Jumanne, 27 Februari 2018

BI.CATHERINE AVITAKA VYOMBO VYA HABARI KUONGOZA MAPAMBANO YA VITA YA UDHALILISHAJI WA KIJINSIA

 KATIBU wa Kamati Maalum ya NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar  Bi. Catherine Peter Nao akizungumza na viongozi na watendaji wa Zenj Fm Radio katika ziara yake kwenye vyombo vya Habari Zanzibar.

 MENEJA wa Zenj Fm Winifrida Mayao(kushoto) Meneja Mkuu wa Zanzibar Media Corperations Ramadhan Sender(kulia) wakizungumza na wageni kutoka Afisi Kuu CCM Zanzibar wakiongozwa na Mkuu wa Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar Bi.Catherine Peter Nao.

 KATIBU wa Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar Bi.Catherine Peter Nao (kulia) akizungumza na Mkurugenzi Iland Media Group  Bw.Fauz Abdul Razaki (kushoto).
 KATIBU wa Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar Bi.Catherine Peter Nao, akiwa katika studio za Zenj Fm.

Mkurugenzi Iland Media Group  Bw.Fauz Abdul Razak (kushoto), akitoa ufafanuzi wa vifaa vya kurushia matangazo ya TV katika Chumba maalum cha kuzalisha vipindi.

 BAADHI ya wafanyakazi wa Coconut Fm Radio wakiwa katika Chumba Cha Habari mara baada ya kuupokea Ugeni kutoka CCM ulioongozwa na Katibu wa Idara ya NEC, Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar  Bi.Catherine Peter Nao aliyetembelea Radio hiyo.
 Katibu wa Idara ya NEC, Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar  Bi.Catherine Peter Nao akiwa katika Studio za Coconut Fm Radio iliyopo Migombani Mnara wa Mbao Zanzibar.


 Muhariri Mkuu Mtendaji wa Bomba Fm Radio Mwinyi Sadala (wa tatu kulia) akiwakaribisha wageni hao walioongozwa na Katibu  wa Kamati Maalum ya NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar  Bi. Catherine Peter Nao katika mwendelezo wa ziara.

 KATIBU msaidizi Mkuu  Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar Daud Ismail Juma akitambulisha maafisa mbali mbali wa CCM waliofustana na Mkuu wa Idara hiyo.

 Katibu  wa Kamati Maalum ya NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar  Bi. Catherine Peter Nao akiwa katika studio za Bomba Fm Radio.
 Kamati Maalum ya NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar  Bi. Catherine Peter Nao (kushoto) akizungumza na Bw. Aziz(kulia)  Mkuu wa udhibiti wa fedha wa Bomba FM Radio. 
Katibu  wa Kamati Maalum ya NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar  Bi. Catherine Peter Nao katika mwendelezo wa ziara, akiwa katika Chumba Cha kuzalisha Vipindi vya Iland TV.



 MKUU wa Vipindi  Tifu TV Bw. Mwanjie Saleh Mgeni (kulia wa mwanzo) akitoa ufafanuzi juu wa chumba cha matangazo cha Tifu TV, Katibu wa Idara ya Itikadi na Uenezi akifuatilia kwa makini maelezo hayo.
 Chumba cha kurushia matangazo cha Tifu TV.
 Meneja Mkuu wa Tifu TV  Bw.Abdalla Kesi Shaaban(kulia) akizungumza na Katibu  wa Kamati Maalum ya NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar  Bi. Catherine Peter Nao akizungumza na viongozi na watendaji wa Zenj Fm Radio katika ziara yake kwenye vyombo vya Habari Zanzibar.



NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.


KATIBU wa Kamati Maalum ya NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar Catherine Peter Nao amesema Vyombo vya Habari ni taasisi muhimu zinazotakiwa kuwa mstari wa mbele kukemea na kuibua vitendo vya udhalilishaji wa wanawake na watoto ili wahalifu wa matukio hayo waweze kuchukuliwa hatua kali za kisheria.

Kauli hiyo ameitoa katika mwendelezo wa ziara yake kwenye Vyombo vya Habari nchini, amesema taasisi hizo zenye dhamana ya kuelimisha,kuburudisha,kukosoa na kushauri zina jukumu kubwa la kueleza kwa upana athari mbaya zinazotokana na vitendo hivyo.

Alisema Chama Cha Mapinduzi kitaendelea kuishauri serikali na wadau mbali mbali wa haki za binadamu kutekeleza wajibu wao wa kuvisimamia vyombo vya kisheria kuharakisha uendeshaji wa kesi hizo na kutoa hukumu kali kwa watu wanaotiwa hatia kwa makosa hayo.

Pia, alilitaka Jeshi la Polisi nchini kuondokana na mfumo duni wa upelelezi juu ya kesi za udhalilishaji badala yake waongeze kasi na kutumia weledi na uaminifu kama kanuni na miongozo ya jeshi hilo inavyowaelekeza.

Katibu huyo alisema tayari serikali imeanza kuchukua hatua ikiwemo Baraza la wawakilishi kupitisha mswaada wa sheria mpya ya mwaka 2018, inafuta sheria ya adhabu kwa makosa ya jinai ya mwaka 2004, hivyo baada ya Rais wa Zanzibar kuitia saini na kuwa sheria kamili kinachobaki ni wananchi na wadau wengine kuunga mkono juhudi hizo.

“ CCM ni taasisi inayojali misingi ya haki za binadamu na utu kwa watu wote bila kujali tofauti za kisiasa, hivyo hawezi kubaki kimya huku nchi yetu inaendelea kuangamia kwa vitendo viovu vya ubakaji kila sehemu, ni muhimu kila mtu kupambana kwa nafasi yake ili tuondoshe janga hili.

Lakini pia taasisi zinazosimamia masuala ya utekelezaji wa Kisheria sasa tunawambia huu ndio muda wa kujitathimini na kufanya kazi vinginevyo Chama Cha Mapinduzi kitachukua hatua kali za kimaadili kwa baadhi ya viongozi wakuu wa Taasisi hizo ambao hawatekelezi wajibu wao kiutendaji”, alisema Bi,Catherine.

Hata hivyo alieleza kuwa Zanzibar haikuwa na utamaduni wa kesi za aina hiyo lakini vitendo hivyo vimeongezeka kutokana na utandawazi unaopelekea baadhi ya wananchi kuacha utamaduni wa asili na kuiga masuala ya kigeni.

Akizungumzia mchango wa vyombo vya Habari katika ukuaji wa Demokrasia, Catherine amesema taasisi hizo za kihabari zimekuwa mstari wa mbele kuandika na kuripoti vipindi, makala na habari mbali mbali za kisiasa zinazochangia ukuaji wa kidemokrasia kwa wananchi.

Alisema Vyombo vya habari  sio tu kutangaza  habari za kisiasa bali hata katika ukuaji wa kiuchumi wa Zanzibar taasisi hizo zimechangia kutangaza  fursa za nchi  katika anga za kimataifa hasa utaliii na zao la karafuu na kusaidia ukuaji wa pato la taifa unaotokana na upatikanaji wa fedha za kigeni.

Pamoja na hayo alisema lengo la ziara hiyo ni kujitambulisha,kubadilishana mawazo, kujenga mahusiano  kwa vyombo hivyo ambavyo ni wadau wakubwa wa CCM katika masuala ya kueneza Itikadi na Habari za Chama kwa wananchi.

Ameahidi kuendelea kufanya kazi na ukaribu na vyombo vya Habari mbali mbali na kuvishauri vielekeze nguvu zake sehemu za kijamii hasa za vijijini kuibua kero zinazowakabili wananchi ili taasisi husika zitafute ufumbuzi wa kudumu.

Naye  Meneja wa Radio ya Zenj Fm, Winifrida Mayao amekipongeza Chama Cha Mapinduzi kwa busara zake za kuendeleza mahusiano ya kiutendaji na Kituo hicho.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Iland Media Group, Hatwab Mbarouk Khamis ameeleza kuwa ziara hiyo imefungua milango ya kiutendaji baina ya Kituo Chake na CCM.

Akizungumza Muhariri Mkuu Mtendaji wa Bomba Fm Radio, Mwinyi Sadala amesema Kituo hicho kimekuwa ni mdau mkubwa wa kuripoti na kuandika habari za kisiasa, kijamii na kiuchumi zinazohamasisha dhana ya Utawala bora, Demokrasia, uhuru wa kutoa na kupokea maoni kwa wananchi.

Hata hivyo Sadala alikishauri Chama hicho kuwakumbusha baadhi ya Wabunge, wawakilishi,Madiwani na viongozi wengine wa Serikali ambao bado hawajatekeleza  ahadi walizotoa katika Uchaguzi Mkuu uliopita, kutumia wakati huu kutekeleza ahadi hizo kwa lengo la kurejesha matumaini ya jamii.

Ziara hiyo imeendelea katika Vyombo vya Habari mbali mbali ikiwemo Zenj Fm, Coconut Fm, Iland TV, Bomba Fm na Tifu TV.


Jumatatu, 26 Februari 2018

NDG.CATHERINE AANZA ZIARA KATIKA VYOMBO VYA HABARI ZANZIBAR

KATIBU wa  Kamati Maalum ya NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar, Catherine Peter Nao (kushoto)  akikaribishwa katika Ofisi za Kituo Cha Radio ya Hits FM Radio katika ziara yake ya kutembelea Vyombo vya Habari Zanzibar.
 KATIBU wa  Kamati Maalum ya NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar, Ndugu
Catherine Peter Nao (kushoto)  akiwa pamoja na Katibu msaidizi Mkuu wa Idara hiyo , Ndugu Daud Ismail Juma.



VIONGOZI wa Hits FM Radio wakibadilishana mawazo na viongozi wa Afisi Kuu ya CCM Zanzibar kutoka Idara ya Itikadi na Uenezi waliotembelea kituo hicho.

 MENEJA Mkuu wa Hits FM Radio Hafidh Kassim pamoja na Mkuu wa Utawala wa Kituo hicho wakifuatilia kwa makini mazungumzo na viongozi wa CCM waliofika katika kituo hicho kwa lengo la mazungumzo.

 MKUU wa Vipindi Hits FM Radio Bi.Zuhura Hussein(kushoto) akiwa pamoja na Mhariri Mkuu wa Kituo hicho Bi. Moza Saleh(kulia) wakifuatilia kwa makini kikao hicho.

 MKUU wa Vipindi Zuhura Hussein (kushoto  wa kwanza aliyevaa miwani) akieleza kazi mbali mbali zinazofanyika katika Studio ya Hits FM Radio ambapo Katibu wa NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar  Bi. Catherine Peter Nao( wa kwanza kulia) akimsikiliza kwa makini Mkuu wa vipindi.

 MKUFUNZI wa mafunzo na utafti kwa watendaji wa Hits FM Radio Bi. Kudra Mawazo akiwa katika Chuma Cha Habari cha Kituo hicho mara baada ya kutembelewa na watendaji hao wa CCM.

 MHARIRI Mkuu wa Mwenge FM Radio Bw. Haji Ramadhan Suwed akizungumza mara baada ya kutembelewa na KATIBU wa Kamati Maalum ya NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar Ndugu Catherine Peter Nao, aliyefika katika Kituo hicho kwa lengo kujitambulisha na kubadilishana mawazo.

 MKURUGENZI wa Mwenge FM Radio  Bi. Badria Atai Masoud (wa kwanza kushoto) akizungumza na kuwatambulisha watendaji wake kwa Ujumbe uliowatembelea Kutoka Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar.

 WATENDAJI mbali mbali wa Mwenge FM Radio wakiwa katika Kikao hicho.

WATENDAJI wa Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar wakiwa katika Studio za Mwenge FM Radio.

 PICHA ya pamoja na viongozi na Watendaji wa Mwenge FM Radio na  Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar.


 MKURUGENZI wa Bahari FM Radio Yussuf Omar Chunda (wa pili kushoto aliyevaa chati nyeupe yenye mistari) akizungumza na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar Bi. Catherine Peter Nao na watendaji wengine waliotembelea  Kituo hicho cha Habari Kinachomilikiwa na Chama Cha Mapinduzi

 Mkuu wa Utawala wa Kituo hicho Bw. Ali Ndota(kulia aliyesimama) akiwasilisha masuala mbali mbali ya utawala katika Radio hiyo, kwa Katibu wa NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi Zanzibar.

 BAADHI ya Wafanyakazi wa Bahari FM Radio wakiwa katika kikao cha pamoja na ujumbe wa Idara ya Itikadi na Uenezi waliotembelea Radio hiyo.
KATIBU wa Kamati Maalum ya NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar Bi. Catherine Peter Nao (katikati) akizungumza na wafanyakazi na Kituo hicho.


 MTANGAZAJI wa Kipindi Cha Michezo wa Kituo hicho Bi. Donisya Thomas akizuingumzia masuala mbali mbali ya kiutendaji ndani ya Radio hiyo.


VYOMBO vya Habari nchini vimeshauriwa kufuatilia na kuwahoji viongozi mbali mbali wa Serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM) hasa Mawaziri, Wabunge, Wawakilishi na Madiwani ili kujua ni kwa kiwango gani Chama kimeisimamia Serikali kutekeleza iIlani ya Uchaguzi ya mwaka 2015/2020.

Rai hiyo imetolewa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi ya Chama Cha Mapinduzi Zanzibar, Bi. Catherine Peter Nao katika ziara yake ya mwanzo kwa Vyombo vya habari Zanzibar  toka ateuliwe kuongoza Idara hiyo.

Akizungumza viongozi na watendaji wa Vyombo hivyo ambavyo ni Bahari Fm Radio, Hits Fm Radio iliyopo Migombani pamoja na Mwenge FM Radio, alisema Serikali ya Awamu ya Saba chini ya uongozi wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein inatekeleza kwa ufanisi na kwa kasi kubwa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020.

Katibu huyo aliendelea kufafanua kwa kueleza kuwa licha ya utekelezaji huo bado baadhi ya Vyombo vya Habari vimekuwa  haviandiki wala kuripoti utekelezaji huo hasa uimarishaji wa Huduma za msingi za kijamii zikiwemo Afya, Elimu, Kilimo, Uvuvi, ujenzi wa mitandao ya kisasa ya Barabara, uimarishaji wa miundombinu ya Anga pamoja na miundombinu ya Baharini.

Ameeleza kuwa CCM inathamini sana mchango wa Vyombo vya Habari nchini vinavyotoa habari na taarifa muhimu za Chama na Serikali bila upendeleo na ubaguzi huku vikifuata maadili kwa mujibu wa miongozo ya Tasnia ya Habari.

Alisema lengo la ziara hiyo ni kubadilishana mawazo na kujenga mahusiano endelevu baina ya Chama na Taasisi hizo za Kihabari nchini ili wananchi waweze kupata taarifa sahihi zinazohusu CCM.

Pamoja na hayo amesema CCM ili iweze kuendelea kufanya vizuri katika medali za kisiasa,  ni lazima iwe karibu na vyombo vya Habari ambavyo ni wadau wakubwa wa kuhabarisha, kuelimisha na kuibua kero na changamoto zinazoikabili jamii.

“ Leo nimefurahi sana kukutana na waandishi wa habari tukaweza kubadilishana mawazo na uzoefu, lakini pia wito wangu kwenu fuatilieni utekelezaji wa Ilani ya CCM ili muweze kuwambia wananchi uhalisia juu ya mambo yaliyotekelezwa na Serikali chini ya usimamizi wa CCM.

Pia suala la kulinda maadili na miiko yenu ya Kitaaluma ni jambo muhimu kwa maendeleo ya taasisi zetu na taifa kwa ujumla”, amesema Catherine.

Pamoja na hayo aliahidi kuendelea kushirikiana na waandishi wa Habari kwa lengo la kuwarahisishia kazi zao na kupata taarifa za CCM kwa wakati mwafaka.

Akitoa ufafanuzi juu ya baadhi ya malalamiko yaliyotolewa na watendaji wa vyombo vya Habari kwa kutopewa ushirikiano na baadhi ya Watumishi wa umma wenye dhamana ya kutoa taarifa kwa jamii, alisema changamoto hiyo ataitafutia ufumbuzi wa haraka ili viongozi wenye tabia hizo kujirekebisha na kutekeleza wajibu wao kwa mujibu wa Katiba ya Chama ya mwaka 1977 na Katiba ya Zanzibar ya mwaka1984.

Nao baadhi ya viongozi wa Vituo hivyo vya Radio wameeleza masikitiko yao kwa Katibu huyo, kwa kile walichodai kuwa baadhi ya Mawaziri ndani ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na baadhi ya viongozi wa Chama hawatoi ushirikiano pale wanapotakiwa na Vyombo hivyo na kupelekea Habari kutokuwa na uwiano sawa wa Vyanzo vya Kihabari.

Akizungumza Meneja wa Hits FM Radio iliyopo Migombani Unguja, Hafidh Kassim amesema licha ya Vyombo vya Habari nchini kukabiliwa na changamoto mbali mbali bado wanaendelea kutekeleza majukumu yao ya msingi ya kutoa habari sahihi na zilizofanyiwa utafti wa kina kwa jamii.
Naye Mhariri Mkuu wa Mwenge FM Radio, Haji Ramadhan Souwed alizitaja changamoto zinazowakabili katika Kituo hicho kuwa ni pamoja na ukosefu wa baadhi ya vifaa vya kurusha matangazo yao ili yafike katika masafa ya mbali kama zilivyo Radio zingine na kuwaomba wadau, wafanyabishara na watu wenye uwezo kuwasaidia ununuzi wa vifaa hivyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Bahari FM Radio iliyopo Migombani Unguja , Yussuf Omar  Chunda alisema changamoto waliyonayo ni ukosefu wa matangazo ya biashara hali inayopelekea kituo hicho vyanzo vya mapato vya uhakika.

Ziara hiyo inaendelea kesho katika vyombo mbali mbali vya habari vilivyopo nchini.

Jumamosi, 24 Februari 2018

WANASIASA WAKONGWE NA WAASISI WA UWT WASISITIZA MAGEUZI YA KIUTENDAJI

 MAKAMU Mwenyekiti wa UWT Taifa Ndugu Thuwayba Kisasi akiongoza msafara wa Umoja huo katika mwendelezo wa ziara ya kuwatembelea waasisi wa UWT katika Mkoa wa Magharibi Unguja, huko Mbweni kwa Mwanasiasa Mkongwe Bi. Rufea Juma Mbarouk.

 MWENYEKITI wa UWT Mkoa wa Magharib Ndugu Zainab Ali Maulid akizungumza nyumbani kwake muasisi huyo.
 KAIMU Naibu Katibu Mkuu wa UWT anayefanyia kazi zake Zanzibar Ndugu Tunu Kondo akizungumza kabla ya kumkaribisha Makamu Mwenyekiti kuzungumza na muasisi Bi.Rufea 



 WATENDAJI wa UWT wa ngazi mbali mbali wakiwa katika ziara hiyo nyumbani kwake Bi.Rufea.

 MUASISI wa UWT Bi.Rufea Juma Mbarouk(kushoto) akizungumza na viongozi mbali mbali wa UWT waliofika nyumbani kwake kwa lengo la kumtembelea.

 MAKAMU Mwenyekiti wa UWT Taifa Thuwayba Kisasi(kulia) akimkabidhi bahasha yenye zawadi Muasisi huyo Bi.Rufea Juma Mbarouk (kushoto).

 VIONGOZI na Watendaji wa UWT wakiomba dua nyumbani kwake Bi.Rufea.


 MJUMBE wa Baraza la Wadhamini wa CCM Taifa Bi.Mariam Hengwa(aliyekuwa katikati pichani) akitoa nasaha kwa Uongozi wa UWT uliofika nyumbani kwake kwa Mchina Mwisho kwa ajili ya kumtembelea.

  MAKAMU Mwenyekiti wa UWT Taifa Thuwayba Kisasi(kushoto) akimkabidhi bahasha yenye zawadi Muasisi huyo Bi.Mariam Hengwa (kulia).
 VIONGOZI wa UWT wakiomba Dua pamoja na Bi.Mariam Hengwa. 

 VIONGOZI wa UWT wakiwa nyumbani kwake muasisi wa Umoja huo Bi.Salama Majaliwa huko Mwera.

  MAKAMU Mwenyekiti wa UWT Taifa Thuwayba Kisasi(kushoto) akizungumza na muasisi wa UWT Bi.Salama Majaliwa, hapa Nyumbani kwake Mwera.
 MAKAMU Mwenyekiti wa UWT Taifa Ndugu Thuwayba Kisasi(kushoto) akimkabidhi bahasha yenye zawadi muasisi huyo Bi.Salama Majaliwa(kulia).



NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.

VIONGOZI na watendaji wa Umoja wa Wanawake wa Chama cha Mapinduzi (UWT) Tanzania wameshauriwa kuendeleza utamaduni wa kuwatembelea wananchi ili kuibua kero zinazowakabili na kuzifanyia kazi kwa mujibu wa matakwa ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya  mwaka 2015/2020.

Pia wametakiwa kuzitendea haki dhamana za uongozi walizonazo katika medali za kisiasa kwa kuhakikisha CCM inazidi kuwa Chama bora na imara chenye sera , taratibu na misingi ya maadili yanayokidhi matakwa ya wananchi wote bila ya ubaguzi wa kidini na kikabila.

Ushauri huo umetolewa kwa wakati tofauti na Waasisi na viongozi wa zamani wa UWT katika mwendelezo wa ziara ya Makamu Mwenyekiti wa Umoja huo Taifa Ndugu Thuwayba Kisasi, katika Mkoa wa Magharibi Unguja.

Akizungumza mwasisi wa UWT aliyewahi kushika nyadhifa mbali mbali ndani Umoja huo na Mjumbe wa Baraza la Wadhamini wa CCM Taifa Bi.Mariam Hengwa (75) hapo nyumbani kwake kwa Mchina mwisho, amesema Chama Cha Mapinduzi kipo ngazi za chini kwa wananchi hivyo viongozi hao wapange utaratibu wa kuwatembelea wananchi mara kwa mara.

Bi. Mariam amesema viongozi wa UWT wanatakiwa kubuni mipango mbali mbali ya kimaendeleo itakayoongeza Ari na utendaji kwa Akina Mama wa Umoja huo, na kuwavutia wanawake wa upinzani kujiunga na CCM.

Hata hivyo amewakumbusha kuwa ni lazima viongozi hao wawe na mbinu mpya za kuwasimamia watendaji kwa lengo la kuondokana na mfumo wa kufanya kazi kwa mazoea.

Kwa upande wake mwanasiasa mkongwe visiwani Zanzibar na muasisi wa UWT Bi. Rufea Juma Mbarouk (73), amesema njia ya pekee ya kurejesha hadhi na heshima ya UWT ni Akina mama hao kuacha tabia za fitna, majungu na kauli za kuchafuana kisiasa  badala yake washikamane na kulinda maslahi ya  Chama.

Bi.Rufea aliyewahi kushika nyadhifa ndani ya SMZ na Chama Cha Mapinduzi, amesema enzi za uongozi wake wanawake walikuwa kitu kimoja wakipendana na kushirikiana kwa kila jambo, ndio maana taasisi hiyo ilivuka vikwazo na changamoto za kisiasa na imebaki salama na  kuwa na heshima kitaifa na kimataifa.

“ Viongozi, watendaji na wanachama wote wa UWT  acheni tabia na ubinafsi usiokuwa na faida kwa Chama na Umoja wetu, fanyeni kazi kwa bidii na mtambue kuwa CCM inakutegemeeni sana”, aliwasihi viongozi hao Bi. Rufea.

Naye Bi.Salama Majaliwa ambaye ni miongoni mwa waasisi wa Umoja huo, alisema UWT imekuwa taasisi yenye nguvu toka enzi za Afro-Shiraz Party(ASP), ambapo Akina mama walikuwa mstari wa mbele katika kupigania demokrasia ndani na nje ya CCM.

Bi.Salama ameeleza kwamba licha ya kuwepo na mabadiliko ya mfumo wa kisiasa ni lazima viongozi wa UWT waliopo hivi sasa madarakani wasome alama za nyakati na kufanya siasa zinazoendana na mahitaji ya wananchi.

Pamoja na hayo muasisi huyo amesisitiza suala la mshikamano kwa UWT huku akiwakumbusha jukumu la msingi la Chama Chochote cha kisiasa ni kushinda kwa kila uchaguzi na ibara ya tano(5) ya Katiba ya CCM inaelekeza suala hilo, hivyo ni jukumu la Umoja huo kuhakikisha Chama Cha Mapinduzi kinashinda na kuendelea kuongoza dola mwaka 2020.

Pia Waasisi hao wamekiri kuwa Makamu Mwenyekiti Thuwayba Kisasi ni kiongozi wa mwanzo aliyewatembelea kwa lengo la kuomba ushauri na mazungumzo, na wakawataka viongozi wa Chama na Jumuiya nyingine kufuata nyayo hizo zenye dhamira ya kuleta mageuzi ya kimaendeleo ndani na nje ya taasisi hiyo.

Akitoa tathimini ya ziara hiyo Makamu Mwenyekiti wa Umoja huo Taifa Ndugu Thuwayba Kisasi, ameahidi kuzifanyia kazi kwa vitendo nasaha, maelekezo na ushauri uliotolewa na viongozi hao wa zamani ili kujenga Jumuiya na Chama yenye nguvu kisiasa, kiuchumi na kijamii.

Amesema lengo la ziara hiyo ni kuwatembelea na kuwakagua waasisi wa Chama, Serikali na Jumuiya kwa kujifunza mambo mengi ya kiuongozi na kiutendaji kutoka kwao.

Pia ameeleza kuwa miongoni mwa tunu ya kujivunia kutoka kwa viongozi hao ambao ni Akina mama ni kupigania Demokrasia na misingi ya usawa ndani ya CCM, iliyowawezesha wanawake kusimama wenyewe na kupata nafasi za uongozi katika Chama na Serikali.

Mapema akizungumza Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa UWT Zanzibar Ndugu Tunu Kondo, amesema Umoja huo unathamini na kuwaenzi wastaafu mbali mbali kwani nguvu na maarifa yao ndio matunda yanayowanufaisha wanachama na wananchi kwa ujumla.

Ijumaa, 23 Februari 2018

CCM YAIFARIJI FAMILIA ILIOPATA AJALI MOTO ZANZIBAR



CHAMA Cha Mapinduzi(CCM),Zanzibar, kimetoa mkono wa rambirambi kwa familia ya mtoto aliyefariki, Tarik Abubakari,(3) baada ya nyumba kungua, Magomeni, visiwani humu.

Akitoa mkono wa pole kwa niaba ya Chama, Katibu wa Idara ya Mambo ya Siasa, Ushirikiano wa Kimataifa,Maalim Kombo Hassan Juma , kwa familia hiyo alisema CCM imesikitishwa sana  na tukio hilo la ajali ya moto ambalo lilitokea mnamo Februari 16, mwaka huu na kusababisha kifo cha mtoto.

Katika maelezo yake Katibu huyo aliongeza kuwa kwa niaba ya CCM, idara hiyo imeona ni vyema kufika kwa familia hiyo na kuungana nao ili kuwapa faraja kutokana na tukio hilo.

"Tulipata taarifa kutoka kwenye vyombo vya habari kuwa kumetokea tukio la ajali ya moto ambalo lilisababisha kutokea kwa kifo cha mtoto wa kiume hivyo tumekuja kutoa ubani ambao kwa namna moja ama nyingine itasaidia,"alisema.

Kwa upande wake akitoa shukrani kwa niaba ya familia, Hamis Salum Nassor, alishukuru kwa CCM kwa namna tukio hilo walivyolichukuliwa kwa uzito mkubwa na namna walivyoguswa.

Alisema kitendo cha CCM kufika kuwatembelea familia hiyo ni faraja kubwa kwao na kwamba imewapa imani ya kuwa na subira kwa wakati ambao ni mgumu.

"Tunachosema kwa niaba ya familia ni kiwa kama babu wa mtoto aliyefariki tunawashukuru sana CCM kwa namna mlivyochukulia swala hilo uzito na kipeumbele hivyo tunaomba mungu atupewe wepesi wake,"alisema.