Alhamisi, 5 Aprili 2018

MHE.SAMIA ASHUTUSHWA NA UHARIBIFU WA MAZINGIRA DONGE, AFUNGUA OFISI ZA KISASA ZA CCM


MJUMBE wa Kamati Kuu ya CCM taifa Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Wana CCM katika Ofisi mpya ya Mkoa wa Kaskazini Unguja aliyoifungua leo katika mwendelezo wa ziara zake Unguja.

 Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM taifa Mhe. Samia Suluhu Hassan.akiangalia kadi ya ACT-Wazalendo baada ya aliyekuwa mwanachama wa Chama cha ACT kumkabidhi na kujiunga na CCM.

 MWENYEKITI wa Mkoa wa Kaskazini Idd Ali Ame pamoja na Mjumbe  wa Kamati Kuu ya CCM taifa Mhe. Samia Suluhu Hassan, wakiangalia kadi ya CCM wanachama wapya waliojiunga na Chama Cha Mapinduzi leo

 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Abdulla Juma Saadalla Mabodi akizungumza katika mkutano wa ndani mara baada ya  uzinduzi wa Ofisi ya Mkoa wa Kaskazini.

 MJUMBE wa Kamati Kuu ya CCM Taifa Mhe. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi mbali mbali kutoka kwa UWT Mkoa wa Kaskazini Unguja.

 Picha ya hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere akiweka jiwe la msingi katika Ofisi ya Mkoa wa Kaskazini Unguja.

 MJUMBE wa Kamati Kuu ya CCM Taifa Mhe. Samia Suluhu Hassan akikagua eneo linalochimbwa mchanga maeneo ya Donge chechele.

MJUMBE wa Kamati Kuu ya CCM Taifa Mhe. Samia Suluhu Hassan ambaye pia ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akitoa maagizo juu ya udhibiti wa uchimbaji mchanga wakati akizungumza na Waziri wa kilimo, maliasili, mifugo na uvuvi Rashid Ali Juma, katika ziara yake Donge Chechele.

BAADHI ya wananchi wanaojishughulisha na shughuli za uchimbaji mchanga huko Donge Chechele.
 MJUMBE wa Kamati Kuu ya CCM Taifa Mhe. Samia Suluhu Hassan(kushoto) akisalimiana na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja Idd Ali Ame mara baada ya kuwasili katika maeneo ya uwekezaji yanayomilikiwa na CCM huko katika kijiji cha Nungwi.

 MJUMBE wa Kamati Kuu ya CCM Taifa Mhe. Samia Suluhu Hassan(kushoto) akikagua maeneo ya vitega uchumi vya Chama Cha Mapinduzi yaliyopo Nungwi Mkoa wa kaskazini Unguja katika mwendelezo wa ziara yake.
 MJUMBE wa Kamati Kuu ya CCM Taifa Mhe. Samia Suluhu Hassan (kulia) akisalimiana na mwakilishi wa mwekezaji wa eneo hilo Ngugu Braiyan huko Nungwi.

 MJUMBE wa Kamati Kuu ya CCM taifa Mhe. Samia Suluhu Hassan akikata utepe kuashiria ufunguzi wa Ofisi ya Jimbo la Donge.



NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.

MJUMBE wa Kamati Kuu ya CCM Taifa Mhe. Samia Suluhu Hassan amesema wakati umefika wa  Serikali kuzuia uchimbaji wa mchanga katika maeneo ya Donge Chechele ili kuepuka madhara yanayotokana na  uharibifu wa mazingira katika maeneo hayo.

Ushauri huo ameutoa leo katika mwendelezo wa ziara zake kichama  katika Mkoa wa Kaskazini Unguja, Amesema serikali isipochukua maamuzi magumu ya kudhibiti uchimbaji mchanga katika maeneo hayo, visiwa vya Zanzibar vitatoweka.

Amesema miongoni mwa njia za kupunguza uharibifu wa mazingira katika maeneo hayo ni kuweka mkazo katika matumia ya  njia mbadala za ujenzi unaotumia mchanga kidogo kuliko unaotumiwa hivi sasa.

“Haiwezekani tukaendelea kufumbia macho hali hii inayosababisha hatari kubwa katika mazingira yetu, kwani maeneo yanayochimbwa sioni juhudi za kuyarejesha katika hali yake japo kupanda miti ili ardhi ainze kurudi katika sehemu zake.

Pia wananchi msiangalie fedha za siku moja mnazopata katika shughuli za uchimbaji mchanga bali muangalie na vizazi vyenu mtaviacha katika mazingira ya aina gani na mjiulize watalima na kujenga wapi kama maeneo yote yakishaharibiwa.”, amesema Mhe. Samia.

Amesisitiza kuwa kila mwananchi anatakiwa kulinda mazingira yasiharibiwe ikizingatiwa Zanzibar ni nchi ya visiwa.

Baadhi ya takwimu mbali mbali za kimazingira zilizowahi kufanyika nchni, zinaeleza kuwa miaka 50 ijayo visiwa vya Zanzibar vipo hatarini kutoweka kutokana na mabadiliko ya tabia nchi na uharibifu wa mazingira unaoendelea kufanyika.

Pia mhe. Samia ambaye pia ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ametembelea miradi ya CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja katika eneo la uwekezaji katika kijiji cha Nungwi.

Akizungumza katika eneo hilo Mhe. Samia ameuagiza uongozi wa CCM kutumia vizuri vitega uchumi vya miradi ya Chama ili Mkoa huo na Wilaya zake zijitegemee kiuchumi.

Amekemea vitendo vya ubadhirifu na uhujumu wa mali za Chama na kuweka wazi kuwa mtu yeyote mtu yeyote atakayebainika anahujumu miradi ya chama hatobaki salama.

Katika ziara hiyo pia amefungua Ofisi ya CCM Jimbo la Donge na kuwataka Wana CCM wa jimbo hilo kutumia Ofisi hiyo ipasavyo kwa kufanya vikao na mikutano ya kikatiba ya kuimarisha Chama.

Wakati huo huo amefungua Ofisi ya CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja, na kuwataka viongozi wa Mkoa huo kuendeleza juhudi za kurejesha katika mstari hali ya kisiasa katika Mkoa huo.

Amesema huu sio wakati wa Wana CCM hasa viongozi kurumbana na kutengeneza migogoro isiyokuwa na tija, bali washikamane na kukijenga Chama ili kipate ushindi wa kihistoria katika Uchaguzi Mkuu ujao.

Naye Mwenyekiti wa CCM Mkoa huo, Idd Ali Ame amefafanua kuwa viongozi mbali mbali kuanzia wazi hadi Mkoa wamejipanga uchaguzi Mkuu ujao wanashinda kwa ngazi zote hadi kiwango cha asilimia 70.

Katika Mkutano wa ndani uliofanyika katika Ofisi mpya ya Mkoa huo, zaidi ya wanachama wapya 5501 wamekabidhiwa kadi za CCM na Jumuiya zake.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni