Alhamisi, 28 Desemba 2017

TABIA MWITA-AISHAURI SMZ KUONGEZA KASI UDHIBITI WA VITENDO VYA UDHALILISHAJI WA KIJINSIA

 MAKAMU Mwenyekiti wa UVCCM Taifa Tabia Maulid Mwita (kusho) Msimamizi na mwandaji wa Vipindi vya  Shirika la Utangazaji Zanzibar ZBC Radio  Suzan Kunambi (kulia) akimfanyia mahojiano kiongozi huyo kuputia kipindi cha Asubuhi na ZBC huko katika Studio za Shirika hilo Rahaleo Unguja.


NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR 
 MAKAMU Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) Tabia Maulid Mwita ameishauri serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuongeza kasi katika usimamizi wa mamlaka zinazohusika na uendeshaji wa kesi za udhalilishaji wa kijinsia kwa wanawake, watoto na watu wenye ulemavu kuhakikisha zinatenda haki.

Kauli hiyo ameitoa leo wakati akizungumza katika kipindi Maalum kinachorushwa mubashara kila siku asubuhi na ridhaa ya Taifa ya Zanzibar  ambayo ni Shirika la Utangazaji  Zanzibar (ZBC Radio) katika jengo la Shirika hilo lililopo Rahaleo Mjini Unguja.

Amesema miongoni mwa mikakati ya UVCCM ni kukemea vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia, dawa za kulevya pamoja na vitendo viovu vinavyosababisha mmomonyoko wa maadili kwa vijana.

Tabia ameeleza kuwa Umoja huo umejipanga kufanya kazi kwa bidii kwa lengo la kuharakisha maendeleo ya taasisi hiyo kisiasa na kiuchumi.

Amesema wakati wa vijana kutumiwa kama ngazi ya kufikia mafanikio kwa baadhi ya watu umekwisha na badala yake vijana hao watumie fursa zilizowazunguka kujitafutia kipato.

“ Vijana tunatumiwa na baadhi ya wanasiasa hasa inapokaribia kipindi cha kampeni za uchaguzi na wanapopata nafasi hawaanzishi miradi ya maendeleo ya kulisaidia kundi hilo ambalo wengi wao hawana ajira za uhakika.

Sasa ifikie wakati na sisi tuwe na misimamo kwa kujiajiri wenyewe kupitia sekta ya ujasiria mali na ufundi na watushauri mambo mbali mbali ya kuimarisha taasisi yetu kisiasa.

Kupitia kipindi hicho Makamu Mwenyekiti huyo ametoa wito kwa vijana wote nchini kuwaunga mkono viongozi wa Chama na Serikali hasa Mwenyekiti wa CCM Taifa Dkt. John Pombe Magufuli na Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein kwani viongozi wanaojali maslahi ya vijana.

Amesisitiza wananchi kuheshimu utawala wa kisheria kwa kuepuka uvunjaji wa sheria na miongozo mbali mbali ya nchi.


Pamoja na hayo amewataka viongozi wa UVCCM kuwa mfano wa kuigwa kivitendo, kauli, maadili, hekima na busara ili vijana wengine waliopo katika vyama vya upinzani wavutike na kujiunga na umoja huo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni