Alhamisi, 30 Novemba 2017

NAGMA GIGA- AFUNGUA MKUTANO WA UCHAGUZI WAZAZI, ASISITIZA USHIRIKIANO KUDHIBITI UDHALILISHAJI

Na Is-haka Omar, Zanzibar.
             
NAIBU Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wazazi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Nagma Giga amewataka wazazi na walezi kuunga mkono juhudi za serikali na wanaharakati kwa kupinga vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia kwa wanawake na watoto nchini.

Kauli hiyo ameitoa wakati akifungua mkutano Mkuu wa uchaguzi wa Wazazi katika Mkoa wa Mjini, uliofanyika Amaani Unguja.

Amesema wazazi ndio walezi na waangalizi wa malezi ya makundi yote katika jamii hivyo ni lazima wawe mstari wa mbele kupinga vitendo vyote vinavyoensda kinytume na maadili, mila desturi na utamaduni visiwani humo.

Amefafanua kwamba ushindi dhidi ya vitendo vya udhalilishaji itafanikiwa endapo jamii itakuwa tayari kushirikiana na Serikali na vyombo vingine vya kisheria ili kudhibiti uhalifu huo unaochafua heshima na sifa ya nchi kitaifa na kimataifa. 

"Hii ni vita yetu sote kila mzazi amuone mtoto wa mwenziwe kama wake hapo ndipo tutakapoweza kuwalinda watoto wetu ili wakue katika malezi bora yasiyokuwa na vikwazo vya kukatisha malengo yao ya baadae.

Wanawake na watoto wengi wamekuwa ni wahanga kubakwa,kulawitiwa na kutelekezwa hali inayosababisha wengi wao kuathirika kisaikolojia ” Ameeleza kwa uzuni Nagma. 

Pia aliwasihi wazazi, viongozi wa dini na wanasiasa nchini kuhakikisha wanakemea kuporomoka kwa maadili kwa baadhi ya vijana wanaovaa nguo zinazokwenda kinyume na utamaduni sambamba na kutumia lugha zisizofaa katika jamii. 

Akizungumzia Uchaguzi wa Mikoa mbali mbali ya jumuiya hiyo, Nagma amewasisitiza wajumbe wa mikutano hiyo kuwachagua viongozi imara na wenye dhamira ya kweli katika kuleta mabadiliko ya kimaendeleo ndani ya jumuiya na Chama Cha Mapinduzi kwa ujumla.

Amesema wasimamizi wa uchaguzi huo kutenda haki na wapiga kura kuwa na uadilifu wakati wa kutekeleza wajibu wao wa kidemokrasia kwa kuchagua viongozi wanaowataka bila ya kufanya vurugu.

Naibu Katibu Mkuu huyo, amesema Jumuiya hiyo ina majukumu mawili makubwa ya kuhakikisha CCM inashinda na kubakia madarakani kupitia uchaguzi mkuu wa Dola sambamba na kusimamia mwenendo wa elimu, malezi, utamaduni na mazingira kwa jamii.

Ameeleza kuwa  nchi zilizoendelea Ulimwenguni ni zile zilizowekeza katika sekta ya elimu inayozalisha wataalamu wa fani mbali mbali za kuleta maendeleo ya haraka katika kukuza uchumi wa nchi kupitia mfumo wa uzazilishaji mali katika sekta za viwanda vinavyotegemea mfumo wa sayansi na teknolojia.

“Kila wana CCM anatakiwa kuchukua jukumu la kuwaelimisha vijana wetu wasome kwa bidii ili Chama na jumuiya zetu ziwe na wanachama wengi wenye uwezo mzuri wa kitaaluma watakaoweza kusimamia maslahi ya taasisi zetu bila kuyumba.

Mikakati hiyo itafanikiwa kama tutapata viongozi makini kupitia uchaguzi huu ambao ni wapambanaji wasiochoka wala kukata tama katika uwanja wa kisiasa.” Amefafanua Naibu Katibu Mkuu Giga. 

Naye Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Amani ambaye ni mjumbe wa Mkutano huo, Abdi Ali Mzee ‘’Mrope’’ amesema wakati umefika wa Chama cha Mapinduzi na jumuiya zake kuwa na ajenda moja ya kutumia vizuri rasilimali zinazomilikiwa na Chama kuanzisha miradi mikubwa itakayozalisha kipato na kutoa ajira za kudumu kwa vijana.

Kwa upande wake mjumbe wa Mkutano huo, Salma Abdi Ibada amewashauri viongozi watakaochaguliwa kupitia uchaguzi huo wawe mfano wa kuigwa katika kuleta maendeleo ndani ya jumiya na kupiga vita vitendo vya rushwa na makundi ya kuhatarisha uhai wa Chama. 

Uchaguzi huo umefanyika katika Mikoa yote jumuiya ya Wazazi nafasi ambazo zinashindaniwa ni Wenyeviti wa Mikoa, nafasi ya Mkutano mkuu taifa/Baraza la wazazi taifa, nafasi mkutano mkuu wa CCM mkoa, pamoja na nafasi za Baraza kuu la wazazi Mikoa kutoka kila Wilaya.
Katibu wa CCM Mkoa wa Mjini Mohamed Omar Nyawenga(kushoto) Naibu katibu Mkuu wa Jumuiya ya wazazi Zanzibar Nagma Giga (katikati) na viongozi wengine wa jumuiya ya wazazi.

 BAADHI ya wajumbe wa Mkutano huo wakisikiliza kwa makini hotuba ya ufungunguzi ya mgeni rasmi


Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Amani, Abdi Ali Mzee “Mrope” akiwasalimia wajumbe wa mkutano huo wa uchaguzi jumuiya ya wazazi Mkoa wa Mjini.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni