Jumamosi, 11 Agosti 2018

TAASISI ZA VIJANA ZANZIBAR ZAJADILI MAAZIMIO 14 YA VIJANA


 WAZIRI wa Fedha na Mipango Zanzibar Dkt.Khalid Mohamed Salum akifungua mkutano wa kujadili maazimio ya kongamano la siku ya vijana Duniani uliofanyika hoteli ya Ngalawa Bububu.

 MWENYEKITI wa Baraza la Vijana Zanzibar, Khamis Rashid Kheir akizungumza katika mkutano huo.

 MAKAMU Mwenyekiti wa UVCCM Taifa, Tabia Maulid Mwita akisoma maazimio hayo 14 yaliyowasilishwa katika kongamano la vijana 300 lililofanyika Augost 9 mwaka huu.

 MWENYEKITI wa muda Mkutano huo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Vijana Zanzibar Khamis Rashid akiongoza mkutano huo wa kujadili maazimio 14 ya vijana.
 WAZIRI wa Afya Zanzibar Mhe. Hamad Rashid Mohamed akizungumza katika mkutano huo.

 MBUNGE wa viti maalum (CCM) kupitia nafasi za Vijana katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Khadija Nassir  Ali akichangia maazimio mbali mbali katika mkutano huo.
MWENYEKITI wa CCM Mkoa wa Mjini Talib Ali Talib akizungumza katika Mkutano huo.


NAIBU Mkurugenzi wa Manispaa ya Mjini Zanzibar , Said Natepe akizungumza katika mkutano huo.

MJUMBE wa Kamati Kuu ya CCM Taifa Leila Burhan Ngozi akizungumza katika mkutano huo.

NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Saadalla Mabodi akichangia juu ya mikakati ya CCM ya kuwezesha vijana.

KATIBU Mkuu Wizara ya Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo Zanzibar Omar Hassan Omar akizungumza katika Mkutano huo.

 BAADHI ya washiriki wa mkutano huo.


 MKUU wa Mkoa wa Mjini Magharib Ayoub Mohamed Mahmoud akifunga Mkutano huo wa siku moja uliofanyika katika Hoteli ya Ngalawa Bububu Nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.


NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.

WAZIRI wa Fedha na Mipango Zanzibar Dkt.Khalid Salum Mohamed amesema uchumi wa Zanzibar utaendelea kukua kwa kasi endapo vijana watashirikishwa ipasavyo katika mipango ya maendeleo.

Alibainisha kwamba taifa lolote linaloshindwa kushirikisha ipasavyo kundi hilo katika mikakati yake ya kimaendeleo basi taifa hilo haliwezi kupata maendeleo badala yake uchumi wake utayumba na kuendelea kuwa tegemezi kwa mataifa yaliyoendelea.

Hayo aliyasema wakati akifunga mkutano wa kujadili maazimio 14 ya kongamano la siku ya vijana duniani kwa viongozi mbali mbali lililofanyika katika hoteli ya Ngalawa nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.

Dkt.Khalid alisema serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa juhudi zake za kuwaweka karibu vijana ilianzisha kwa makusudi Baraza la Vijana la Taifa ili kundi hilo lipate sehemu maalum ya kukutana pamoja na kujadili masuala mbali mbali ya kuisaidia nchi kiuchumi, kijamii na kisiasa.

Alieleza kuwa vijana ndio nguvu kazi ya taifa lolote kwani kila jambo jema la kuiletea nchi manufaa linasimamiwa kwa kiasi kikubwa na kundi la vijana wenye taaluma na uwezo mzuri wa kufikri mawazo chanya ya kuisadia nchi kimaendeleo.

Alisema siri ya mafanikio katika nchi mbali mbali zilizoendelea kiuchumi ni kutokana na mbinu za kutumia vizuri rasilimali watu ya vijana, waliosaidia kuinua kwa kasi mikakati endelevu ya kiuchumi na kijamii kupitia sekta mbali mbali hasa za uzalishaji mali na viwanda.

Waziri Dkt. Khalid alizitaja takwimu za kiuchumi, kwa kufafanua kuwa mwaka 2018 uchumi wa Zanzibar unatarajia kukua kwa asilimia 7.7 ikilinganishwa na mwaka, 2017 ambapo umekuwa kwa asilimia 7.5.
Alisema uchumi huo ni lazima uwe jumuishi na endelevu unaogusa makundi yote ya kijamii.

“Wananchi sote lazima tushiriki kupanga na kukuza uchumi wetu ili uwe endelevu na wenye maslahi ya kutunufaisha wote, na hapo ndipo tutakapokuwa tumefikia malengo ya serikali ya kufikia kiwango cha nchi zenye uchumi wa kati.

Imani yangu kwa nyie vijana mlioshiriki kongamano hili na wengine waliopo katika shughuli mbali mbali za ujenzi wa taifa ambao hawakuweza kujumuika nasi hapa, leo hakika matarajio haya yatafikiwa kwa haraka na kwa ufanisi.

Aliwasisitiza vijana kuendeleza utamaduni wa kufanya kazi kwa bidii na kuachana na mazoea ya kubagua kazi kwa kigezo cha kusubiri ajira kutoka serikalini.

Alisema hakuna nchi iliyoweza kuwaajiri vijana wote kwani sekta binafsi ndio chombo pekee chenye fursa pana za kutosheleza mahitaji ya ajira kutokana na wingi wa vijana.

Kupitia sekta binafsi serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaimarisha sekta mbali mbali zikiwemo za kilimo cha kisasa cha umwagiliaji, kuboresha uvuvi wa bahari kuu na kuwa wa kisasa wa kuwasaidia vijana kujiajiri wenyewe.

Pia serikali imetenga zaidi ya shilingi bilioni tatu kutekeleza sera ya viwanda Zanzibar, sekta ambayo endapo wananchi wataipokea kwa dhati itaweza kupunguza au kumaliza kabisa changamoto za ajira nchini.

Pamoja na mikakati hiyo Dkt. Khalid alibainisha kwamba serikali imekusudia kuwekeza zaidi katika sekta ya utalii ili uwe sehemu mahsusi ya kuongeza pato la taifa, sambamba na kuimarisha kwa vitendo dhana ya utalii kwa wote.

Alitoa wito kwa vijana kuthamini, kutangaza na kuunga mkono hatua za maendeleo zinazofanywa na serikali ya awamu ya saba chini ya uongozi wa Dk. Ali Mohamed Shein, katika utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya mwaka 2015/2020.

Akizungumza Mwenyekiti wa Baraza Vijana Zanzibar, Khamis Rashid Kheir amesema kongamano hilo limefungua fursa mbali mbali za vijana ambao wengi wao wamepata kujua sehemu sahihi za kuwasilisha changamoto zao na zikafanyiwa kazi kwa haraka.

Naye Makamu Mwenyekiti wa UVCCM Taifa Tabia Maulid Mwita, akiwasilisha maazimio 14 yaliyotolewa na vijana 300 walioshiriki katika kongamano la kuelekea maadhimisho ya siku ya  vijana Duniani yaliyofanyika August 9 mwaka 2018, alisema vijana wanatakiwa kuzitumia vyema fursa za kilimo, ufugaji na uvuvi ili kujiajiri wenyewe.

Makamu Mwenyekiti wa UVCCM Taifa Tabia, maazimio mengine aliyataja kuwa ni pamoja na kuiomba serikali kuandaa sera na sheria shirikishi zitakazotoa kipaumbele cha kuwanufaisha vijana wa Zanzibar kisiasa, kiuchumi na kijamii.

Akizungumza katika kongamano hilo Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Mabodi alizishauri taasisi za vijana zilizobuni kongamano hilo kuendeleza utamaduni huo wa kukutana mara kwa mara kujadili masuala muhimu yanayogusa maendeleo ya nchini na ustawi wa tasisi zao.

Alisema CCM Zanzibar  inaunga mkono harakati za vijana wa makundi yote hasa wale wanaoanzisha vuguvugu la kujadili masuala mbali mbali ya kuimarisha maendeleo, amani,utulivu na umoja wa kijamii kwa maslahi ya nchini.

“Hatuwezi kuizungumzia historia ya Zanzibar bila kutaja vijana kwani waasisi wa ASP walianzisha harakati za kuikomboa Zanzibar kutoka katika utawala wa kibabe, viongozi hao walikuwa ni vijana.”, alieleza Dk.Mabodi.

Wakichangia maazimio hayo washiriki mbali mbali kutoka taasisi za Serikali, Vyuo vya elimu ya juu na taasisi za kisiasa wamesema pamoja na mikakati mizuri ya serikali ya kuwajengea mazingira mazuri vijana bado kundi hilo linatakiwa kujitathimini na kurudi katika misingi ya uzalendo.

Walisema endapo vijana hawatokuwa na misingi imara ya kuishi katika misingi ya uzalendo juu ya nchi yao, kuna hatari ya Zanzibar huko miaka ijayo kushindwa kufikia malengo yake ya kuwa nchi yenye nguvu kiuchumi na kimaendeleo kwani vijana wengi watatumia elimu zao kuhujumu maendeleo badala ya kuyalinda na kuyaendeleza kwa maslahi ya wote.

 Akifunga Mkutano huo Mkuu wa Mkoa Mjini Magharibi, Mhe. Ayoub Mohamed Mahmoud amewataka vijana kujiamini na kupanga mikakati madhubuti ya kuimarisha taasisi zao ili ziwe chachu ya kutatua changamoto zilizowazunguka.

Mhe. Ayoub amezipongeza taasisi hizo za vijana kwa kuandaa kongamano lenye tija lililoweza kujadili mambo mengi yanayohusu taifa kwa muda mfupi na kupata maazimio madhubuti yanayolenga kumaliza changamoto zinazowakabili katika kazi zao za kila siku.

Pamoja na hayo Mkuu wa Mkoa huyo, Mhe. Ayoub alitoa rai kwa vijana kuacha tabia za kulalamika na badala yake wafuatilie kwa karibu mambo mbali mbali yanayowahusu katika sehemu husika  ili yapatiwe ufumbuzi wa kudumu.


Kongamano hilo lililoendeshwa na taasisi mbali mbali zikiwemo Wizara ya Vijana,utamaduni,sanaa na michezo Zanzibar, Baraza la vijana Zanzibar pamoja na UVCCM Zanzibar.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni