Ijumaa, 15 Februari 2019

DK.SHEIN: ASEMA SMZ ITAENDELEA KUIMARISHA MIUNDOMBINU SEKTA YA ELIMU

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akiweka Jiwe la Msingi Skuli ya msingi Kwarara Wilaya ya Magharibi 'B' Unguja.

 BAADHI ya Wananchi wakiwemo wanafunzi walioudhuria hafla ya uwekaji wa Jiwe la msingi katika Skuli ya msingi Kwarara.



RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk Ali Mohamed Shein  amesema katika kutekeleza sera ya elimu bila malipo, Serikali inaendelea na juhudi za kuimarisha miundo mbinu ya kielimu ili kwenda sambamba na mahitaji yaliopo.

Dk Shein amesema hayo leo katika hafla ya  uwekaji wa jiwe la Msingi wa Skuli ya msingi Kwarara, Wilaya ya Magharibi ‘B’ Unguja.

Amesema kutokana  na  ongezeko kubwa la wanafunzi hali inayotokana na kiwango kikubwa cha wakaazi wa Zanzibar hivi sasa, Serikali inalazimika kuongeza idadi ya madarasa ili kwenda sambamba na ongezeko la wanafunzi katika skuli za msingi na sekondari.

Amesema ongezeko la idadi ya watu kutoka 300,000 mwaka 1964 hadi kufikia Milioni moja na nusu hivi sasa imefanya kuwepo mahitaji makubwa ya madarasa , huku baaadhi ya skuli zikiwa na wanafunzi wanaofikia 234 katika darasa moja,

Amesema hivi karibuni Serikali  imeagiza madawati 44,000 kutoka nchini China  na kubainisha kuwa nusu ya samani hizo zimewasili nchini na kugawiwa katika skuli za msingi na sekondari.

Dk. Shein amesisitiza azma ya serikali na kuwataka wazazi na walezi wa wanafunzi kutokuchangia huduma zote za kielimu katika skuli za msingi  na sekondari, ikiwemo vitabu madaftari.

Amesema lengo la serikali ni kuwaandaa vijana wake kielimu ili kufanikisha azma ya kuwa an wataaalamu  katika fani mbali mbali ili kuliwezesha Taifa kupata maendeleo ya haraka.

Alisema uchumi wa Zanzibar umeendelea kuimarika kadri miaka inavyosonga hatua inayotokana an makusanyo mazuri ya mapato na kubainisha kuwa hivi sasa Serikali inakusanya kati ya  shilingi Bilioni 65 hadi 70 kwa mwezi, hivyo kumudu gharama za uendeshaji wa  miradi mbali mbali ya maendeo, ikiwemo ya maji na barabara.

Amesema hali hiyo imechangia kufanikisha azma ya serikali ya kusomesha wataalamu wake katika fani tofauti, ikiwemo madaktari.

Akigusia historia ya elimu nchini, Dk. Shein amesema Mapinduzi ya 1964 yamekuja kuwakomboa watoto wa wanyonge kutokana an dhuluma ya kukoseshwa elimu.

Ameeleza wakati chama cha ASP kikipigania uhuru, kilibainisha wazi katika Ilani zake, dhamira ya kuipa kipaumbele elimu na kutolewa bila malipo.

Alisema elimu ina umuhimu mkubwa katika maisha ya binadamu, kama Mwenyezi Mungu alivyobainisha katika kitabu kitakatifu cha Quran.

Amesema ni lengo la Serikali katika siku zijazo kujenga skuli za msingi za ghorofa, ili kukidhi mahitaji kutokana na  ufinyu wa ardhi uliopo.

Dk. Shein alichukuwa fursa hiyo kuipongeza taasisi ya Good Neighbor kutoka Jamuhuri ya  Korea Kusini kwa msaada mkubwa wa kufanikisha ujenzi  wa skuli hiyo.

Nae, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Riziki Pembe Juma amesema Wizara hiyo kwa kushirikiana Wizara ya Nchi (OR) Tawala za Mikoa na serikali za Mitaa, Tawala za Mikoa, idara maalum  na Vikosi vya SMZ pamoja na Jamuhuri  ya Korea italiendeleza jengo hilo katika awamu inayofuata.

Waziri Pembe amesema Rais Dk. Shein kuwa huduma za kielimu pamoja na vitabu na madaftari zitaendelea kutolewa bure nchini kote ili kwenda sambamba na Sera ya Elimu.

