Jumanne, 19 Februari 2019

DK.SHEIN ASEMA MCHANGA UNATOWEKA, AWATAKA WANANCHI KUTAFUTA NJIA MBADALA.

 RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akiwa na Mawaziri mbali mbali wa SMZ akikagua eneo linalochimbwa Mchanga la Donge Chechele.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewataka wananchi watambue kuwa kuna uhaba mkubwa wa mchanga hivi sasa hapa Zanzibar kutokana na uchimbaji mbaya wa rasilimali hiyo unaofanyika.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika ziara yake ya Wilaya ya Kaskazini B Unguja wakati alipotembelea maeneo yanayochimbwa mchanga huko Pangatupu, Chechele na Kiombamvua na kujionea jinsi maeneo hayo yalivyoathirika kutokana na rasilimali hiyo kuanza kumalizika kabisa.

Katika ziara hiyo ambapo Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd na Mama Mwanamwema Shein walishiriki kikamilifu, Rais Dk. Shein aliwataka wananchi wajue uhaba uliopo wa rasilimali hiyo ya mchanga.

Akiwa katika eneo la Pangatupu na Chechele, Rais Dk. Shein alieleza kuwa rasilimali ya mchanga hapa Zanzibar imeanza kutoweka na haipo hivyo kuna haja ya kuweka mikakati maalum ya kunusuru huo mchache uliobakia ambapo tayari Serikali anayoiongoza imeshaanza kazi hiyo.

Alieleza kuwa tayari ameshawapa kazi Mawaziri wake watatu pamoja na Kamati yao ya Makatibu Wakuu kufuatilia hali hiyo kwani tayari kwa upande wake hivi karibuni aliagiza shughuli za uchimbaji wa mchanga kusisitiswa.

Aliongeza kuwa Serikali imefanya hivyo si kama inawakomoa wananchi wake bali inatafuta utaratibu wa kufanya ili rasilimali hiyo iwasaidie wananchi wote kwani tayari kuna wafanyabiashara wameshahodhi mchanga katika maeneo yao ya biashara hasa wale wanaofanya biashara ya matofali.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwataka waandishi wa habari waliokuwepo katika eneo hilo na wale waliokuwa hawapo katika ziara yake hiyo kuwaeleza wananchi ukweli juu ya uhaba wa rasilimali hiyo ambayo wao wenyewe hali hiyo wameiona.

Akiwa katika eneo la Kiombamvua, Dk. Shein alipata maelezo kutoka kwa uongozi wa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi pamoja na kutoka kwa Sheha wa Shehia ya Kiombamvua Mohamed Ali Ame ambaye aliomba aondolewe mchanga uliokusanyika kondeni kwake ili aendelee na kilimo ambapo mchanga ulipelekwa na maji na jumla ya tani 2,020 zilichukuliwa na Kampuni ya CRJ kwa ajili ya matumizi ya mradi wa ujenzi wa misingi ya maji ya mvua.

Katika majumuisho yaliokwenda sambamba na mazungumzo na viongozi wa CCM wa Wilaya hiyo huko katika hoteli ya “SeaCliff” Kama Wilaya ya Kaskazini B, Dk. Shein alisema kuwa wapo wafanyabiashara wa matofali wameuficha mchanga kwenye maeneo yao hali ambayo imekuwa usumbufu kwa wananchi wanaotaka kujenga.

Akieleza historia ya uuzaji wa mchanga, udongo, mawe na kifusi ulivyokuwa hapo zamani, Dk. Shein alisema kuwa kunatofauti kubwa na biashara hiyo inavyofanywa hivi sasa hali ambayo inachangia uhaba wa rasilimali hiyo.

Alisema kuwa katika shimo la mchanga la Pangatupu mchanga umemaliza na zimebaki tani 50,000 tu za mchanga ambao haufiki hata miezi miwili ambapo mchanga wa CheChele nao umebaki tani 2000 tu ambao umewekwa kwa ajili ya miradi ya Serikali.

Alisema kuwa jengo la Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati Zanzibar (ZURA) limesita ujenzi wake kutokana na ukosefu wa mchanga na kupelekea mafundi wa ujenzi kutoka kampuni ya Hainan International kutoka China kukaa bila ya kazi.

Alieleza kuwa licha ya Serikali kusimamia rasilimali hiyo hivi sasa ambapo hatua hizo zilianza mnamo mwezi Machi na Novemba mwaka jana 2017 bado kumetokea wananchi ambao wanahoji na kusema kuwa Serikali inawachukulia mchanga wao.

Alisisitiza kuwa ni vyema wananchi wakaelewa kuwa ardhi yote ya Zanzibar ni mali ya Serikali hivyo rasilimali ya mchanga yote ni mali ya Serikali kwa mujibu wa Sheria na Katiba ya nchi na yeye ndie msimamizi wa ardhi hiyo.

Pia, alieleza kuwa jambo jengine lililochangia kwa kiasi kikubwa kutokea uhaba wa rasilimali hiyo ni pamoja na kutofuatwa kwa sheria za nchi kwani tayari kila kitu kina sheria yake huku akieleza kuwa baadhi wa viongozi na wananachi wa Wilaya hiyo wamechangia kutokea kwa athari hiyo iliyopelekea uhaba wa mchanga.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa juhudi za makusudi zimechukuliwa ikiwa ni pamoja na kuzungumza na wananchi wa maeneo yanayochimbwa mchanga yakiwemo maeneo ya Donge ambapo aliwatuma Mawaziri wake waende kuzungumza nao ili watambue hali iliyopo hivi sasa.

Dk. Shein alisema kuwa Serikali imo katika kufanya utaratibu ili mchanga mchache uliopo uweze kutumika vizuri na uwafae wananchi wote na wala haikusudii kuwasumbua wananchi wake juu ya matumizi ya rasilimali hiyo hapa Zanzibar.

Aidha, alisema kuwa Serikali ina kazi kubwa ya kuwaelimisha na kuwaeleza wananchi juu ya hali ya mchanga ilivyo hivi sasa hapa Zanzibar.

Alisema kuwa wapo baadhi ya wafanyabiashara walitaka kuruhusiwa waagize rasilimali hiyo kutoka Tanzania Bara lakini Serikali imekataa huku akisisitiza kuwa kwa upande wa kisiwa cha Pemba rasilimali hiyo ipo lakini bado inatosheleza kwa wananchi wa kisiwa hicho.

Nae Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Mariam Juma Abdalla Sadalla alieleza kuwa uchimbaji chini ya usimamizi wa moja kwa moja wa Serikali ulianza katika mwezi Machi 2017 katika eneo la Donge Chechele na baadae mnamo mwezi wa Novemba 2017 kuhamia eneo la Pangatupu ambalo lilikuwa shamba la miwa chini ya Kiwanda cha Sukari Mahonda.

Alieleza kuwa eneo la Pangatupu lenye hekta 64 limebaki tani 50,000 tu za mchanga huku akieleza kuwa baada ya Wizara hiyo kusimamia kiasi cha TZS Bilioni 11 zimepatika ambazo hugaiwa kwa Halmashauri,Wizara na Hazina.


Katibu Mariam alieleza kuwa jitihada imekuwa ikifanyika ya kupanda miti ikiwemo mikeshia na mihojoro ambapo tayari hekta 56 zimepandwa miti ipatayo 2000 kuanzia mwaka 2016 hadi mwaka huu wa 2019 na kueleza kuwa eneo hilo limetoa ajira 700 ambalo lina Jumuiya mbili ikiwemo ya Madereva na Jumuiya ya Wapakizi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni