Alhamisi, 15 Desemba 2016

CCM YAFANYA UTEUZI WA MGOMBEA MBUNGE WA JIMBO LA DIMANI




KAMATI  Kuu ya CCM Zanzibar  imemteuwa   Juma Ali Juma kuwa mgombea Ubunge kwa Tiketi  ya Chama  hicho katika Jimbo la Dimani, Wilaya ya Magharibi  “B” Unguja.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Vuai Ali Vuai aliwambia waandishi wa Habari kuwa uamuzi huo umefikiwa katika kikao cha Kamati hiyo iliyokutana jana chini ya Mwenyekiti wake ambaye pia ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dkt. Ali Mohamed Shein.

Alisema Kikao hicho ambacho kilikasimiwa madaraka na kikao Cha Halmashauri Kuu ya Taifa ya kufanya uamuzi huo, na wajumbe walipitia mapendekezo yaliyotolewa na vikao vya ngazi ya jimbo, wilaya na Mkoa juu ya wanachama 25 waliojitokeza kuwania nafasi hiyo.“ kikawaida halmashauri kuu ya taifa ndiyo inayofanya uteuzi wa mwisho, lakini  ilikasimu madaraka yake kwa kamati maalum baada ya kuomba ili kwenda na wakati uliopangwa.
Pia baada ya taratibu zote kwa ngazi husika kukamilisha hatimaye Kamati Maalum imefanya maamuzi ya mwisho ya kumpata Mgombea atakayeweza kupeperusha bendera ya CCM katika Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Dimani Unguja,”. Alisema  Vuai na kuongeza kuwa kazi iliyobaki kwa Sasa ni Wana CCM na Wananchi kwa ujumla wanaopenda maendeleo ya jimbo hilo kumuunga mkono mgombea huyo ili apate kushinda kwa kishindo .

Alieleza kuwa pamoja na wagombea wote waliochukua fomu kuomba nafasi hiyo  walikuwa na sifa lakini kutokana na utaratibu wa CCM umemteuwa mgombea mmoja ambaye atakayeweza kutumia tiketi ya Chama hicho katika uchaguzi huo na wagombea wengine ambao hawakubahatika kupata nafasi hiyo wasikate tamaa badala yake waendelee kukiunga mkono chama.

Vuai alieleza kuwa matarajio ya CCM katika Uchaguzi huo ni mgombea wa Chama hicho kushinda kwa kura nyingi kwani ana sifa na vigezo vinavyotakiwa na wananchi wa jimbo hilo ikiwemo uaminifu, weledi, utendaji bora na hana sifa za ufisadi wala tuhuma yoyote mbaya kwa jamii.

Aliongeza kwamba jukumu la kampeni za Uchaguzi wa jimbo hilo utasimamiwa na Mkoa wa Magharibi kwa kushirikiana na Afisi Kuu CCM Zanzibar ili kuhakikisha mgombea wake anashinda na kuendelea kuandika historia ya CCM katika uwanja wa siasa za ndani na nje ya nchi.

Aidha aliwasihi  wafuasi wa chama hicho na wananchi kwa ujumla kukiunga mkono chama hicho kuanzia kampeni hadi Uchaguzi kwa lengo la kuhakikisha CCM inashinda ili iweze kuendeleza utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM ya mwaka 2015/2016 katika jimbo hilo.
Akijibu hoja za baadhi ya waandishi wa Habari kuhusu ushiriki wa Chama cha CUF chini ya mwavuli wa UKAWA katika Uchaguzi wa Jimbo hilo, Vuai alifafanua kwamba CCM inafurahi kuwepo na Chama cha Upinzani  katika uchaguzi huo kwani itaongeza ushindani pamoja na hamasa kwa chama cha mapinduzi  kuendelea kufanya siasa za kistaarabu na kujitathimini kisiasa.

Pamoja na hayo alieleza kuwa viongozi, wanachama na watendaji wa CCM wameelimishwa vizuri juu ya kuepuka athari za makundi baada ya kumalizika hatua ya kura za maoni  ambapo kwa sasa wanachama wote wanasimama kwa timu moja ambayo ni Chama Chama Mapinduzi kwa kuhakikisha mgombea aliyeteuliwa anashinda kwa kura nyingi.

Kwa masikitiko makubwa Naibu Katibu Mkuu huyo alitumia nafasi hiyo kuwaeleza waandishi wa habari juhudi zilizofanywa na aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo Marehemu Hafidh Ali Tahir kuwa alikuwa ni kiongozi bora aliyepigania maendeleo ya wananchi wa jimbo lake na jamii kwa ujumla bila kuchoka.
 
Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Dimani unafanyika baada ya aliyekuwa Mwakilishi wa Jimbo hilo Hafidh Ali Tahir, kupitia tiketi ya CCM kufariki dunia mapema mwaka huu baada ya kuuguwa ghafla akiwa Mbungeni Dodoma.

Kutokana na kifo hicho Tume ya Uchaguzi ya Taifa Tanzania (NEC), tayari imetangaza kufanyika kwa uchaguzi mdogo , January 22 mwakani.

"KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI"

.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni