Ijumaa, 12 Januari 2018

DK.SHEIN: KUANZIA MWEZI JULAI MWAKA HUU ELIMU YA SEKONDARI BURE







RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein ametangaza kuanzia Julai mwaka huu serikali yake itaanza kutekeleza azma ya kurudisha utoaji wa elimu bure katika shule za Sekondari ili kuendelea  kwa vitendo Shabaha ya Mapinduzi ya Januari 12,1964.

Amesema kuwa hatua hiyo itahusisha elimu ya ngazi ya msingi hadi sekondari na kwamba katika kipindi cha miaka 54 ya mapinduzi hayo SMZ inajivunia kuimarika kwa huduma za elimu ambapo kabla ya Mapinduzi shule zilikuwa chache na zikitolewa kwa ubaguzi na zilikuwa za kulipia.

Rais Dk.Shein alitangaza neema hiyo wakati akihotubia wananchi katika sherehe za kuadhimisha miaka 54 ya Mapinduzi kwenye uwanja wa Aman Karume,ambapo alisema kutokana na juhudi za serikali ya SMZ sekta ya elimu imeendelea kuimarika huku shule za msingi zikiongezeka mara saba.

Awali kabla ya kuhutubia, Rais, Shein ambaye alikuwa ni mgeni rasmi aliingia katika uwanja huo saa 2:56 asubuhi ambapo alipanda gari maalum la wazi na kupigiwa mizinga 21 ya heshima na kupata fursa ya kukagua gwaride liloandaliwa katika sherehe hizo.

Kabla ya kuingia Dk.Shein, alitanguliwa na Rais Dk.John Magufuli ambapo aliingia saa 2:35 asubuhi naye alipata fursa ya kupanda jukwa maalum ambalo alipokea salamu za heshima kwa ajili ya kukaribishwa katika sherehe hizo.

Sherehe hizo zilihudhuriwa na viongozi wa serikali na Chama Cha Mapinduzi(CCM) wakiwemo Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, Makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi.

Wengine ni Marais wa wastaafu akiweo wa awamu ya tatu Benjamini Mkapa, Rais Mstaafu wa awamu ya pili Ali Hassan Mwinyi, Rais Mstaafu wa awamu ya nne Jakaya Kikwete na Rais wa Zanzibar wa awamu ya sita Aman Abedi Karume. 

Sherehe hizo ziliambatana na maandamano yaliyoandaliwa kutoka kwa wafanyakazi wa taasisi za serikali na vyama vya siasa ambao walibeba mabango mbalimbali yalikuwa na ujumbe tofauti tofauti iliolenga kusherekea madhimisho ya mapinduzi ya miaka 54.

 Dk.Shein aliongeza kuwa kwa upande wa shule za Sekondari zimeongezeka mara 53 huku idadi ya wanafunzi wa shule za Msingi na sekondari zikiongezeka mara 14 kutoka wanafunzi 25,372 kwa mwaka 1963 hadi wanafunzi 378,211 kwa mwaka 2017.

"Ni wazi kuwa baada ya mapinduzi kufaulu tatizo ambalo walilotengeneza wakoloni kuwa watoto wa wafanyakai na wakulima tusiingie sekondari na kupata elimu ya juu, leo  halipo tena na kwamba haya ni mafanikio makubwa yakupigiwa mfano,"alisema.


Alitaja juhudi za serikali ya SMZ katika sekta hiyo ya elimu kuwa katika jitihada za kuhakikisha inaongeza madarasa kwa mwaka 2017 serikali yake ilianza ujenzi wa shule 9 za ghorofa za sekondari kwa Unguja na Pemba.

Rais Dk.Shein alisema pamoja na hatua hzio serikali yake imeendelea kushughulikia suala la ununuzi wa madawati yote kw ajili ya shule zote za Unguja na Pemba hivyo kutokana na hatua zinachukuliwa katika kukusanya fedha inatarajiwa tatizo la uhaba wa madawati kumalizika mwaka huu.

"Mipango yetu ya elimu imepata mafanikio makubwa ambapo sasa Zanzibar ina vyuo vikuu vitatu vinavyoendeshwa na wataalamu wetu wenyewe ambapo wanafunzi 1,800 wa fani mbalimbali wanahitimu kwenye vyuo vikuu visiwani humu kila mwaka kwa hivyo Zanzibar itajitosheleza kwa kuwa na wataalamu wake wenyewe hivi karibuni," alisema.

 Mbali na hilo, Rais Dk.Shein aliongeza kuwa serikali yake ya SMZ imechukua juhudi kubwa za makusudi katika kuimarisha huduma za afya ambapo sera mpya ya afya ya mwaka 2014 inatekelezwa katika kuwapa wananchi huduma hizo bila ya malipo kutokana na malengo ya Mapinduzi.

"Hivi sasa huduma za afya zinatolewa katika hospitali za serikali 12 baadala ya  hospitali 5 na vituo vya afaya 158, badala ya 36 vilivyokuwepo kabla ya mapinduzi na vilevile huduma za afya zinatolewa na hospitali za vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na Idara ya Maalum za SMZ, mpango ambao kabla ya mapinduzi haukuwepo,"alisema Dk.Shein

Rais Dk.Shein aliendelea kueleza namna katika kipindi cha miaka 54 ya mapinduzi hayo serikali ya SMZ inavyojivunia ambapo mafanikio katika sekta hiyo ya afya imeendelea kuimarika ikiwemo ununuzi na upatikanaji wadawa na vifaa tiba.

Alisema katika kipindi cha mwaka wa fedha 2016/2017 serikali yake ya SMZ ilitenga sh.bilioni 4.9 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba ambapo kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2017/2018 serikali imetenga sh.bilioni 7 na hivyo kwa zaidi ya hayo kwa mwaka wa fedha 2018/2019 imetenga bajeti ya jumla ya wizara ya afya sh.bilioni 12.

"Katika kujivunia mafanikio yaliopatikana katika kipindi cha miaka 54 ya mapinduzi serikali ya SMZ imeendelea kutambua umuhumi wa kilimo ambapo wakulima wamepatiwa ruzuku ya asilimia 75 ya pembejeo na huduma za matrekta hivyo hatua hiyo imepekea mavuno ya mpunga kuongezeka kutoka tani 33,655.06 za mpunga kwa mwaka 2013 hadi tani 39,000 kwa mwaka 2017,"alisema.

Katika hotuba yake Rais Shein alitumia fursa ya kumpongeza Rais Dk.Magufuli katika jitihada zake za kuingoza Tanzania katika kupambana na vitendo vya rushwa, ufisadi, uhujumu uchumi, dawa za kulevya na kulinda rasilimali na kwamba kila mtu ana wajibu wa kumuunga mkono.

Alisema Serikali ya SMZ itaendelea kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano katika kuendeleza na kuimarisha Muungano katika kushirikiana kwenye mambo yasiokuwa ya Muungano kwa faida ya pande zote mbili.

"Mimi na Mwenzangu Rai Dk.Magufuli tunatambua dhamana tulionayo katika kuhakikisha kuwa muungano wa Tanzania unadumu na unaimarika kwa dhamira ile ile ya viongozi wetu wa awamu zilizotangulia hivyo ninawahakikishia wananchi kuwa serikali zetu hizi mbili zitaendelea kuchukua hatua ili nchi yetu iendelee kupiga hatua kubwa zaidi na ibaki kuwa nchi ya amani na utulivu,"alisema Rais Dk.Shein. 

alieleza kuwa katika kuwahudumia wakulima visiwani humo kwa msimu wa mwaka 2017/2018 tani 1,800 za mbolea, tani 350 za mbegu ya mpunga na lita 15,000 za dawa za kuulia magugu zimenunuliwa na zinatarajiwa kusambazaw kwa wakulima hao.

"Pia katika kuhakikisha kuwa huduma za matrekta zinakua za uhakika visiwani humu serikali imeanzisha wakala wa serikali wa huduma za Matrekta na zana nyinginezo za kilimo ambapo mbali na matrekta ya zamani yaliopo kwenye kiwanda cha matrekta, SMZ imetiliana saini hati ya maelewano na kampuni ya Mahindra Mahindra ya India ya kununua matrekta 100 na matrekta 20 kutoka kampuni ya Mahindra Mahindra tayari yamekwishaagizwa,"alisema Rais Dk.Shein.

Pia, aliongeza kuwa serikali yake imeanzisha kituo cha kutotolea vifaranga vya samaki kilichopo Beit el Raas kwa kushirikiana na serikali ya Japan na FAO chenye uwezo wa kuzalisha vifaranga milioni 10 kwa mwaka.

"Aidha, serikali ya SMZ imeanzisha kampuni ya uvuvi ya Zanzibar(ZAFICO) kwa mtaji wa sh.bilioni 7 ambapo imeamua kununua meli mbili za uvuvi kwa ajili ya kufanya shughuli hiyo ya uvuvi visiwani humo,"alisema.

Rais Dk.Shein alisema katika mwaka wa tatu wa kipindi cha pili cha mwaka 2017/2018 cha awamu ya saba serikali ya SMZ imetekeleza vyema ilani ya Chama Cha Mapinduzi(CCM),  ya uchaguzi wa mwaka 2015-2020, MKUZA 3, na dira ya Maendeleo 2020 na hivyo kupata mafanikio ya kuridhisha.

Alisema juhudi kubwa zilizochukuliwa na serikali ya SMZ katika kuimarisha uchumi zimewezesha kuongezeka kwa ukusanyaji wa mapato ambapo sh.bilioni 548.571 zilikusanywa katika mwaka 2017 ikilinganishwa na sh.bilioni 487.474 kwa mwaka 2016.

"Katika mwaka 2017 mapato yameongezeka kwa sh.bilioni 61.097 ikilinganishwa na makusanyo ya ikilinganishwa na makusanyo ya mwaka 2016 ikiwa sawa na ongezeko la asilimia 12.5 hivyo natoa pongezi kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania na Bodi ya Mapato Zanzibar(ZRB) za juhudi za ukusanyaji wa mapato"alisema.

Pia, alisema katika sekta ya utalii imeendelea kuimarika ambapo watalii 433,116 waliingia visiwani humo, katika mwaka 2017 ikilinganishwa na idadi ya watalii 379,242 waliongia katika kipindi cha mwaka 2016 ambapo ni sawa na ongezeko la asilimia 14.2.

"kuongezeka kwa idadi ya watalii visiwani humu inaonesha wazi kuwa lengo la kufikia watalii 500,000 ifikapo mwaka 2020 litafananikiwa kabla ya mwaka huo na kwamba kwa upande wa biashara kati ya Zanzibar na Tanzania bara inaendelea vizuri ambapo bidhaa zenye thamani ya sh.bilioni 32.32 zilisafirishwa kwenda Tanzania bara na bidhaa zenye thamani ya sh.bilioni 184.84 zilisafirishwa kutoka Tanzaia bara kuja Zanzibar kwa kipindi cha Januari hadi Desemba mwaka 2017,"alisema Rais Shein.

Viongozi mbali mbali wa Kitaifa walioudhuria katika sherehe hiyo ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Samia Suluhu Hassan  Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mzee Ali Hassan Mwinyi, Rais mstaafu wa Awamu ya tatu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania William Benjamini Mkapa, Rais mstaafu wa awamu ya nne wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete pamoja na Rais Mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Dkt.Amani Abeid Karume. 

Wengine ni Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi(CDF) Jenerali Venance Mabeyo, Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar Zubeir Ali Maulid, Makamu wa Rais mstaafu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.mohamed Gharib Bilal  Mke wa alikuwa Rais wa awamu ya kwanza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mama Fatma Karume.

Viongozi wa vyama vya kisiasa ni MAKAMU Mwenyekiti wa CCM Tanzania bara Philip Mangula, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdalla Juma Saadalla Mabodi, Mwenyekiti wa Chama cha Wakulima(AFP) Said Soud, Makamu Mwenyekiti wa Chama cha ADA-TADEA Juma Ali Khatib.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni