Jumapili, 21 Januari 2018

DK.MABODI: AMEWAAGIZA WASOMI WA CCM KUFANYA UTAFITI UTAKAOLETA MATOKEO CHANYA


NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.


 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Abdulla Juma Saadalla ‘Mabodi’ akifungua Mkutano Mkuu wa Uchaguzi wa Shirikisho la Vyuo Vikuu Seneti ya Unguja uliofanyika Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui Zanzibar.

 MAKAMU Mwenyekiti wa CCM Taifa Tabia Maulid Mwita akizungumza na kusisitiza juu ya umuhimu wa vijana wa UVCCM hasa wa shirikisho hilo kusoma Kanuni na miongozi mengine ya Kikatiba ili kutambua wajibu wao.

MWENYEKITI wa Shirikisho hilo aliyemaliza muda wake Khamis Kheri Ame akitoa nasaha zake katika mkutano huo. 

Wajumbe wa Shirikisho la Vyuo Vikuu CCM seneti ya Unguja wakimsikiliza Mgeni rasmi Naibu katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Saadalla ‘Mabodi’ wakati akifungua  mkutano wa Uchaguzi wa seneti hiyo uliofanyika Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui Zanzibar.


 
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar kimewaagiza  vijana wasomi wa Chama hicho kuanzisha utamaduni wa kufanya Tafiti mbali mbali za kitaalamu ili kubaini baadhi ya changamoto zinazokabili kundi la vijana na jamii kwa ujumala  hasa upungufu wa ajira.

Agizo hilo amelitoa wakati akifungua Mkutano wa Uchaguzi wa Shirikisho la Vyuo vikuu CCM Unguja la kuwachagua viongozi  Watano wa Seneti ya Unguja, ambapo Mkutano huo umefanyika katika Afisi Kuu CCM Kisiwandui Mjini Zanzibar.

Dk.Mabodi alisema Wasomi wa Vyuo vikuu ndani ya CCM ni lazima wakubali mabadiliko ya nyakati kwa kufanya kazi zao za kisiasa, kiuchumi na kijamii katika mfumo wa Sayansi na Teknolojia kwa lengo la kuleta mabadiliko chanya ndani ya taasisi hiyo imara ya Kisiasa.

Alisema nchi zilizoendelea duniani zinategemea msaada mkubwa wa wasomi ambao ni vijana waliohitimu fani mbali mbali katika vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu ambao wana uwezo na maarifa  ya kitaalamu yanayochochea ufanisi wa kimaendeleo.
Pia, aliongeza kwa kueleza kwamba CCM ina utajiri wa Rasilimali watu waliobobea katika fani mbali mbali hivyo ni lazima watoe mchango wao katika kuandaa mipango mikakati ya kukiletea chama hicho ushindi wa kishindo katika Uchaguzi Mkuu wa Dola mwaka 2020.

Hata hivyo amesema vijana hao wa Vyuo vikuu wana wajibu wa kusoma alama za nyakati kwa kuwa mfano bora wa kubuni na kutekeleza kwa vitendo mikakati mbali mbali ya kiuchumi na kijamii ili vijana vya vyama vya upinzani wavutiwe na utamaduni huo na kujiunga na hatimaye kujiunga na Chama cha Mapinduzi.

Akizungumzia fursa zinazotokana na usimamizi pamoja na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020 alitaja mchakato wa Utafiti wa Uchimbaji wa mafuta na Gesi Zanzibar  kuwa ni sehemu muhimu inayohitaji vijana wasomi watakaolinda rasilimali hiyo isifilisiwe na nchi za kigeni.

Alisema fursa ya kuanza utafti huo ni miongoni mwa matunda ya Mapinduzi ya Zanzibar ya  mwaka 1964 chini ya uongozi wa aliyekuwa Rais wa kwanza wa nchi hiyo Marehemu Mzee Abeid Amani Karume, aliyeasisi mfumo rasmi wa Zanzibar kujitawala kiuchumi, kisiasa na kijamii.

“ Utafiti huu umeanza mwaka 1952 ambao ulibaini ndani ya Ardhi na mwambao wa visiwa vya Zanzibar kuwepo kwa dalili za rasilimali hiyo inayoingia katika kundi la madini asilia, na juhudi ziliandelea hadi kufikia Serikali ya awamu ya saba chini ya Uongozi wa Rais wa Zanzibar Dk.Shein kupigania suala hilo likapewa baraka za kisheria zilizoruhusu Zanzibar  kushugulikia yenyewe mchakato wa utafiti hadi uchimbaji”,. Alieleza Dk.Mabodi.

“ Nyinyi ni wasomi ambao jamii ya Wazanzibar na Watanzania kwa ujumla wanakutegemeeni mlete mabadiliko ya kweli ndani ya Chama chetu na Serikali zote mbili zinazotokana na CCM.

Lakini pia ni lazima muwe wabuni  kwa kufanya utafiti ndani na nje ya CCM kwa lengo la kupata takwimu sahihi za mambo  mbali mbali yatakayosaidia Chama kuimarika kisiasa kutokana na mingo yake kutekelezwa Kisayansi.”, alisema.

Akizungumzia kwa ufupi historia ya Zanzibar  Dk.Mabodi alisema kuwa maandiko mbali mbali ya historia yanadhibitisha kuwa Zanzibar kabla ya kutawaliwa na Wakoloni ilikuwa na Utawala wake wa jadi uliokuwa katika mfumo wa ujima, ambao wananchi wake waliishi kwa amani , ujamaa na kujitegemea.

Alisema kupitia muongozo huo wa historia ni lazima vijana wa sasa wajijue kuwa wana jukumu la kuhakikisha CCM iliyotokana na vyama vya ASP na TANU inaendelea kutawala na hakuna Chama chochote cha upinzani kitakachoshika madaraka.

Akizungumzia  Uchaguzi wa viongozi mbali mbali wa Shirikisho hilo alisema ni lazima wachague viongozi bora wenye uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa waliowachagua bila ya kusukumwa.

Pamoja na hayo aliwasisitiza wajumbe wa Mkutano huo kuhakikisha wanachagua wenye uwezo na uthubutu wa kujenga hoja imara na kujibu hoja za wapinzani  bila ya kuteteleka.

Aliwataka wasimamizi wa Uchaguzi huo kutenda haki bila ya upendeleo wa mgombea yeyote ili kulinda heshima ya CCM na kuruhusui mkondo wa Demokrasia ifanye kazi yake kwa mujibu wa miongozo na kanuni za uchaguzi.

Naye Makamu Mwenyekiti wa UVCCM Taifa Tabia Maulid Mwita alisema mafanikio yaliyopatikana Zanzibar katika sekta mbali mbali yametokana na juhudi za kiutendaji na ushiriki  wa vijana wasomi wa Chama hicho.

Ametoa nasaha wa vijana hao kuwa ili kufikia malengo waliojiwekea kisiasa ni lazima wafanye kazi  kwa bidii ili kukisaidia chama kufikia malengo yake ya kushika dola kila uchaguzi mkuu na chaguzi ndogo ndogo.

Pamoja na hayo alisisitiza umuhimu wa vijana wa shirikisho hilo la vijana wa CCM wa vyuo vikuu kusoma Katiba ya CCM pamojana na kanuni ya UVCCM kwa lengo la kutambua wajibu,haki zao pamoja na mipaka yao kiutendaji.

Akitoa salamu za Mwenyekiti wa Umoja huo Kheri James, Tabia alisema kuwa kiongozi huyo anawasihi waendelee kuwa wamoja kwa kila jambo jema lenye malengo ya kuleta manufaa ndani ya CCM na Serikali zote mbili ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mapema Mwenyekiti anayemaliza  muda wake katika Shirikisho hilo Khamis Kheri Ame alisema lengo la uchaguzi huo ni kutimiza matakwa ya Kikatiba yanayoruhusu mabadiliko ya awamu za uongozi kwa kila kipindi cha miaka mitatu.

Pamoja na hayo amewashukru wajumbe wa Shirikisho hilo alioshirikiana nao kwa kipindi chote cha uongozi wake na kuwataka viongozi wapya watakaochaguliwa kuhakikisha wanalivusha salama shirikisho hilo kuelekea ng’ambo ya maendeleo endelevu.


Katika Uchaguzi huo wanachaguliwa viongozi mbali mbali ikiwemo nafasi ya  Mwenyekiti, Katibu, Katibu wa hamasa pamoja na wajumbe wawili wa Kamati ya Uratibu.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni