BAADHI ya
walengwa wa mpango wa kunusuru katika shehia ya Ndagoni, wakichimba msingi wa
kujengea tuta kwa lengo la kuzuwia maji chumvi yasivyamie mashamba ya wananchi,
katika bonde la Uchangani. |
MRATIBU wa TASAF Pemba, Mussa Said akijibu maswali ya walengwa wa mpango wa kunusuru kaya
masikini, mbele ya Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk Abdulla Juma Mabodi. |
NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Dk Abdulla Juma Mabodi, akikagua shughuli za Upandaji wa miti ya Mikandaa, kutoka kwa moja ya walengwa wa mpango wa kunusuru kaya masikini. |
NAIBU katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Dk Abdulla Juma Mabodi, amewataka watendaji wa Chama na Serikali Kisiwani Pemba, kuwa na utamaduni wa kufanya ziara za mara kwa mara kwa wananchi ili kuratibu kero zinazowakabili kwa lengo la kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu.
Amesema wananchi hususani wa Vijijini wamekuwa wakikumbana na changamoto mbali mbali, wakati wa utekelezaji wa miradi yao ya kiuchumi na kijamii, hivyo ni vyema kwa watendaji hao kuhakikisha kuwa wanafika katika kaya ili kujua shida zinazoikabili jamii na sio kubakia Ofisini.
Dk. Mabodi, ameyasema hayo kwa wakati tofauti katika mwendelezo wa ziara yake Kisiwani Pemba yenye lengo la ufuatiliaji wa Utekelezaji wa Ilani ya CCM ya 2015/2020 na ametembelea miradi ya kuzuwia Maji Chumvi na Upandaji Mikoko huko Ndagoni, Miradi ya Ukarabati wa Mto na Ufugaji na Ususi huko Mtangani.
Amesema Sera za Chama cha Mapinduzi zinawajali watu wa makundi yote katika jamii bila ubaguzi wa rangi, kabila na dini.
Naibu Katibu Mkuu huyo amemtaja muasisi wa Mapinduzi ya Zanzibar ya Januari 12, 1964 Marehemu Mzee Abeid Amani Karume kuwa enzi za utawala wake amesimamia misingi ya ubinadamu na utu kwa kugawa eka tatu za ardhi kwa wananchi wa kipato cha chini ili kuwapunguzia ukali wa maisha.
Akizungumzia mradi wa TASAF, Dk.Mabodi ameeleza kuwa mradi huo ni fursa muhimu kwa wananchi wa visiwa vya Zanzibar ambapo utekelezaji wake unagusa maisha ya wananchi wote.
Amesema mradio huo umesaidia kujenga ukuta maalum wa kuzuia maji ya bahari yanayovamia makaazi na mashamba ya kilimo na kuathiri mazao.
Pia akizungumza na kikundi cha ufugaji wa mbuzi kilichopo shehia ya Mtangani, Dk. Mabodi amewasihi wananchi hao kuendesha vizuri mradi huo bila ya kujali tofauti za kisiasa kwani maendeleo hayana Chama wa siasa.
Katika ziara hiyo, Naibu katibu mkuu wa CCM Zanzibar, ameahidi kila kikundi kukipatia msaada wa shilingi laki moja (tsh. 100,000) kwa vikikundi 13 vya walengwa wa mpango wa kunusuru kaya masikini shehia ya Kangani, pamoja na vikundi 14 vya shehia ya Kibokoni Vitongoji.
Naye Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Mkoani ambaye pia ni mkuu wa Wilaya ya Chake Chake, Rashid Khadid Rashid amesifu juhudi za kikundi cha ufugaji wa mbuzi na kueleza kuwa wananchi hao wamepiga hatua kubwa za kimaendeleo kupitia mradi huo.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Uratibu shughuli za Serikali, Khalid Bakar Amran, amesema mikakati ya Serikali ni kuhakikisha wananchi ambao bado hawajalipwa wanapewa fedha zao mara baada ya utaratibu wa malipo utakapokamilika.
Amefafanua kuwa walengwa 42 kwa Pemba ambao bado hawajalipwa, lakini tayari uongozi unaoratibu mradi huo wamewasilisha majina yote Makao Makuu ya TASAF ili wananchi hao wapate fedha hizo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni