Alhamisi, 15 Desemba 2016

CCM YAFANYA UTEUZI WA MGOMBEA MBUNGE WA JIMBO LA DIMANI




KAMATI  Kuu ya CCM Zanzibar  imemteuwa   Juma Ali Juma kuwa mgombea Ubunge kwa Tiketi  ya Chama  hicho katika Jimbo la Dimani, Wilaya ya Magharibi  “B” Unguja.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Vuai Ali Vuai aliwambia waandishi wa Habari kuwa uamuzi huo umefikiwa katika kikao cha Kamati hiyo iliyokutana jana chini ya Mwenyekiti wake ambaye pia ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dkt. Ali Mohamed Shein.

Alisema Kikao hicho ambacho kilikasimiwa madaraka na kikao Cha Halmashauri Kuu ya Taifa ya kufanya uamuzi huo, na wajumbe walipitia mapendekezo yaliyotolewa na vikao vya ngazi ya jimbo, wilaya na Mkoa juu ya wanachama 25 waliojitokeza kuwania nafasi hiyo.“ kikawaida halmashauri kuu ya taifa ndiyo inayofanya uteuzi wa mwisho, lakini  ilikasimu madaraka yake kwa kamati maalum baada ya kuomba ili kwenda na wakati uliopangwa.
Pia baada ya taratibu zote kwa ngazi husika kukamilisha hatimaye Kamati Maalum imefanya maamuzi ya mwisho ya kumpata Mgombea atakayeweza kupeperusha bendera ya CCM katika Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Dimani Unguja,”. Alisema  Vuai na kuongeza kuwa kazi iliyobaki kwa Sasa ni Wana CCM na Wananchi kwa ujumla wanaopenda maendeleo ya jimbo hilo kumuunga mkono mgombea huyo ili apate kushinda kwa kishindo .

Alieleza kuwa pamoja na wagombea wote waliochukua fomu kuomba nafasi hiyo  walikuwa na sifa lakini kutokana na utaratibu wa CCM umemteuwa mgombea mmoja ambaye atakayeweza kutumia tiketi ya Chama hicho katika uchaguzi huo na wagombea wengine ambao hawakubahatika kupata nafasi hiyo wasikate tamaa badala yake waendelee kukiunga mkono chama.

Vuai alieleza kuwa matarajio ya CCM katika Uchaguzi huo ni mgombea wa Chama hicho kushinda kwa kura nyingi kwani ana sifa na vigezo vinavyotakiwa na wananchi wa jimbo hilo ikiwemo uaminifu, weledi, utendaji bora na hana sifa za ufisadi wala tuhuma yoyote mbaya kwa jamii.

Aliongeza kwamba jukumu la kampeni za Uchaguzi wa jimbo hilo utasimamiwa na Mkoa wa Magharibi kwa kushirikiana na Afisi Kuu CCM Zanzibar ili kuhakikisha mgombea wake anashinda na kuendelea kuandika historia ya CCM katika uwanja wa siasa za ndani na nje ya nchi.

Aidha aliwasihi  wafuasi wa chama hicho na wananchi kwa ujumla kukiunga mkono chama hicho kuanzia kampeni hadi Uchaguzi kwa lengo la kuhakikisha CCM inashinda ili iweze kuendeleza utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM ya mwaka 2015/2016 katika jimbo hilo.
Akijibu hoja za baadhi ya waandishi wa Habari kuhusu ushiriki wa Chama cha CUF chini ya mwavuli wa UKAWA katika Uchaguzi wa Jimbo hilo, Vuai alifafanua kwamba CCM inafurahi kuwepo na Chama cha Upinzani  katika uchaguzi huo kwani itaongeza ushindani pamoja na hamasa kwa chama cha mapinduzi  kuendelea kufanya siasa za kistaarabu na kujitathimini kisiasa.

Pamoja na hayo alieleza kuwa viongozi, wanachama na watendaji wa CCM wameelimishwa vizuri juu ya kuepuka athari za makundi baada ya kumalizika hatua ya kura za maoni  ambapo kwa sasa wanachama wote wanasimama kwa timu moja ambayo ni Chama Chama Mapinduzi kwa kuhakikisha mgombea aliyeteuliwa anashinda kwa kura nyingi.

Kwa masikitiko makubwa Naibu Katibu Mkuu huyo alitumia nafasi hiyo kuwaeleza waandishi wa habari juhudi zilizofanywa na aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo Marehemu Hafidh Ali Tahir kuwa alikuwa ni kiongozi bora aliyepigania maendeleo ya wananchi wa jimbo lake na jamii kwa ujumla bila kuchoka.
 
Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Dimani unafanyika baada ya aliyekuwa Mwakilishi wa Jimbo hilo Hafidh Ali Tahir, kupitia tiketi ya CCM kufariki dunia mapema mwaka huu baada ya kuuguwa ghafla akiwa Mbungeni Dodoma.

Kutokana na kifo hicho Tume ya Uchaguzi ya Taifa Tanzania (NEC), tayari imetangaza kufanyika kwa uchaguzi mdogo , January 22 mwakani.

"KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI"

.

Jumatano, 14 Desemba 2016

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI.

MAKAMU Mwenyekiti wa CCM, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi (BLM), Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, kesho tarehe 15/12/2016 anatarajia kukiongoza Kikao cha Kamati Maalum ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa. 

Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa leo na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar - Idara ya Itikadi na Uenezi, Mhe. Waride Bakar Jabu, amesema kikao hicho cha kawaida cha siku moja kitafanyika Afisi Kuu ya CCM, Kisiwandui kuanzia saa 4:00 asubuhi. 

Amesema kikao pamoja na mambo mengine, kitapokea na kujadili Mapendekezo ya wanachama wa CCM wanaoomba kuteuliwa kugombea nafasi ya Ubunge katika Uchaguzi Mdogo wa Jimbo la Dimani na kuongeza kuwa maandalizi yote yamekamilika.

Aidha, Katibu Waride amesema kikao hicho kilitanguliwa na Kikao cha Sekretarieti ya Kamati Maalum ya NEC, kilichokutana tarehe 14 Disemba, mwaka huu, chini ya Mwenyekiti wake Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Mhe. Vuai Ali Vuai, kwa lengo la kuandaa Agenda za kikao hicho.

“KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI” 

Waride Bakar Jabu 
Katibu wa Kamati Maalum ya NEC 
Idara ya Itikadi na Uenezi - CCM 
ZANZIBAR
14/12/2016

Jumatatu, 21 Novemba 2016

AWASIHI VIONGOZI WA CHAMA KUENDELEZA UTAMADUNI


Na Is-haka Omar, Zanzibar.


NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar ,  Nd. Vuai Ali Vuai amewasihi Viongozi  wa ngazi mbali mbali za Chama  kuendeleza   utamaduni  wa  kuandaa mafunzo ya kuwajengea uwezo Watendaji  wao ili wawe na uelewa  na ujuzi  wa kutekeleza shughuli za Chama kwa ufanisi.


Akizungumza katika Ufunguzi wa Mafunzo elekezi ya Watendaji  wa Chama na Makatibu wa Siasa na Uenezi kuanzia  ngazi za Matawi, Wadi hadi Jimbo  Wilaya ya Amani Kichama yaliyofanyika katika Hoteli ya Villa iliyopo  Maruhubi  Nje Kidogo ya Mjini wa Zanzibar.


Alisema mafunzo  ni nyenzo muhimu  inayosaidia  kuwaongezea maarifa na mbinu mbadala za  kiutendaji  watumishi na watendaji wa taasisi ili wafanye  kazi zao kwa kujiamini zaidi.


Vuai  Alifafanua kuwa CCM inakabiliwa na majukumu ya Uchaguzi wa Chama na Uchaguzi Mkuu wa Dola hivyo  watendaji wa chama hicho wanatakiwa  wanatakiwa kuandaliwa vizuri kupitia mafunzo ya chama kwa lengo la kukumbushwa baadhi ya majukumu yao ya msingi yakiwemo matumizi sahihi ya kanuni, katiba na miongozi ya Chama kwa makada wengine.


“Tuendelee kufanya mafunzo kwa  wingi kadri hali itakavyoruhusu  kwani  ni jambo muhimu kwa binadamu yeyote yule anayetaka maendeleo mazuri ya kazi yake  kwa lengo la kuongeza ujuzi na ufanisi  katika utekelezaji  wa shughuli  zetu za kisiasa ndani na nje ya Chama chetu.”, alisema Vuai na kuongeza kuwa mafunzo  yatawasaidia watendaji hao  kuelewa kwa upana  wanayoyafanya na kuepuka athari ya kufanya kazi kwa mazoea.


Naibu Vuai alieleza kwamba utaratibu wa mafunzo umeanza zamani  ambapo Chama kilikuwa na vyuo vyake maalum vya kuwaandaa makada , watendaji na viongozi makini waliokuwa na uwezo mkubwa wa kujenga hoja  na kuzisimamia katika kuimarisha maendeleo ya Chama.


Alisema kwa mujibu wa ibara ya 5 ya Katiba ya Chama hicho ni kushika Dola Tanzania bara na Zanzibar serikali za mitaa na serikali kuu, hivyo amewapongeza  makada hao kwa uwezo na jitihada zao za kuahakikisha kila uchaguzi toka umeanza mfumo wa vyama vingi CCM imekuwa ikishinda.


Aidha aliwataka watendaji hao kuanzia ngazi za Matawi hadi Wilaya kutumia fursa walizokuwa nazo katika maeneo yao kwa kuanzisha miradi mbali mbali itakayowasaidia kupata kipato cha kutatua baadhi ya changamoto zinazohitaji fedha na kujitegemea wenyewe badala ya kuendelea kuwategemea  Viongozi wa majimbo pekee.


Hata hivyo aliendelea kuwakumbusha  washiriki wa mafunzo hayo kwamba  Watendaji watakaopata fursa ya kugawa fomu za kugombea Uongozi  ndani ya CCM waongeze bidii katika kutenda haki kwa kuhakikisha kila mwanachama  mwenye sifa ya kuchagua na kuchaguliwa  anapata haki hiyo kwa mujibu wa  ibara ya 14 ya Katiba ya Chama hicho.


“ Najua watendaji na viongozi wa CCM ni waadilifu lakini naomba tuongeze umakini katika suala la Uchaguzi wa Chama kwa kuwapatia fomu wale wote wenye Haki ya kuchagua na kuchaguliwa msiwanyime fursa hiyo  kama mtu hafai basi mwacheni  akanyimwe kura  na wanachama wenzake  lakini nyinyi msihusike  na kufanya hivyo kutapunguza malalamiko .”, alisisitiza Vuai.


Naye  Katibu wa Wilaya ya Amani Kichama, Abdallah Mwingi  amesema  lengo la mafunzo hayo kwa lengo la kuzidi  kuwajengea uwezo  watendaji hao ili waweze kusimamia ipasavyo Chaguzi za Chama na Dola zijazo kwa kuwachuja wanachama wanaotaka nafasi za uongozi na kuwapata viongozi ambao ni waumini wa dhati wa itikadi na sera za CCM na serikali zilizopo madarakani.


Alisema  Wilaya hiyo imekuwa ikifanya kazi ya ziada ya kuimarisha chama kwa kuongeza wanachama wapya na kuwapatia mafunzo maalum  kupitia madarasa ya itikadi kwa lengo la kuwajenga kuwa waumini wa kweli  watakaosimamia maslahi ya CCM bila ya hofu.


Akitoa maneno ya Shukrani Mbunge wa Jimbo la Mpendae, Salim Hassan Turky, amesema  washiriki hao watazifanyia kazi nasaha hizo kwa lengo la kuhakikisha CCM inaendelea kuwa Chama bora kinachokubalika kwa wananchi.


Aliwasihi  watendaji  hao  makundi ya kukigawa chama wakati wa Uchaguzi kwani  kuna baadhi ya watendaji waliowahi kusimamia chaguzi zilizopita wamekuwa wakilalamikiwa kwa kufanya upendeleo kwa baadhi ya Wagombea wanaowataka na hatimaye wanapatikana viongozi wenye sifa za kutilia shaka.


 Aliwaomba washiriki hao kuwasaidia na kuwaongoza   wanachama wa Chama hicho katika  kuanzisha miradi midogo midogo kuanzia ngazi za Mashina hadi Mikoa, itakayoweza kuwasaidia kujiajiri wenyewe na kukuza Uchumi wa nchi.

Jumatatu, 3 Oktoba 2016

MATUKIO MBALI MBALI KATIKA PICHA YA ZIARA YA KATIBU WA IDARA YA ITIKADI NA UENEZI YA CCM ZANZIBAR. HUKO KATIKA KIJIJI CHA BOMA WADI YA KIWENGWA LENGO LA ZIARA HII NI KUWASHUKURU WANANCHI KWA JUHUDI ZAO KATIKA KUHAKIKISHA CHAMA CHA MAPINDUZI KINSHINDA KATIKA UCHAGUZI MKUU












































.

.

WANACCM WATAKIWA KUWANIA NAFASI ZA UONGOZI

WAFUASI wa Chama Cha Mapinduzi Wilaya ya Kaskazini “B” kichama wameshauriwa  kujiandaa kisaikolojia  kuwania nafasi za uongozi katika Uchaguzi ujao wa CCM  ili kupata viongozi bora  watakaokuwa na uwezo na weledi wa kiutendaji.



Akizungumza kwa nyakati tofauti  Katibu wa Kamati Maalum ya NEC, idara ya Itikadi na Uenezi Zanzibar,  Waride Bakar Jabu katika ziara ya kuimarisha Chama huko  katika  Matawi ya Bubwini Mafufuni na Donge Kitaruni.


Alisema  maandalizi yakifanyika mapema kwa kutoa taarifa mbali mbali kwa watu wenye nia na sifa za kugombea uongozi zinazokubalika ndani ya CCM itasaidia kuwapata viongozi wazuri na waliokomaa kisiasa.


Alieleza kwamba suala la kujiandaa kuwa kiongozi ndani ya Chama hicho linatakiwa kwenda sambamba na kujitathimini hali ya kisiasa iliyopo ndani na nje ya chama hicho kwa lengo la kupata fikra mpya zitakazoiwezesha CCM kushinda katika uchaguzi Mkuu wa 2020.


“Kwanza CCM inawapongeza Wilaya ya Kaskazini “B” kupitia majimbo yenu mmefanya kazi nzuri katika Chaguzi zote zilizopita chama kimeweza kushinda kwa ngazi mbali mbali na kushika Dola.


Pia nakukumbusheni viongozi muanze  mapema kutoa taarifa kwa wanachama ili wapate muda mzuri wa kujiandaa na uchaguzi huo wa chama ili kupata viongozi wenye uwezo kiutendaji na kukabiliana na changamoto za kisiasa zilizopo Zanzibar, na kuepuka malalamiko yasiyokuwa ya lazima.”, alifafanua Waride.


Aliwasihi viongozi wa Majimbo wakiwemo wabunge , wawakilishi na madiwani kushirikiana na viongozi wa Chama katika utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2015/2020 ili kupunguza ama kumaliza kabisa changamoto zinazowakabili wananchi.


Aliwaagiza viongozi wa matawi ndani ya wilaya hiyo kufanya vikao vya mara kwa mara ili kujadili na kubuni njia mbadala ya kuongeza wanachama wapya ndani ya chama ambao ndio wapiga kura halali katika Uchaguzi Mkuu ujao.


Naye Katibu wa Kamati Maalum Idara ya Ogarnazesheni ya CCM Zanzibar, Haji Mkema alisema lengo lla ziara hiyo ni kuwapongeza wanachama wa chama hicho na wananchi kwa ujumla kwa kuichagua CCM kwa kura nyingi na hatimaye ikaongoza dola.


Aliwambia Makatibu wa Chama wa ngazi mbali mbali ndani ya Wilaya hiyo kujenga utamaduni wa kuandaa takwimu sahihi za wanachama kwa lengo la kujua ni wanachama wangapi wamepungua na  wameongezeka.


Mkema alisema wafuasi wa Chama hicho wanatakiwa kufanya kazi za kuimarisha CCM , lakini pia watumie fursa zinazowazunguka zikiwemo kilimo cha biashara na Chakula  kujenga uchumi wao.


“ Tufanye siasa kwa kuimarisha chama chetu, lakini pia tunatakiwa kujenga uchumi wetu kwa kutumia fursa zinazotuzunguka zikiwemo kilimo cha biashara kwani ardhi yetu ya Donge ina historia ya rutuba kwa mazao mbali mbali hasa Karafuu.”, alishauri Mkema.


Hata hivyo aliwataka wanachama hao kujiunga na Jumuiya mbali mbali za CCM hasa za wanawake na vijana ili waweze kunufaika na fursa mbali mbali zinazopatikana kupitia jumuiya hizo na kuweza kujikwamua kiuchumi.


Kwa upande wa wanachama wa chama hicho waliiomba CCM kuendelea kuishauri serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutafuta ufumbuzi wa kudumu wa kupunguza tatizo la ajira hasa kwa vijana wanaoishi maeneo ya vijijini.


Aidha ameiomba serikali kudhibiti  vitendo vya uhamiaji holela ndani ya Wilaya hiyo kwani unasababisha kuongezeka kwa vitendo vya uhalifu na kuibuka kwa tabia zisizofaa katika jamii.