtando na ngwanda zimeharibiwa na mvua zilizonyesha katika maeneo mbali mbali ya mkoa huo na kuathiri mali za wananchi.

Mbali na maafa hayo Mulla alifafanua kuwa maafa hayo yamesababisha kifo cha mtoto wa mwaka mmoja aliyetumbukia katika shimo la takataka katika shehia ya Chaani kubwa Wilaya ya Kaskazini ‘A’ Unguja.

Akiwafariji wananchi wa Mkoa huo Katibu wa NEC, Idara ya Organazesheni CCM Zanzibar Bakari Hamad aliuagiza uongozi wa CCM Mkoa huo kusaidia shughuli za ujenzi wa nyumba ya Mkaazi wa shehia ya Mwange Mbaki Makame Ali (54), ambaye nyumba yake imeanguka kutokana na mvua zinazonyesha nchini.

Katibu huo wa Organazesheni Bakari aliwasihi wananchi waliopata maafa kuwa wavumilivu kwa kipindi hichi, huku Chama Cha Mapinduzi kikiendelea kuisimamia serikali iharakishe misaada kwa wananchi waliopata maafa hayo.

Naye mkaazi wa shehia ya Mkwajuni  Kero  Chumu Juma alikipongeza Chama Cha Mapinduzi kwa kuendeleza utamaduni wa waasisi wa ASP waliokuwa wakiwatembelea wananchi mara kwa mara kwa lengo la kuratibu changamoto zao na hatimaye kuzitafutia ufumbuzi kupitia serikali.

“Nimefurahi sana kuona uongozi wa CCM umekuja kunifariji kwani utamaduni huu ulikuwa umepotea kwa muda mrefu na kwa sasa naona umerudi kwa kasi kubwa, hii inaonyesha wazi kuwa Chama kinarudi kwa wananchi wake”, alisema Mkaazi huyo ambaye ukuta wa nyumba yake ulianguka kutokana na mvua hizo.

Maeneo yaliyotembelewa katika ziara hiyo ni shehia ya Sebleni, Kwa wazee, eneo la Mtumwa jeni, Pwani mchangani, Chaani kubwa, shehia ya Kibeni, Shehia ya Mwange, shehia ya Mkwajuni na Mwanga pwani.




Jumatano, 18 Aprili 2018

CCM Z'BAR YAWAFARIJI WANANCHI WALIOATHIRIWA NA MVUA MIKOA YA MAGHARIBI NA KUSINI UNGUJA

 KATIBU wa NEC, Idara ya Organazesheni CCM Zanzibar Ndugu Bakari Hamad Khamis(kulia wa pili) akizungumza na mmiliki wa nyumnba iliyopata madhara ya kubomoka kwa shimo la choo  Bi. Sania Zahor Omar(alikaa chini)  uko Magogoni kwa mabata, katika ziara ya CCM ya kuwatembelea wananchi walioathiriwa na mvua.

  ENEO la  shimo la choo  cha Bi. Sania Zahor Omar mkaazi wa Magogoni kwa Mabata  kilichoanguka kutokana na mvua zinazonyesha visiwani Zanzibar.

 

 VIONGOZI mbali mbali wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Magharibi wakiongozwa na KATIBU wa NEC, Idara ya Organazesheni CCM Zanzibar Ndugu Bakari Hamad Khamis,katika ziara ya Chama ya kuwatembelea wananchi walioathiriwa na mvua katika Wadi ya Pangawe mtaa wa Pangawe bondeni. 
 VIONGOZI mbali mbali wa CCM wakikagua maeneo yaliyoathiriwa na maji ya mvua kutokana na baadhi ya wananchi kuziba mitaro ya kupitisha maji.


VIONGOZI wa Chama cha Mapinduzi pamoja na Diwani wa wadi ya Pangawe ndugu Makame Pandu Mgana wakiangalia mitaro ya maji iliyozibwa na nyumba za makaazi ya wananchi katijka eneo hilo. 

 BAADHI ya nyumba iliyoathiriwa na maji ya mvua zinazoendelea kunyesha uko Fuoni Chunga.

 MUONEKANO wa eneo lililojaa maji ya mvua katika mtaa wa Fuoni Chunga(Janga mizini)

 MUONEKANO wa eneo lililojaa maji ya mvua katika mtaa wa Fuoni Chunga(Janga mizini)

 NYUMBA zilizoathiriwa na maji Fuoni Chunga 

 NYUMBA iliyoangukiwa na mti huko Dimani Tasaf ambayo mmiliki wake ni Ndugu Muhidin Khamis Muhidin.

 NYUMBA iliyoanguka ukuta kutokana na mvua zinazonyesha uko Mtoni kidatu juu ambayo mmiliki wake ni Makame Sheha Juma.

 KATIBU wa NEC, Idara ya Organazesheni CCM Zanzibar Ndugu Bakari Hamad Khamis(kushoto)akisalimiana na Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Tanzania-Zanzibar Abdallah Haj Haidar alipowasili katika Mkoa wa kusini kwa ajili ya ziara ya kuwatembelea wahanga wa madhara yaliyosababishwa na mvua.
 KATIBU wa NEC, Idara ya Organazesheni CCM Zanzibar Ndugu Bakari Hamad Khamis, akizungumza na Wana CCM na viongozi wa SMZ wa Mkoa Kusini Unguja katika ziara yake ya kukagua maeneo yaliyoathiriwa na mvua.



 MWENYEKITI wa CCM Mkoa wa kusini Unguja Ndugu Ramadhan Abdalla Ali  akizungumza katika kikao cha dharura kabla ya kuanza ziara ndani ya Mkoa huo.

 MKUU wa Mkoa Kusini Ungua Hassan Hatib Hassan ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya siasa ya CCM Mkoa akitoa tathimini ya athari ya mvua ndani ya Mkoa huo.

 VIONGOZI mbali mbali wakiwemo WANEC na wajumbe wa Kamati ya Siasa ya Mkoa huo wakifuatilia kwa makini kikao hicho.

 MAAFISA kutoka Afisi Kuu ya CCM Zanzibar walioshirikim ziara hiyo wakifuatilia kwa makini masuala mbali mbali yanayofanyika katika kikao hicho.

 NYUMBA iliyoezuliwa na upepo inayomilikiwa na Seif Salum katika kijiji cha Paje Mkoa wa Kusini Unguja.



 MITI mbali mbali iliyong'olewa na upepo ulioambatana na mvua katika shehia ya Michamvi Mkoa wa Kusini Unguja.


 KITUO cha Afya cha Michamvi kilichoezuliwa na upepo.


NA IS-HAKA OMAR,ZANZIBAR.


CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) imeitaka serikali kuwachukulia hatua za kisheria baadhi ya wananchi wanaojenga kwa makusudi katika mabonde na miundombinu ya maji.

Pia imetaka baadhi ya viongozi wa wadi na shehia ambao ni madiwani na masheha, wanaoshindwa kudhibiti ujenzi holela na vitendo vya uharibifu wa mazingira katika maeneo yao, wawajibishwe kwa mujibu wa sheria.

Ushauri huo umetolewa na Katibu wa NEC, Idara ya Organazesheni CCM Zanzibar  Bakari  Hamad Khamis, alipotembelea maeneo yaliyoathiriwa na mvua za masika katika Mikoa ya Magharibi na Kusini Unguja.

Amesema wakati umefika wa Serikali kuondosha muhali na kuwachukulia hatua kali za kisheria wananchi wanaoharibu miundombinu kwa makusudi na kusababisha maji ya mvua kwenda sehemu zisizostahiki na hatimaye kusababisha mafuriko.

Amebainisha kuwa maeneo mengi yaliyopata majanga hayo yameonekana kuathiriwa na shughuli za kibinadamu zikiwemo uchimbaji wa mchanga, ujenzi holela  na ukataji wa miti ovyo.

Amesema kila mwaka serikali imekuwa ikitoa tahadhari na kuwataka wananchi waliojenga mabondeni wahamie maeneo salama lakini wamekuwa wakikaidi maelekezo hayo.

Amezitaka manispaa hadi Serikali kuu kuratibu maeneo yote yenye historia ya kupata mafuriko kila mwaka pamoja na kutafuta ufumbuzi wa kudumu juu ya changamoto hiyo.

Kupitia ziara hiyo amesema CCM imetoa pole wananchi wote waliopata maafa hayo na kuwataka kuwa wawe wavumilivu katika kipindi hiki kigumu na kitaisimamia Serikali kupitia mfuko wa maafa itoe msaada wa haraka kwa wahanga wa mafuriko hayo.

"CCM ipo bega kwa bega na wananchi wote waliopata maafa haya na tutajitahidi kushirikiana na serikali kuhakikisha hatua za dharura hasa misaada ya kibinadamu inawafikia walengwa.

Lakini pia wananchi nakuombeni sana tujenge utamaduni wa kujilinda na kuchukua tahadhari juu ya matukio kama haya, kwani kuna baadhi ya sehemu nimesikitika kuona nyinyi wenyewe ndio chanzo cha kusababisha mafuriko kutokana na uharibifu wa mazingira na miundombinu mingine", amesema Bakari.

Ameuagiza uongozi wa CCM na UVCCM Mkoa Magharibi kwenda kumsaidia shughuli za ujenzi wa nyumba Mwenyekiti wa CCM Tawi la Buyu Ndugu Matias Theodori ambaye nyumba yake imeporomoka kutokana na mvua hizo.

Akitoa katika ziara hiyo Katibu wa CCM Mkoa wa Magharibi Aziza Mapuri, amesema mvua zinazoendelea kunyesha katika Mkoa huo zinasababisha madhara makubwa kwa wananchi na mali zao na Chama kipo karibu na wananchi wote waliopata maafa hayo.

 Naye Diwani wa wadi ya Pangawe Makame Pandu Mgana ambaye wadi yake ni miongoni mwa sehemu zilizoathiriwa na mvua hizo, amesema kwa kushirikiana na uongozi wa jimbo wanafanya juhudi za kuifanyia matengezo mitaro iliyozibwa kwa shughuli za ujenzi na baadhi ya wananchi.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa Kusini Hassan Hatib Hassan, amesema jumla ya nyumba 106 katika maeneo mbali mbali ya Mkoa huo zimeharibiwa na mvua iliyonyesha April 16, mwaka 2018.

Amesema mbali na nyumba hizo kuna miti ya matunda na ya kawaida, migomba pamoja na mazao ya kilimo yameharibiwa na mvua hizo zilizochanganyika na upepo.

Ameeleza kuwa katika juhudi za kuwafariji wananchi waliopata maafa hayo, uongozi wa Mkoa unaendelea na juhudi ya kuratibu maeneo yote yaliyopata majanga ili mamlaka inayohusika na masuala ya maafa iweze kuchukua hatua za haraka.

Akizungumza katika shehia ya Michamvi Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kusini Unguja, Ramadhan Abdallah Ali amesema Chama Cha Mapinduzi katika Mkoa huo kitaendelea kushirikiana na wananchi wote waliopata maafa hayo mpaka watakaporudi katika hali za kawaida za kuendelea na harakati za kimaendeleo.


Maeneo yaliyotembelewa ni Magogoni kwa mabata, Pangawe, Fuoni jangamizi, Fuoni chunga, Dimani Tasaf, Mtoni kidatu juu,Buyu pamoja na shehia ya michamvi na Paje.