Mapema,Naibu Katibu Mkuu Wizara ya elimu na maunzo ya Amali Madina Mjaka, amesema ujenzi wa skuli hiyo itawasogeza wanafunzi karibu  na makazi, kama ilivyoainishwa kwenye ilani ya CCM.

Aidha, amesema itapunguza mlundikano wa wanafunzi wa skuli za jirani, hususan Kijitoupele, ambapo kwa sasa darasa moja hujumuisha hadi wanaafunzi 100 – 120.

Ameeleza kuwa awamu ya kwanza ya ujenzi wa skuli hiyo umegharimu zaidi ya shilingi Bilioni 1.5, ambapo skuli hiyo inatarajiwa kuchukuwa wanafunzi 3,780.

Aidha alisema katika kufanikisha ujenzi wa skuli hiyo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imetowa msamaha wa vifaa vya ujenzi pamoja na kuchangia samani.

Wakati huo huo, Dk Shein ameendelea na ziara yake kwa uwekaji wa Jiwe la msingi wa Kituo cha Afya Magirisi, Wilaya ya Magharibi ‘B’ Unguja.

Akizungumza na wananchi Dk. Shein amesema ujenzi wa kituo hicho cha Afya ni jambo la faraja kwa wananachi wa Jimbo la Kijitoupele, akiwashukuru viongozi wa jimbo hilo kwa uamuzi wao wa busara.

Amesema Ilani za Uchaguzi za Chama cha ASP za mwaka 1961 na 1965 ziliweka bayana azma ya Serikali kutowa  huduma za Afya  bila malipo, jambo ambalo Serikali ya Mapinduzi inaliendeleza.

Ameeleza kuwa Mapinduzi ya 1964 yameleta mabadiliko makubwa katika sekta ya Afya  na elimu, mbali na kuwepo kwa changamoto ya ongezeko la watu hapa nchini.

Akinasibishana  kauli hilo, Dk. Shein alisema kituo hicho kina uwezo wa kutoa huduma kwa wastani wa watu 15,000 pekee hivyo hakitoshelezi mahitaji kwa kuzingatia  wananchi 93,119 wanaotarajiwa kukitumia.

Ameishukuru taasisi ya Direct AID kutoka Kuwait kwa kuunga mkono juhudi za viongozi wa jimbo hilo baada ya kukubali kukamilisha hatua iliypobaki ya ujenzi.

Alisema kituo hicho kitakapokamilika kitaweza kutoa elimu ya kinga ya maradhi mbali mbali na kubainisha wazi upatikanaji wa uhakika wa dawa, kutokana na juhudi za Serikali za kuimarisha bajeti ya Wizara ya Afya katika mwaka wa fedha unaoendelea.

Amesema katika mwaka wa fedha wa 2018/19 Serikali imetenga kiasi cha shilingi Bilioni 12.7  kwa ajili ya kuimarisha huduma za Afya, hususan katika suala zima la upatikanaji wa dawa, akibainisha huduma zote muhimu ikiwemo uchunguzi wa magonjwa mbali mbali kupatikana bure.

Dk. Shein ameiagiza Wizara ya Afya kujiandaa vyema, ili pale kituo hicho kitakapofunguliwa kiwe na waataalamu na wafanyakazi wanaotosheleza ili kutoa huduma bora kwa wananchi.

Nae, Mkuu wa Wilaya ya Maghribi “B” Kepteni Silima Haji Haji amesema ujenzi wa kituo hicho kwa kiasi kikubwa kutavipungumzia mzigo vituo vyengine , ikiwemo kituo cha Afya Mwera katika kutoa huduma za Afya.

Mapema, Waziri wa Nchi (OR)Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa, Idara maalum na Vikosi vya SMZ, Haji Omar Kheir amesema Wizara hiyo kwa kushirikiana na Wizara Afya itajenga uzio pamoja na kukipatia wataalamu an wafanyakazi kituo hicho.

Ameipongeza taasisi ya Direct Aid kwa kuendelea kutoa misaada ya kijamii  kwa wananchi wa Jimbo la Kijitoupele baada ya kufanikisha ujenzi wa kisima.

Nae, Mkurugenzi wa Baraza la Manispaa Magharibi “B” Ali Abdalla Said amesema ujenzi wa kituio hicho umegharimu zaidi ya shilingi Milioni 90 ambapo miongoni mwa fedha hizo zinatoka Halmashauri na  mfuko wa Jimbo kupitia Mbunge na Mwakilishi wa Jimbo la Kijitoupele.

Amesema ni matarajio ya kituo hicho pale kitakapokamilika kuweza kutoa huduma bora za afya kwa wananchi wapatao 93,119.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni