Jumatano, 13 Desemba 2017

WAJUMBE WA MKUTANO MKUU UMOJA WA WAZAZI WATOA YA MOYONI.

 MWENYEKITI wa Umoja wa Wazazi Tanzania Mkoa wa Mara, Ekwabi Denis akizungumza juu ya matarajio yake juu ya viongozi wa kitaifa waliochaguliwa katika umoja huko.


NA IS-HAKA OMAR, DODOMA.


BAADHI ya Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Tisa wa Umoja wa Wazazi CCM Taifa, wamesema wakati umefika wa Umoja huo kuwa shamba darasa la Jumuiya zingine kujifunza kwao mambo mema ya kiutendaji, uadilifu pamoja na uzalendo.

Wakizungumza kwa wakati tofauti na mwandishi wa habari hizi katika mkutano wa Mkuu wa Tisa wa Jumuiya hiyo, wamesema umoja huo umebeba rika la watu wenye umri na mazingatio ya utu uzima yaliyojaa busara na hekima.

Kwa mtazamo huo, wameeleza kuwa kila jambo linalofanywa nadani ya umoja huo kwa sasa liwe ni nukta ya kujifunza na kuwaelekeza mambo mema wanachama wa Jumuiya zingine ndani ya Chama cha Mapinduzi.

Akizungumza Mwenyekiti wa Umoja huo Mkoa wa Mara Ekwabi Denis Michael, alisema maendeleo ya taasisi hiyo hayawezi kuletwa na mtu mmoja bali yatapatikana kwa ushirikiano baina ya viongozi na wanachama wote.

Amewasihi viongozi wenzake kwa ngazi mbali mbali kujipangia mipango mikakati ya utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku ili jumuiya hiyo iweze kuondokana na utendaji wa kimazoea kwa baadhi ya viongozi na watendaji.

Naye Katibu wa Umoja huo Mkoa wa Shinyanga, Masanja Salu amesema viongozi wote bila ya kujali vyeo walivyonavyo wanatakiwa kushuka ngazi za chini kufahamu changamoto na kuzitafutia ufumbuzi hatua itakayochangia kupatikana kwa wanachama wapya wa kujiunga na umoja huo na Chama kwa ujumla.


Hata hivyo aliongeza kwamba rasilimali zinazomilikiwa na umoja huo katika Mikoa mbali mbali endapo ikisimamiwa vizuri na kitaalam itaingiza mapato ya kumaliza changamoto za ukata wa fedha kwa watumishi wa taasisi hiyo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni