Jumapili, 10 Desemba 2017

DKT.MAGUFULI ANENA MAZITO, AWATAKA UVCCM KUWA KIOO CHA JAMII

NA IS-HAKA OMAR, DODOMA.


MWENYEKITI  wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Taifa Dkt. John Pombe Magufuli amewataka viongozi wapya watakaochaguliwa kupitia Mkutano Mkuu wa Umoja huo kutobweteka na badala yake waanzishe miradi mikubwa ya kiuchumi itakayotoa fursa za ajira kwa vijana na wananchi kwa ujumla.

Agizo hilo amelitoa leo wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Tisa wa UVCCM Taifa uliofanyika katika ukumbi wa Chuo cha Mipango mjini Dodoma, Dkt. Magufuli amebainisha kwamba umoja huo umejaliwa kuwa na bahati ya kumiliki rasilimali nyingi lakini cha kusikitisha zinawanufaisha wa wachache huku kundi kubwa la vijana naishi bila ajira.

Amesema sasa ni wakati wa UVCCM kufungua ukurasa mpya wa kuwachagua viongozi waadilifu na wachapa kazi watakaoweza kusimamia uhai na ustawi wa umoja huo ili uweze kuwatumikia vijana wote bila ya ubaguzi.

Dkt. Magufuli ambaye ni  Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania amesema umoja huo utakuwa na nguvu endapo utapata viongozi wenye uthubutu wa kupinga vitendo vya rushwa,ufisadi pamoja na makundi yasiyofaa ndani ya umoja huo.

“ Anzisheni miradi sisi mkitujia mnataka msaada tupo tayari kuwasaidia na sijawahi kuwaona mkitaka msaada, lakini najua wenda baadhi yenu mliogopa kuomba msaada kutokana na matendo yenu ya kuhujumu mali za UVCCM.

Lazima tuambizane ukweli kuwa rasilimali nyingi za UVCCM zinaishia mikononi mwa wajanja huku vijana wengi ambao ndio kundi kubwa hawanufaiki.”, alieleza Dkt. Magufuli.

Aliwambia vijana hao kuwa ndio tegemeo la CCM katika kujenga taifa huru kiuchumi, kisiasa na kijamii.

Aliweka wazi kuwa serikali ya awamu ya Tano anayoiongoza inawathamini vijana kuliko wao wanavyofikiria ndio maana amekuwa akiwateuwa katika nafasi mbali mbali za uongozi.

“Huu ni wakati wenu vijana wa kilipeleka mbele taifa letu kiuchumi kwani wengi wenu mna ujuzi na maarifa tofauti, fanyeni kazi kwa bidii ili nchi yetu iwe imara kiuchumi.

Lakini pamoja na yote hayo Mimi na Rais mwenzangu Dk.Shein hatuwezi kukubali kuiacha nchi katika mikononi mwa viongozi mafisadi na wala rushwa, hata waasisi wetu wa ASP na TANU huko waliko hawatoridhika.”, amesema Dkt. Magufuli.

Amefafanua kwamba UVCCM inahitaji viongozi wenye uzalendo uliokidhi sifa za uwajibikaji, waadilifu na wenye uthubutu wa kujenga hoja zenye fikra za kuwanufaisha vijana wa makundi yote.

Amewatanabaisha kwamba endapo watachagua viongozi wala rushwa na walioingia madarakani kwa hongo basi wakubali kuumia kwa miaka mitano ijayo.

Hata hivyo alieleza kwamba CCM inatambua mchango mkubwa wa vijana wake katika kulinda na kupigania maslahi ya chama kisiasa na kijamii, hivyo hatowaangusha bali ataendelea kushirikiana nao kwa kila japo.

Mapema akisoma taarifa ya utekelezaji ya UVCCM ya kipindi cha miaka mitano iliyopita Kaimu Katibu Mkuu wa UVCCM Taifa Shaka Hamdu Shaka, alisema umoja huo umekuwa mstari wa mbele katika kujenga itikadi, imani na kudumisha uzalendo kwa vitendo.

Amesema umoja huo unajiuvunia kuwa na Marais wenye imani na mapenzi ya kweli kwa wananchi wanaowangoza ambao wapo tayari kuwapigania ucku na mchana ili waweze kunufaika na rasilimali zilizopo nchini.


Shaka ameeleza kwamba kwa kipindi cha miaka mitano Umoja huo umejiimarisha katika Nyanja mbali mbali za kiuchumi, kijamii na kisiasa na kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa kitovu cha amani na utulivu wa kudumu.


MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar  Dkt. John Pombe Magufuli akiwahutubia mamia ya Vijana wa UVCCM katika ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Tisa uliofanyika leo katika ukumbi wa Chuo cha  Mipango Dodoma.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni