Jumapili, 29 Aprili 2018

KISONGE YAPATA VIONGOZI WAPYA


 Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Amani Abdi Ali Mzee ‘Mrope’ (anayezungumza wa pili kulia) akifungua mkutano wa uchaguzi wa viongozi wa maskani ya Kisonge.

 Baadhi ya wajumbe wa mkutano huo wa uchaguzi wakifuatilia matukio mbali mbali yanayoendelea kabla ya uchaguzi kufanyika.

 Mgombea wa nafasi ya Mwenyekiti wa maskani ya CCM Kisonge Juma Raja Juma akipiga kura katika uchaguzi wa viongozi wa maskani hiyo kabla ya kushinda nafasi hiyo.









MASKANI ya Kisonge ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar imempata Mwenyekiti wao mpya,Juma Rajab Juma baada ya kuchaguliwa katika uchaguzi uliofanyika jana,ukumbi wa Nasari ya matumbaku Miembeni.

Uchaguzi huo ulikuwa ni wa ushindani mkubwa ambapo Mwenyekiti huyo aliibuka kidedea baada ya kupata kura 93 kati ya 198 huku kuura 6 ziliharibika.

Wagombea wengine wa waliogombea nafasi hiyo ni Mohamed Haji Dau aliyepata kura 3,Mwanangasama Mohamed aliyepata kura 66.

Akizungumza na wajumbe wa mkutano huo Mwenyekiti huyo mpya,Juma, aliwashukru  wanachama hao kwa kumuamini na kumchagua ambapo ameahidi kushirikiana nao kwa lengo la kuiletea maendeleo Kisonge.

Mapema akifungua Mkutano wa uchaguzi wa maskani hiyo , Mwenyekiti wa CCM Wilaya Amani  Abdi Ali Mzee ‘Mrope’ amewataka wajumbe wa mkutano huo kutochaguana kwa urafiki na kwamba wachaguane kwa uwezo wa kiutendaji na watakaounganisha wana CCM.

Aidha, Mwenyekiti huyo amewasisitiza viongozi watakaochaguliwa kupitia uchaguzi huo kutokubali kuharibiwa heshima ya maskani hiyo ambayo imekuwa na historia ya ukomavu wa kisiasa.

“ Baadhi ya watu wasioipenda CCM wakisikia maskani ya Kisonge ina mpasuko basi wao wanafurahi na kuendeleza mbinu chafu za kuihujumu, kwani hata uchaguzi huu najua kuna watu nje huko hawakupenda ufanyike lakini ndo sasa ushakuwa endeleeni na mapambano ya kukilinda na kukitetea Chama Cha Mapinduzi.

"Kisonge haiwezi kusimama bila ya umoja na mshikamano kwani wazee wetu walioasisi CCM na kuikomboa Zanzibar walikuwa na umoja wakipendana na kutumia vikao halali kusuluhisha migogoro iliokuwa ikijitokeza katika kuwagawa hivyo na sisi tunatakiwa kuweka fikra zetu katika  utamaduni huo na kuachana na misuguano isiyokuwa ya lazima na yenye kubomoa chama,"alisema Mwenyekiti huyo wa Wilaya

Alisema ni wakati wa kila mwana- CCM kuelekeza nguvu zake katika kujiandaa na ushindi wa uchaguzi wa mwaka 2020 na kupoteza muda katika kurumbana wenyewe kwa wenyewe katika mambo yasiyokuwa na tija.

Mwenyekiti huyo wa Wilaya ya mjini  Mrope, alitoa wito kwa wagombea ambao kura zao hazitotosha wasinune na badala yake washirikiane katika kushauri viongozi watakaochaguliwa ili kuendelea kuwa wakomavu wa kidemokrasia.

Kwa mujibu wa katiba na kanuni viongozi mbali mbali waliochaguliwa katika maskani hiyo wataongoza kwa kipindi cha miaka mitano.


Pia, kwa upande wa wagombea wa nafasi ya wajumbe wa kamati ya uongozi ya maskani hiyo ambao ni wajumbe wanne lakini walijitokeza ni 12, ambapo jumla ya kura zilizopigwa ni 168 huku zilizoharibika ni 13.

Walioshinda nafasi ya wajumbe wa kamati hiyo ni ni Dauwat Saleh kwa kura 70, Omar Mohamed Suleiman kura 84, Suwaila Masoud Mohamed kura 96 na Mbaraka Haji Vuai kwa kura 85.

Kupitia uchaguzi huo uongozi mpya wa Kisonge ulimteuwa mjumbe mmoja ambaye ni Suwaila Masoud Mohamed kuwa Katibu wa maskani hiyo kati ya wanne waliochaguliwa katika uchaguzi huo.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni