Alhamisi, 2 Novemba 2017

CCM Z'BAR YASHUSHA RUNGU KWA WANAOHUJUMU MIUNDOMBINU YA MAJI SAFI NA SALAMA.


Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzbar akiwa katika ziara ya kukagua miundombinu ya Maji huko katika Kisima Cha Kitope Skuli akiwa ameongozana na viongozi wa CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja  kushoto  Katibu wa CCM wa Mkoa wa Kaskazini Unguj, Mulla Othiman Zubeir na kulia ni Mwenyekiti wa CCM  Mkoa wa  Kaskazini Unguja Juma Haji.


Mashine ya Kisima cha Maji safi na Salama katika Skuli ya Kitope iliyoharibika hivi karibuni na kwa sasa inayofanyiwa matengenezo ili wananchi wa maeneo hayo waweze kuendelea kupata huduma ya maji.

Naibu Katibu Mkuu wa CCM  Zanzbar akimsiliza kwa makini Afisa  wa Maji wa Wilaya ya Kaskazini “B”  Amour Mohamed Ame wakati wa zaiara ya kutombelea Kituo cha maji cha Kitope Skuli chenye kisima kilichoharibika baadhi ya vifaa katika mashine Wilaya ya Kaskazin ‘’B’’ Unguja .

Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdalla Juma Mabodi akiangalia sehemu iliyoibiwa waya wa umeme katika Kituo namba 4 kisima kilichopo eneo la Kiashange Wilaya ya Kaskazini “A”.  (PICHA NA AFISI KUU ZANZIBAR).



CHAMA Cha Mapinduzi  (CCM) Zanzibar kimekemea  vitendo vya kuhujumu miundombinu ya maji safi na salama vinavyofanywa na baadhi ya watu wenye nia ya kukwamisha juhudi za serikali katika kuwapelekea wananchi huduma muhimu za kijamii.

Akizungumza Naibu Katibu Mkuu wa Chama hicho Zanzibar Dk. Abdulla Juma Mabodi katika ziara Maalum ya kukagua baadhi ya maeneo yaliyohujumiwa miundombinu hiyo katika Mkoa wa Kaskazini Unguja huko katika shehia ya Mkwajuni katika Kisima namba 4 cha Kiashange  Wilaya ya Kaskazini “A”.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa ikitumia fedha nyingi za walipa kodi kuimarisha miundombinu ya maji mijini na vijijini ili wananchi waondokana na kero ya ukosefu wa huduma hiyo lakini kuna baadhi ya watu kwa maslahi yao binafsi wamekuwa wakiharibu  miundombinu hiyo kwa makusudi.

Kisima hicho kilichoibiwa waya za umeme wa mashine inayosukuma maji hadi tangi kubwa la Kijiji cha Nungwi na maeneo jirani linalosambaza maji katika maeneo mbali mbali ya Wilaya ya Kaskazini “A” hali inayosababisha usumbufu kwa baadhi ya wananchi wa maeneo hayo.

Dk.Mabodi alieleza kwamba maji yana mahitaji muhimu katika maisha ya kila siku ya mwanadamu hivyo yanapokosekana ama kutopatikana kwa wakati yanasababisha usumbufu na madhara makubwa hasa katika maeneo ya huduma za kijamii yakiwemo Nyumba za Ibada, Hospitalini, Shuleni na kwa wagonjwa wanaotibiwa wakiwa majumbani mwao.

Alisema  vitendo vya kuziba mipira ya maji kwa kutumia zege, kuiba mipira, mabomba, pumbu, mashine za kusambazia maji, waya za umeme, Transfoma  pamoja  kufunga mifugo katika maeneo ya miundombinu ya maji ni vitendo hivyo ni miongoni mwa hujuma zisizokubalika kisheria na kijamii.

Naibu Katibu Mkuu huyo alifafanua kuwa CCM miongoni mwa majukumu yake ni kuisimamia serikali itatue kero za wananchi hivyo haitokuwa tayari kuona vinafanyika vitendo vya kuharibu hali ya kisiasa na amani ya nchi kwa kuharibu kwa makusudi rasilimali za nchi katika Mkoa huo.

Alitoa wito kwa wananchi wa maeneo mbali mbali yenye miundombinu ya maji katika Mkoa huo kuhakikisha wanakuwa walinzi wa rasilimali hizo na kutoa taarifa sahihi kwa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) ili wawachukulie hatua za kisheria watu wanaijihusisha na hujuma hizo.


Ameagiza viongozi wa CCM wa ngazi za Wilaya na Mkoa wa Kaskazini Unguja kukaa karibu na wananchi kuibua kero zao na kusimamia utekelezaji wa ilani ya uchaguzi unaofanywa na serikali.

Pia amehimiza  serikali kukamilisha taratibu za upatikanaji wa huduma za maji kutoka katika visima vilivyochimbwa na wadau wa maendeleo ili viwasaidie  wananchi kupata huduma za maji kwa uhakika.


Pamoja na hayo Dk. Mabodi ameishauri serikali kuanzisha mpango wa kutengeneza matangi makubwa ya maji katika shehia na zoni mbali mbali nchini.

Hata hivyo amezitaka Kamati za maendeleo za shehia zenye tatizo la maji  huko Kitope kukaa kimkakati na watendaji wa Wizara inayoshughulikia maji na nishati ya umeme kuhakikisha umeme unapatikana muda wote katika miundombinu ya maji.

Naye Kaimu Afisa wa Maji wa Mkoa huo  wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA), Dude Juma Ame alishauri kuwekwa  walinzi katika maeneo mbali mbali yenye miundombinu ya maji katika Mkoa huo ili kudhibiti hujuma hizo.

Mapema akizungumza Naibu Katibu Mkuu huyo Dk. Mabodi  katika Kisima cha maji kilichopo maeneo ya Kitope Skuli ambacho hakitoi maji kutokana na  kuharibika kwa kifaa ndani ya Pampu ya kisima hicho aliwataka mafundi wa Mamlaka ya Maji  Zanzibar (ZAWA) kuharakisha matengenezo hayo ili wananchi wa maeneo hayo waendelee kupata huduma za maji.

Kutokana na mahitaji ya huduma ya maji safi na salama katika Hospitali ya Kitope,  Dk. Mabodi  alisema CCM Zanzibar  itachimba kisima cha maji safi na salama ndani ya hospitali hiyo ili wapate huduma hiyo kwa wakati mwafaka.

Akitoa ufafanuzi juu ya matengenezo ya Pambu ya Kisima hicho Afisa wa Wilaya ya Kaskazini “B” Unguja, Amour Mohamed Silima alisema kuwa vifaa vinavyohitajika tayari vimeshapatikana hivyo kufikia kufikia mwezi  Novemba  4,  mwaka huu watakuwa wamekamilisha na wananchi wanapata  huduma ya maji.

Alifafanua kuwa changamoto inayowakabili katika visima vya maji mbali mbali ndani ya Wilaya hiyo ni kuharibika kwa mashine za maji kutokana na athari za umeme zinazosababishwa na madhara ya Radi katika kipindi cha msimu wa Mvua za vuli zinazoendelea kunyesha nchini.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni