Ijumaa, 22 Desemba 2017

DK.SHEIN AIMWAGIA SIFA TIMU YA ZANZIBAR HEROES

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein akizungumza na Timu ya Zanzibar Heroes katika hafla maalum ya chakula cha mchana alichoiandalia timu hiyo na viongozi wake.

 BAADHI ya wachezaji wa Timu ya Zanzibar Heroes wakisikiliza nasaha za Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein katika hafla hiyo

 VIONGOZI mbali mbali wakiongozwa na Dk. Shein wakati wa Chakula cha Mchana cha kuipongeza Timu ya Zanzibar Heroes baada ya kufanya vizuri katika mashindano ya CECAFA.
Picha ya pamoja ya wachezaji wa Timu ya Zanzibar Heroes pamoja na Rais wa Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein.

WACHEZAJI wa Timu ya Zanzibar Heroes wakijumuika na viongozi mbali mbali katika Chakula cha Mchana kilichoandaliwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein.






RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameendelea kutoa pongezi kwa timu ya Taifa ya Zanzibar, ‘Zanzibar Heroes’ kwa kuirudishia Zanzibar heshima yake na sasa imekuwa inasemwa vizuri kutokana na jinsi timu hiyo ilivyoonesha kiwango safi cha kusakata soka.

Dk. Shein aliyasema hayo leo huko katika viwanja vya Ikulu mjini Zanzibar katika chakula maalum cha mchana alichowaandalia wachezaji wa Timu ya Zanzibar Heroes pamoja na viongozi wake wote baada ya kufanya vyema katika mashindano ya mwaka huu ya Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati ‘CECAFA’ yaliofanyika nchini Kenya.

Aliongeza kuwa wachezaji hao wa ‘Zanzibar Heroes’ wamewawakilisha vizuri Wazanzibari wote kutokana na uwezo na nguvu ya mpira waliouonesha na hadi kufikia fainali za mashindano hayo ya CECAFA.

Dk. Shein ameeleza  kuwa watu waliowengi hawakuifikiria timu hiyo ya Zanzibar kama itafika ilipofika na pia baadhi ya watu hawakuwa wakiisema vizuri lakini hatimae imedhihirisha kuwa Zanzibar ina historia nzuri ya soka na kuondosha usemi kuwa ‘Chenga twawala’.

Aidha, Dk. Shein amesema  kuwa kuwaandalia chakula hicho cha mchana hivi leo ni mwanzo tu wa pongezi zake lakini kuna zawadi tatu kubwa amewaandalia ikianzia taarab maalum ya kikundi cha Taifa cha Zanzibar pamoja na zawadi nyengine mbili kubwa ambazo hazijawahi kutokea na kukataa kuzitaja hii leo na kuahidi kuzitaja hapo kesho.

Nae Kocha Mkuu wa Zanzibar Heroes Hemed Suleiman Moroko ametoa  pongezi kwa Rais Dk. Shein pamoja na kwa viongozi wengine wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kocha Abdulkhani Msoma pamoja na Mwalimu Abdalla Mwinyi kutokana na nasaha zake za kutaka wachezaji wawe na silka na hulka za Kizanzibari wakiwa katika mashindano hayo ambazo ndizo zilizowasaidia.

Pamoja na hayo, Kocha mkuu huyo ametoa ombi  maalum kwa Rais Dk. Shein kumualika Rais wa Shirikisho la Soka Barani Afrika Ahmad Ahmad kuja Zanzibar ili kufanya mazungumzo nae kwa ajili ya kuzungumza mustakbali wa Zanzibar katika soka kimataifa.

Wakati huo huo Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdalla Juma Mabodi ameeleza kwamba kwa niaba ya CCM Zanzibar anaipongeza Timu hiyo kwa kulinda heshima ya Zanzibar katika mashindano ya CECAFA.

Dk. Mabodi ameeleza kuwa kutokana na uwezo wa soka ulioonyeshwa na vijana hao, unatoa taswira halisi ya kuwa Zanzibar inastahiki kuingia katika orodha ya nchi za Afrika zinazotakiwa kushiriki bila vikwazo katika soka la kimataifa.

 " Chama cha Mapinduzi Zanzibar kinawapongeza kwa mara nyingine tena wachezaji na viongozi wote walioshiriki katika mashindano hayo na kuibuka mshindi wa pili kwani hatua hiyo ni kubwa sana kwa nchi yetu kwani mmerejea historia ya Zanzibar ya mwaka 1995 ambapo timu yetu ilitwaa kombe la chalenji", alisema Dk. Mabodi.

Pamoja na hayo Naibu Katibu Mkuu huyo amewasihi vijana mbali mbali nchini kuachana na vikundi viovu badala yake watumie sekta ya michezo hasa Soka kujiajiri wenyewe.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni