Jumatatu, 2 Januari 2017

NAIBU KATIBU MKUU WA CCM ZANZIBAR NDUGU VUAI ALI VUAI PAMOJA NA WATUMISHI WA CCM ZANZIBAR WAKIFANYA USAFI KUELEKEA MAADHIMISHO YA MIAKA 53 YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar kimewataka wananchi, wanachama, viongozi na watumishi wa Chama na Jumuiya zake  kufanya suala la Usafi wa Mazingira kuwa utamaduni wa kudumu ili kuenzi Mapinduzi ya mwaka 1964 kwa vitendo.

Rai hiyo imetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai wakati akifanya usafi wa Mazingira kupitia Tawi la CCM la Afisi Kuu Zanzibar Kisiwa Ndui lililopo katika maeneo ya Ofisi hiyo, Mjini hapa.

Alifafanua kwamba suala la usafi wa mazingira nchini lifanyike kwa ushirikiano wa wananchi wote bila ya kujali tofauti zao za kidini, kisiasa na kikabila kwani panapotokea athari mbaya zinazotokana na uchafu zinawakumba jamii nzima. 

Alisema usafi wa mazingira ni miongoni mwa mambo muhimu yaliyokuwa yakisisitizwa na waasisi wa Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964, kwa lengo la kuweka mazingira katika hali ya usafi na haiba nzuri kwa kuepusha jamii na maradhi ya miripuko.

Alisema  Chama Cha Mapinduzi Pamoja na kufanya kazi za kisaiasa bado  kina jukumu la kuhamasisha wafuasi wa chama hicho na wananchi kwa ujumla kuendeleza tabia ya kufanya usafi wa mara kwa mara katika maeneo wanayoishi.

“ Nakuombeni viongozi, wanachama, na watumishi pamoja na wananchi kwa ujumla suala la usafi lianzie katika mioyo yetu hadi katika mazingira tunayoishi, ili kuweka nchi yetu katika muonekano na haiba ya kuvutia wakati wote.

Pia leo tunafanya usafi kuungana na wananchi wengine katika maeneo mbali mbali wanaofanya shughuli mbali mbali za kuadhimisha miaka 53 ya Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964.”, alisema Vuai.

Hata hivyo alisema kuwa Chama hicho kwa sasa kina majukumu makubwa matano yanayotakiwa kutekelezwa kwa ufanisi yakiwemo Maadhimisho ya Sherehe za Mapinduza za kutimiza miaka 53 pamoja na kuadhimisha miaka 40 ya kuzaliwa kwa CCM ambazo kwa mwaka huu zinatarajiwa kufanyika Gombani Pemba.

Naibu Katibu Mkuu huyo, aliyataja majukumu mengine kuwa ni kufanikisha Uchaguzi Mdogo wa Jimbo la Dimani na kuhakikisha CCM inashinda, kufanyika Uchaguzi wa Chama mwaka 2017 na kupatikana viongozi bora wanaoendana na kasi za kiutendaji za chama hicho pamoja Uimarishaji wa Chama katika kutekeleza shughuli zake kuelekea mwaka 2020.

Naye Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wanawake wa CCM Tanzania( UWT), Salama Aboud Talib aliwasihi wanawake nchini kuwa mstari wa mbele katika kufanikisha shughuli za usafi kwani wao  ndio waathirika wakubwa pindi panapotokea majanga yanayotokana na athari za uchafuzi wa mazingira.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Tawi hilo, Nadra Juma Mohamed aliwapongeza Watendaji wa Afisi Kuu Zanzibar pamoja na viongozi wengine walioungana na watendaji hao kufanya usafi huo.

Alisema kufanyika kwa usafi huo ni miongoni mwa harakati za kuunga mkono Waasisi wa Mapinduzi walitoa sadaka maisha yao kwa ajili ya kupigania uhuru na kuondosha dhuruma zilizokuwa zikifanywa na wakoloni dhidi ya waafrika nchini.

“ Tawi la CCM Afisi Kuu Kisiwandui tumekuwa tukifanya usafi na shughuli zingine za kijamii mara kwa mara katika maeneo yetu kwa lengo la kuhamasisha wanachama wenzetu kuiga mambo mema tuyayoyafanya katika maadhimisho haya.”, alieleza Nadra.

Akizungumza Katibu wa CCM Mkoa wa Mjini, Mohamed Nyawenga alisema suala la usafi wa mazingira liendane na kampeni ya kupiga vita uharibifu wa mazingira na miondombinu ya maji na barabara nchini.

Usafi huo uliofanyika katika maeneo ya Afisi Kuu Zanzibar chini ya maafisa wa Afisi hiyo wakishirikiana na viongozi na watendaji kutoka katika ngazi mbali mbali za Chama na Jumuiya zake ni miongoni mwa maadhimisho ya kutimiza miaka 53 ya Mapinduzi ya Zanzibar  ya mwaka 1964 yatakayofikia kilele chake mwaka January 12, mwaka 2017.












Hakuna maoni:

Chapisha Maoni