Jumatano, 13 Desemba 2017

DKT.MNDOLWA- AIBUKA MSHINDI MWENYEKITI WA WAZAZI TAIFA, ATOA VIIPAUMBELE VYAKE.

MWENYEKITI wa Jumuiya ya Wazazi Tanzania Dkt.Edimund Benard Mndolwa akiwashukru wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Umoja huo kwa kumchagua ili aongoze kwa miaka mitano ijayo.

NA IS-HAKA OMAR, DODOMA.

UMOJA wa Wazazi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Taifa wamefanikiwa kumpata Mwenyekiti mpya ambaye ni mwanasiasa mkongwe na msomi wa kada ya Uchumi ambaye ni Dkt. Edimund Benard Mndolwa kufuatia uchaguzi uliokuwa na ushinsani mkubwa uliofanyika jana katika Ukumbi wa JK uliopo Dodoma.

Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo, Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa , Jerry Slaa kwa niaba ya jopo la wasimamizi wa uchaguzi huo  alimtangaza  Mwenyekiti huyo mpya kuwa ameshinda kwa kupata kura 552 sawa na asilimia 68.06 kati ya kura 811 zilizopigwa na akawashinda wenzake watatu alikuwa akichuana nao.

Wagombea wengine wa nafasi hiyo walikuwa ni Eng. Burton Lumuliko Kihaka kura 178, Simon George Rubugu kura 59 na Fadhil Rajabu Maganya aliyepata kura 22.

Kwa nafasi ya Makamu Mwenyekiti wa Umoja huo aliyeibuka kidedea ni mwanasiasa mpambanaji aliyewahi kugombea nafasi hiyo katika awamu iiyopita akakosa lakini kwa awamu ya sasa amefanikiwa kuibuka mshindi ambaye ni Haidar haji Abdallah.

Pia katika nafasi ya NEC Tanzania bara waliotazwa kushinda ni Nemelock Sokoine, Mohamed nassor kingite pamoja na Paul Herman Kirigini, ambao wameshinda kati ya wagombea 11 waliokuwa wakiwania nafasi hiyo. Nafasi zingine za NEC kutoka Zanzibar ni Suleiman Juma Kimea pamoja na Amina Ali Mohamed walioshinda kati ya wagombea wanne waliokuwa wapo katika kinyang’anyiro hicho.

Kwa upande wa Baraza Kuu Zanzibar walioshinda ni Habiba Mohamed, Ali Issa Ali pamoja na Cristina Anton waliochaguliwa kuwawakilisha Wana CCM katika baraza hilo.

Kwa upande wa Baraza Kuu kwa Tanzania bara ni Lulu Mtemvu, Stephan Hilary Maji Marefu pamoja na Sudi Kassim Sudi.

Kwa nafasi ya uwakilishi wa UWT aliyeshinda ni Nuru Kassian Baimanga kati ya wagombea wenzake wawili aliokuwa akishindana nao. Hata hivyo katika nafasi ya uwakilishi wa UVCCM aliyeshinda ni Omar Ajili Kalolo kati ya wagombea wenzake  watano aliokuwa akishindana nao.

Matokeo hayo yametangwazwa mbele ya viongozi mbali mbali akiwemo Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein, Katibu Mkuu wa CCM Taifa , Abdulrahman Omar Kinana, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Mabodi pamoja na Mwenyekiti Mstaafu wa Umoja wa Wazazi wa CCM Tanzania Abdallah Bulembo.

Akizungumza mara baada ya kutangazwa mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti na kuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa, Dkt. Edimund Benard Mndolwa ametoa shukrani zake kwa wajumbe wote wa Mkutano huo na kuahidi kuendeleza mambo mema yaliyoachwa na mtangulizi wake.

Akitaja vipaumbele vyake alieleza kuwa atahakikisha anatatua kwa haraka changamoto ya mishahara kwa watumishi wa Umoja huo sambamba na kumaliza madeni yanayoikabili taasisi hiyo.

“ Mmenichagua nikutumkieni name nakuahidini kuwa sitowaangusha bali nitatumia nguvu na elimu niliyonayo katika masuala ya uchumi kufanya mageuzi ya kiuchumi yatakayowanufaisha wanajumuiya wote bila ubaguzi”, amesema Dkt. Mndolwa.

Pia ameeleza kuwa atakuwa mstari wa mbele kuendeleza mapambano dhidi ya vitendo vya rushwa na ufisadi Ndani na nje ya umoja huo.

Ameitaja dhamira ya kuwania nafasi hiyo kwamba ni kukitumikia Chama cha Mapinduzi kwa uadilifu na utii sambamba na kuhakikisha kinashinda kwa kishindo katika uchaguzi Mkuu wa Dola wa mwaka 2020.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni