Ijumaa, 24 Novemba 2017

MH.KASSIM MAJALI MGENI RASMI FAINALI MAJIMBO CUP ZANZIBAR



Na Is-haka Omar, Zanzibar.

WAZIRI Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Kassim Majaliwa  kesho Novemba 25, mwaka huu anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika mashindano ya fainali ya ligi za Majimbo ya Mkoa wa Mjini  Zanzibar.


Mchezo huo utakaotimua vumbi katika Kiwanja  cha Amaan Stadium Unguja, ambapo utazikutanisha timu mbili zilizofanikiwa kufika finali ambazo ni Timu ya Afisi Kuu CCM Zanzibar na Timu ya Jimbo la Kwahani.

Kabla ya mtanange huo mkali kutatanguliwa na mechi ya kumsaka mshindi wa tatu ambayo itachezwa na timu za jimbo la Kikwajuni na jimbo la Malindi kwa ajili ya kutafuta mshindi wa tatu.
Michezo hiyo inayotarajiwa kuwa na ushindani mkali kutokana na uwezo wa kila timu katika masuala ya Soka.

Akizungumza na mwandishi wa Habari hizi Katibu wa Kamati ya mashindano hayo, Suzan Kunambi amesema maandalizi ya fainali hiyo tayari yamekamilika kwa upande wa Kamati yake na kwa timu zinazotarajiwa kushiriki zote zimedhibitisha ushiriki wao.

Ameeleza kwamba mashindano hayo yaliyoanza mwezi Machi 24 mwaka huu kwa kuzishirikisha timu 18 za majimbo pamoja na vikundi vya uhamasishaji vya CCM kutoka Mkoa wa Mjini pamoja na majimbo jirani yaliyoalikwa kutoka Mikoa yote ya Unguja.

Katibu huyo amefafanua kuwa mashindano hayo yalizinduliwa  na Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar ambaye pia ni Rais wa Zanzibar Dk.Ali Mohamed Shein na yanatarajiwa kufungwa na Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya muungano wa Tanzania Mh. Kassim Majaaliwa.

Suzan ameyataja malengo ya mashindano hayo kuwa ni kujenga umoja na mshikamano kwa vijana mbali mbali waliopo majimboni ili wajikwamue katika changamoto za ukosefu wa ajira na makundi maovu kwa kujiajiri wenyewe kupitia vipaji vyao vya soka.

Amesema  mashindano hayo yamekuwa ni chachu ya kuibua vipaji vya soka ambapo wacheza mbali mbali wamepata fursa za kujiunga na timu kubwa zilizopo katika mashindano ya ligi za madaraja mbali mbali ya soka nchini.

“ Tunamshukru Makamo Mwenyekiti wetu Dk. Shein kwa mchango wake mkubwa wa kuthamini soka la vijana na kuimarisha sekta ya michezo nchini”, alitoa pongezi hizo Katibu huyo na kuongeza kuwa Kamati hiyo imejipanga kushirikisha timu nyingi zaidi ili mashindano yaendelee kuwa bora na kuwanufaisha vijana.

Akizungumzia zawadi zitakazotolewa kwa mshindi wa mwanzo hadi wa tatu amefafanua kuwa mshindi wa kwanza atapata Gari moja, Kikombe na medali ambapo mshindi wa Pili atapata fedha taslim shilingi milioni tatu na medali pamoja na mshindi wa tatu atapata shilingi milioni mbili na medali.

Sambamba na hayo aliwaomba wapenzi wa Soka wa ndani na nje ya Zanzibar kujitokeza kwa wingi katika uwanja wa Amaan kushangilia timu zao kwani kiingilio ni bure.

 Mechi ya mwanzo itachezwa majira ya saa 8:00 mchana na ya pili ambayo ni fainali itachezwa kuanzia majira ya saa 10:00 jioni.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni