Jumapili, 10 Februari 2019

CCM ZANZIBAR YASAMBARATISHA NGOME YA UPINZANI YAVUNA VIGOGO SABA,YASEMA KIMBUNGA CHA SUNAMI YA KISIASA KINAENDELEA.


NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Saadalla ‘Mabodi’ akikabidhiwa kadi ya CHAUMA kutoka kwa aliyekuwa Mwenyekiti wa Vijana wa Chama hicho Wilaya ya Mjini Zanzibar ndugu Salamuu Abdalla Juma ambaye amejiunga na CCM na kupokelewa na viongozi mbali mbali wa UVCCM,UWT,WAZAZI na CCM.
 
 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Saadalla ‘Mabodi’ akikabidhiwa kadi ya uanachama ya Chama cha CHAUMA kutoka kwa  mwanachama wa Chama hicho aliyejiunga na CCM na kupokelewa na viongozi mbali mbali wa UVCCM,UWT,WAZAZI na CCM.



 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Saadalla ‘Mabodi’  na viongozi wengine wa CCM na UWT wakikabidhiwa kadi ya CHAUMA na aliyekuwa Mwenyekiti wa Akina Mama Taifa wa Chama hicho ndugu Salma Mohamed Juma mara baada ya kujiunga na CCM.

 WANACHAMA wapya wa CCM wakila kiapo cha uaminifu mara baada ya kukabidhiwa kadi za CCM na UWT.

 VIONGOZI wa CCM wakiwavisha sare za Chama Cha Mapinduzi wanachama wapya waliotokana CHAUMA.

 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Saadalla ‘Mabodi’  akizungumza na Wajumbe wa Kamati Tekelezaji ya UWT Wilaya ya Dimani katika hafla ya kupokea wanachama wapya wa CCM na Umoja huo.

 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Saadalla ‘Mabodi’  akivishwa sikafu na Vijana wa kikundi maalum cha UVCCM Wilaya ya Dimani mara baada ya kuwasili katika hafla hiyo.

 MAKAMU Mwenyekiti wa UWT Taifa ndugu Thuwayba Kisasi akizungumza kabla ya mgenbi rasmi katika hafla hiyo.

 NAIBU Katibu Mkuu wa UWT Zanzibar Ndugu Tunu Juma Kondo akizungumza katika hafla hiyo.

 BAADHI ya Wajumbe wa Kamati Tekelezaji wa UWT Wilaya ya Dimani wakiwa katika hafla ya kupokea wanachama wapya ndani ya Wilaya hiyo.

NA IS-HAKA OMAR,ZANZIBAR.

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar kimesambaratisha ngome ya Chama Cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA)  kwa kuwang’oa vigogo Saba na Wanachama mbali mbali wa Chama hicho.

Vigogo hao waliong’oka kutoka Chama Cha ukombozi wa umma(CHAUMMA) ni pamoja na aliyekuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Akina Mama Taifa wa Chama hicho Ndugu Salma Mohamed Juma, Mwenyekiti wa Vijana wa Wilaya ya Mjini wa Chama hicho Ndugu Salamuu Abdalla Juma.

Wengine ni Katibu wa Vijana Wilaya ya Mjini ndugu  Mwanabaraka Ali Mohamed, Mjumbe wa chama hicho Wilaya ya Mjini Shadya Juma Khamis, Mjumbe wa Chama hicho  Mkoa wa Magharibi Mariam Peter John  pamoja na Mjumbe wa  ngazi ya wilaya ya Mjini Raya Ali Masoud.

Viongozi hao wa CHAUMA leo wamejiunga rasmi na CCM na kupewa kadi za Chama Cha Mapinduzi na Umoja wa Wanawake wa Tanzania(UWT) hafla iliyofanyika katika Afisiu ya UWT Wilaya ya Dimani Unguja.

Akizungumza mara baada ya kujiunga na CCM, aliyekuwa Mwenyekiti wa Wanawake CHAUMA Taifa, ndugu Salma Mohamed Juma, amekiri kwamba sababu ya kurejea CCM ni kutokana na Utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM unaosimamiwa na Rais wa Zanzibar Dk.Ali Mohamed Shein pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.John Pombe Magufuli.

Ndugu Salma ameweka wazi kwamba mwananchi yeyote ambaye ni mzalendo,mpenda maendeleo ,anayechukia rushwa na ufisadi kwa vitendo hawezi kuendelea kubaki katika Vyama vya upinzani na ndio msaana wao wakaamua kujitoa na kujiunga na CCM.

Kupitia hafla hiyo Kigogo huyo, ametoboa siri ya vyama vya upinzani hasa vilivyounda UKAWA alidai kwamba Chama hivyo vinaongozwa na viongozi mafisadi, wala rushwa,wabinafsi na mawakala wa Mataifa ya kigeni yenye mikakati ya kuhujumu uchumi na maendeleo ya Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.

“Leo najihisi kama nimetoka jela kwani huko tulipokuwa kulikuwa hakuna Demokrasia, Uhuru wa kutoa na kupokea maoni wala kumthamini Mwanamke kama mtu anayesitahiki haki na fursa kama walivyo watu wengine,,,baada ya kunyanyaswa kisiasa kwa muda mrefu ndani ya CHAUMA tumeamua kurudi katika Chama chetu cha asili kinachojali utu na haki za watu wote ambacho ni CCM.

Nimekuwa kiongozi wa ngazi za juu ndani ya CHAUMA nimekutana na vikwazo vingi mpaka nikafikia hatua ya kuacha cheo changu na kuwa mwanachama wa kawaida ndani ya CCM mjue kuwa huko katika upinzani sio sehemu salama ya watu wenye akili timamu kuishi nami nawakaribisha akina mama wenzangu wajiunge na CCM taasisi huru ya kisiasa inayojali maisha ya watu wote.”,alisema Salma.

Naye aliyekuwa kiongozi wa Vijana wa Chama hicho Wilaya ya Mjini ndugu SalamuuAbdallah Juma, alitoa wito kwa vijana waliopo katika vyama vya upinzani kufanya maamuzi sahihi ya kujiunga na CCM kabla ya mwaka 2020 ili wapate uwanja mpana wa kunufaika na fursa mbali mbali za kimaendeleo.

Alisema Vyama vya upinzani vinawaandaa vijana kuwa mabalozi wa vurugu,uchochezi,fitna na siasa za jino kwa jino na sio kuwarithisha elimu na nafasi za uongozi kama kilivyo Chama Cha Mapinduzi.

“ Mimi ni kijana nimeamua kwa ridhaa yangu kujiunga na CCM ili kusaidiana na vijana wenzangu wa Chama hiki  kuendeleza mambo mema ya kuzijenga kiuchumi na kijamii nchi zetu,sambamba na kulinda kwa vitendo dhana ya Umoja na Utulivu kwani ndio chimbuko la maendeleo ya taifa lolote.

Akipokea wanachama hao wapya wa CCM, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdalla Juma Saadalla ‘Mabodi’ , ameeleza kwamba Chama Cha Mapinduzi ndio kimbilio la wananchi wa makundi yote katika jamii.

Ameeleza wananchi wanaotoka katika vyama vya upinzani na kujiunga na CCM sio kwa bahati mbaya wala kushawishiwa bali wanajiunga na taasisi hiyo kutokana na mifumo imara ya kisiasa inayoongoza sera za maendeleo ambazo ni kivutio kwa wananchi wa rika zote.

Alisisitiza kuwa Wapinzani wataendelea ‘kupata tabu sana’ kwani wapo wafuasi wa vyama hivyo makundi kwa makundi wakiwemo vigogo wa ngazi za juu wapo tayari kujiunga na CCM visiwani Zanzibar ambapo kwa sasa wanaandaliwa utaratibu wa kikatiba ili waweze kurudi CCM.

Aliweka wazi kwamba CCM inaendeleza msimamo wake wa kipigo kama kile cha kimbunga cha ‘Sunami’ ndani ya vyama vya upinzani kwa kuhakikisha kabla ya mwaka 2020 vyama hivyo vinabaki bila wanachama na hatima yake vinakosa sifa ya kuwa wawakilishi wa wananchi.

Ameeleza kwamba wanawake wa kiafrika kwa upande wa Zanzibar walidhalilishwa,kudhulmiwa na kuteswa kwa muda mrefu kabla ya Mapinduzi suala lililoondolewa na Chama cha ASP iliyoungana na TANU kasha kuzaliwa kwa CCM inayowathamini wanawake na kuwapa haki na fursa zote za kiuchumi,kijamii na kisiasa.

Dk.Mabodi alieleza kwamba Wanawake wana historia kubwa na ya kipekee ndani ya CCM kwani kundi hilo ndio lililoshiriki kwa kiasi kikubwa kufanikisha Mapinduzi ya Januari 12,mwaka 1964 yaliyowapatia haki,utu na fursa za kimaendeleo jamii ya wakwezi, wakulima na wafanyakazi.

Aliongeza kwamba mbali na hilo Wanawake ndio walioshiriki kuchangia fedha za kujenga jingo la Afisi Kuu ya CCM Zanzibar kisiwandui kwa michango ya fedha kupitia jumuiya ndogo ndogo za Akina mama kwa wakati huo.

 Akitaja tathimini ya uchapakazi kwa wanawake wa UWT alisema wamekuwa wakipigania asilimia 50 kwa kila Nyanja na kwa sasa tayari kinadharia wamefikia asilimia 30 na kwa vitendo wamefikia asilimia 60 hatua ambayo ni ya kupongezwa na kila mpenda maendeleo na umoja na mshikamano.

Katika maelezo yake Dk.Mabodi amesisitiza umuhimu wa Vijana kuthamini Tunu za Taifa ambazo ni Muungano, Mapinduzi, Utu pamoja na Lugha ya Taifa kwani mambo hayo ndiyo yanayochochea umoja na mshikamano kwa wananchi.

Alisema wananchi wanatakiwa kutathimini na kuweka katika uzani mambo yanayotekelezwa na CCM na walinganishe na yale yanayofanywa na Vyama vingine vyenye ruzuku Kisha 2020 watoe hukumu sitahiki kwa kila taasisi ya kisiasa nchini.

Aidha amewakumbusha akina Mama hao kuchangamkia fursa za kuanzisha vikundi vya ujasiriama ili wanufaike na mikopo nafuu kutoka Serikalini ambayo kwa sasa zimetengwa kiasi cha shilingi bilioni 3.6 kwa ajili ya vikundi.

Sambamba na hayo amewasihi wanawake wa UWT katika Wilaya ya Dimani kuachana na tabia za fitna na kumakundi ya kuwania nafasi za uongozi kwani mambo hayo yasipochukuliwa hatua za kinidhamu yanaweza kuharibu sifa ya maendeleo ndani ya Wilaya hiyo.

Naye Makamu Mwenyekiti wa UWT Taifa Thuwayba Kisasi, aliwashukru akina mama wote waliojiunga na CCM pamoja na umoja huo, na kuwaeleza kuwa taasisi hiyo haina ubaguzi wala siasa za chuki na visasi hivyo akawasihi akina mama na vijana warudi nyumbani kumenoga.

Awali Naibu Katibu Mkuu wa UWT Zanzibar ndugu Tunu Juma Kondo, aliseleza kwamba kipaumbele mahsusi cha taasisi hiyo ni kuongeza wanachama kwa wingi ndani ya CCM na UWT ili 2020 CCM iendelee kushinda na kubaki madarakani.

Akizungumza Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Magharibi Ndugu Zainab Ali Maulid amesema Akina Mama ndani ya Mkoa huo wamekuwa na muamko mkubwa wa kushiriki katika shughuli mbali mbali za kimaendeleo zinazowapatia fursa za kujifunza masuala mbali mbali ya kujiwezesha wenyewe.

Alisema hafla hiyo ni miongoni mwa mwendelezo wa ziara yake ya kujitambulisha kwa wanachama na viongozi wa CCM na Jumuiya zake toka ateuliwe kushika nafasi hiyo, pia amewashukru wanachama wote walioshiriki katika mapokezi yake.

Katika taarifa yao UWT Wilaya ya Dimani, wameeleza kwamba taasisi hiyo imeanzisha miradi ya ufugaji wa kuku wa nyama na mayai ili kuondokana na mifumo ya utegemezi wa ajira kutoka serikalini ambapo miradi hiyo imetolewa na Wawakilishi wa Viti Maalum ndani ya Wilaya hiyo.

Pamoja na hayo ameeleza kwamba katika kuadhimisha miaka 42 ya kuzaliwa kwa CCM wamefanya ziara ya kuwafariji Watoto yatima wa Kituo cha African Muslim Agency kwa lengo la kusikiliza changamoto zao na kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu.

Kupitia taarifa hiyo walieleza kuwa ndani ya Wilaya hiyo Wabunge, Wawakilishi, Madiwani, CCM,UWT,Jumuiya ya Wazazi na UVCCM wanashirikiana katika masuala mbali mbali ya kuimarisha Chama Cha Mapinduzi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni