Jumanne, 12 Desemba 2017

SHIBUDA- WAPINZANI WEKENI KANDO SIASA ZA MIHEMUKO

 MWENYEKITI wa Baraza la Vyama vya Siasa Tanzania, Magalla John Shibuda akizungumza mara baada ya ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Tisa wa Umoja wa Wazazi uliofanyika leo katika ukumbi wa JK-Dodoma.



IS-HAKA OMAR, DODOMA.

GWIJI wa siasa za Afrika Mashariki, Magalle John Shibuda ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Siasa Tanzania amesema endapo vyama vya upinzani vitaweka kando siasa za mihemuko na badala yake wakamuunga mkono Dkt. Magufuli Tanzania itaingia katika ramani ya nchi tajiri Duniani.

Kauli hiyo ameitoa leo wakati akichambua hotuba ya Dkt.Magufuli aliyotoa katika ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Tisa wa Umoja wa  Wazazi unaofanyika Dodoma, amesema CCM imepata bahati ya kuwa na Rais mwenye upeo wa kusoma alama za nyakati kwa kutekeleza kwa vitendo mahitaji wa wananchi kisiasa, kijamii na kiuchumi.

Mwanasiasa huyo mkongwe Shibuda, amesema wakati umefika kwa vyama vya siasa kutoa mchango wake wa kumsaidia Rais wa Jamhuri ya muungano Dkt. John Pombe Magufuli katika vita ya kupambana na vitendo vya rushwa na ufisadi ili rasilimali zilizopo ziwanufaishe wananchi wote.

Amesema vita hiyo sio ya Chama cha Mapinduzi pekee bali inahusu maisha ya kila mtu kwani endapo nchi itadhibiti mianya ya upotevu wa mapato ya serikali kila mtu atanufaika.

Ameeleza wazi kwamba Dkt. Magufuli na Dk. Shein ni Marais wa kupigiwa mfano mwema katika nchi za bara la Afrika kwani uongozi wao umeleta mafanikio kwa wananchi na kurejesha heshima ya nchini iliyopotea kwa miaka mingi hasa katika mgawanyo wa rasilimali za umma.

“ Upinzania hauna maana ya kuwa ni lazima tupinge, kubeza na kulaumu kila kitu kinachofanywa na serikali kwa nia njema, bali upinzania wenye manufaa kwa wananchi ni ule unaoshauri, kukosoa na kuibua kero za wananchi ili serikali itafute ufumbuzi wa kudumu.

Pia naomba nieleweke vizuri kuwa kuunga mkono mambo mema yanayotekelezwa na Serikali za CCM sio dhambi, hata wapinzani tunayo fursa hiyo kwani tunanufaika sote”. Anasema Shibuda na kuongeza kuwa vyama vya siasa viwe ushirikiano kama wa kuni ziwapo jikoni kwani uwaka kwa pamoja ili kuivisha chakula.

Shibuda, amesema baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani nchini wametoka katika misingi halisi ya kuwahudumia wananchi kisiasa na badala yake wamekuwa mabingwa wa kujenga hoja dhaifu za kuviza mambo mema yanayofanywa na serikali zote mbili ya Zanzibar  pamoja na ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Amewashauri  viongozi mbali mbali wa Serikali, CCM na jumuiya zake kuyafanyia kazi maelekezo ya kuleta maendeleo kwa wananchi ili kujenga taifa lenye nguvu za kiuchumi.

Akijibu hoja ya mwandishi wa Habari hizi, kuhusu kauli mbiu ya Dkt. Magufuli juu ya Sera ya ukuaji wa uchumi kupitia Viwanda, Mwenyekiti Shibuda ameeleza kwamba hakuna taifa lolote lilofanikiwa kiuchumi bila kupitia viwanda hivyo na Tanzania ikipitia njia hiyo itaweza kunufaika.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni