Jumamosi, 25 Agosti 2018

KHEIR JAMES: ATAKA ELIMU ZA VIJANA ZISAIDIE JAMII ILIYOWAZUNGUKA.


 MWENYEKITI wa UVCCM Taifa Kheir James akiwahubia wanafunzi wa kidato cha sita Zanzibar wa mwaka 2018 waliofaulu kwa kiwango daraja la kwanza, pili na tatu katika hafla ya kuwapongeza iliyoandaliwa na CCM Zanzibar ambayo imefanyika hoteli ya Z-ocean iliyopo Bububu Mkoa wa Mjini  Magharibi Unguja.

 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar ambaye pia ni mlezi wa UVCCM Dk.Abdulla Juma Saadalla Mabodi akizungumza katika hafla hiyo ya kuwapongeza wanafunzi wa kidatu cha sita mwaka 2018 Zanzibar.

 MAKAMU Mwenyekiti wa UVCCM Taifa Tabia Maulid Mwita akizungumza na wanafunzi hao kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi ambaye ni Mwenyekiti wa UVCCM Taifa Kheir James katika hafla ya kuwapongeza wanafunzi wa kidato cha sita waliofaulu.

 NAIBU Katibu Mkuu wa UVCCM Zanzibar Shaka Hamdu Shaka akizungumza katika hafla ya kuwapongeza wanafunzi wa kidato cha sita Zanzibar waliofaulu masomo yao kwa kliwango cha daraja la kwanza, pili na tatu mwaka 2018, iliandaliwa na CCM.

 
BAADHI ya wanafunzi wa kidato cha sita mwaka 2018 waliofaulu wakifuatilia na kusikiliza nasaha mbali mbali kutoka kwa viongozi wa Chama Cha Mapinduzi na Serikali walioudhuria katika hafla hiyo.


NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.

MWENYEKITI wa Umoja wa vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Taifa Kheir James amewataka vijana wasomi nchini kuhakikisha tija ya elimu waliyonayo inanufaisha jamii iliyowazunguka kwa maslahi ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Rai hiyo ameitoa leo katika hafla ya kuwapongeza wanafunzi waliofaulu mtihani wa kidatu cha Sita Zanzibar mwaka 2018 kwa kiwango cha daraja la kwanza, la pili na tatu  (Division I,II na III) hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Z-Ocean iliyopo Bububu Wilaya ya Magharibi ‘’A’’  Zanzibar.

Ameeleza kuwa endapo vijana hao watashindwa kuzitumia vizuri elimu zao kwa kuzinufaisha jamii zilizowazunguka basi elimu hizo zitakuwa hazina maana kwao wao na taifa kwa ujumla.

Amesema serikali zote mbili ambazo ni Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zinaendelea kuthamini vijana kwa kuwawezesha kupitia nyanja mbali mbali hasa za kitaaluma.

Amewataka vijana hao ambao watajiunga na elimu ya juu katika vyuo mbali mbali nchini kuwa wanatakiwa kusoma masomo ambayo wana uwezo nayo ili waweze kufaulu vizuri katika masomo ya elimu ya juu na wawe wataalamu wenye uwezo wa kuleta mabadiliko chanya katika jamii.

Mwenyekiti huyo Kheir amefafanua kwamba CCM na serikali zake mbili inawaamini vijana kwa kuwapatia nafasi mbali mbali za uongozi sio kwa sababu za kujuana bali ni kutokana na sifa walizokuwa nazo kitaaluma.

“ CCM haina vijana wa ovyo ovyo kama zilivyo taasisi zingine za kisiasa bali ina vijana madhubuti, wazalendo,weledi na wenye sifa na kila vigezo vinavyokubalika katika nyanja mbali mbali za uongozi na utendaji katika taasisi za serikali na binafsi.”amefafanua  Mwenyekiti huyo.

Alisema taasisi yoyote isiyokuwa na utaratibu wa kurithisha uongozi kutoka kizazi kimoja kwenda kingine basi taasisi hiyo itakuwa ni sawa na mfu na ndio maana CCM inaendeleza utaratibu wa kuwarithisha na kuwaanda vijana wake kiungozi ili waweze kuwa viongozi bora ndani na nje ya Serikali zao.

Ameeleza kuwa suala la vijana kupendana ni lazima na sio hiari kwani endapo kundi hilo litaendekeza tabia ya kufanyiana fitna, majungu na kuchafuana hawatokuwa na uwezo wa kulinda rasilimali za taifa kwani nguvu nyingi watakuwa wanazitumia kuchafuana badala ya kufanya mambo ya maendeleo.

Pia amewataka viongozi wa serikali kuendeleza utamaduni wa kusema na kutangaza mambo mema yanayofanywa na serikali kwa wananchi pamoja na kutoa ufafanuzi wa masuala mbali mbali yanayopotoshwa na baadhi ya watu wasioitakia mema CCM na serikali zake.

Pamoja na hayo aliwambia viongozi vijana walioaminiwa na kupewa nafasi za uongozi ndani ya Chama na Serikali wafanye kazi zao kwa uadilifu ili vijana na wananchi kwa ujumla waendelee kuwaamini na kujifunza mambo mema kutoka kwao.

Mwenyekiti huyo amekemea vikali tabia za baadhi ya vijana wanaopenda kulalamika bila ya kujituma kufanya kazi kwa kubuni mambo mbali mbali ya kuwaingizia kipato pamoja na kulitumikia taifa kwa maendeleo endelevu.

Kupitia hafla hiyo ameipongeza CCM Zanzibar kwa juhudi zake  za kuendeleza utamaduni wa kuwaamini vijana wasomi kwa kuwapatia fursa mbali mbali zinazowasaidia kupata elimu ya juu na mafunzo ya ujasiriamali bila ya usumbufu.


Aidha Kheir amempongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein kwa kuipa kipaumbele sekta ya elimu pamoja na kuimarisha Amani na Utulivu wa Zanzibar hatua ambayo imechangia kuharakisha maendeleo ya nchi.

Naye Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Saadalla (Mabodi) amesema Chama Cha Mapinduzi kinaendelea kulea kitaaluma vijana wa makundi yote ili waweze kunufaika na rasilimali za nchi.

Amesema CCM Zanzibar inatekeleza mipango mbali mbali ya kuwawezesha vijana kwa kuwajengea mazingira bora yatakayowawezesha kujiajiri wenyewe na kuwasaidia vijana wenzao ambao bado hawajafika ngazi ya elimu ya juu.

 Pia ameeleza kwamba taasisi hiyo pia inaendelea na mikakati ya kuanzisha miradi mikubwa ya ujasiriamali itakayowezesha vijana ambao hawakufika elimu ya juu kuweza kujiajiri wenyewe.

“Chama chetu kinajali vijana wa makundi yote na sio wasomi pekee na ndio maana mipango yetu ya kuwajengea uwezo ipo kwa vijana wa makundi yetu na ndio maana hata nchi yetu imekombolewa na vijana waliokuwa wakwezi na wakulima.”, amesema Dk.Mabodi.

Mapema Makamu Mwenyekiti wa UVCCM Taifa, Tabia Maulid Mwita amesema vijana hao wapo tayari kutumia uwezo wao wote kulinda na kuthamini mambo mema yanayotekelezwa na Serikali zote mbili chini ya usimamizi wa Chama Cha Mapinduzi.

Hafla  hiyo imeandaliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar  kwa kushirikiana na UVCCM  kwa lengo la kuwapongeza vijana 470 wa kidato cha sita Zanzibar waliofaulu kwa kiwango cha daraja la kwanza, pili na tatu (Division I,I na III) mwaka 2018.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni