Jumamosi, 4 Agosti 2018

DK.MABODI " WANASIASA WALIOFILISIKA KISIASA NA KIFIKRA WAPUUZWE "



 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Saadalla ''Mabodi'' akifungua mfereji wa maji safi na salama mara baada ya uzinduzi wake uko shehia ya Magogoni Zanzibar.

 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Saadalla akimtwisha ndoo ya maji mwananchi wa shehia ya Magogoni kuashiria uzinduzi rasmi wa Kisima cha maji kilichozinduliwa ambacho kimejengwa na shirika la Direct AID kutoka nchini Kuwait.


NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Saadalla’’Mabodi’’ akiwahutubia wananchi wa Wadi ya Ijitimai shehia ya Magogoni katika hafla ya uzinduzi wa kisima cha maji safi na salama kitachowahudumia zaidi ya wananchi 2000.



MKURUGENZI  wa shirika la Direct AID la nchini Kuwait, Ayman Mohamed akizungumza katika hafla hiyo ambao ni wadau wa maendeleo walioshirikiana na SMZ kuchimba kisima hicho.


 DIWANI wa wadi ya Ijitimai, Asha Hassan Juma akizungumza katika hafla hiyo.

 BAADHI ya viongozi na wananchi walioudhuria hafla hiyo ya uzinduzi wa kisima.


NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar kimewataka wananchi  kisiwani humo kupuuza hoja dhaifu zinazotolewa na baadhi ya wanasiasa waliofilisika kisiasa na kifikra ambao wanajali maslahi yao binafsi kuliko maendeleo ya wananchi.

Akizungumza Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Saadalla ‘’Mabodi’’ katika hafla ya uzinduzi wa kisima cha Maji safi na salama huko shehia ya Magogoni Wadi ya Ijitimai, amesema wanasiasa wa aina hiyo hawafai kuaminiwa wala kupewa dhamana ya uongozi katika jamii.

Dk. Mabodi alisema suala la kuimarisha miundombinu ya maji safi na salama limo katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020, na linatekelezwa kwa kasi kubwa katika maeneo mbali mbali nchini.

Pia  amefafanua kwamba huo ndio ungwana wa CCM kwani inaahidi na inatekeleza kwa vitendo sio maneno matupu kama wanavyofanya baadhi ya wanasiasa wa vyama vya upinzani wanaobeza kila maendeleo yanayoletwa Chama Cha Mapinduzi kupitia serikali.

Amewambia  wananchi hao kuwa CCM kwa sasa inashughulika zaidi kutatua kero za wananchi, na sio kuangaika na wanasiasa walioshindwa kujenga hoja zao sehemu husika na badala yake wanatafuta makubaliano sehemu zisizostahiki.

“Kuna watu mpaka sasa wanaota ndoto za mchana kwa kusema kuwa eti 2020 hakuna uchaguzi sasa nawambia kama 2016 walitia mpira kwapani wakakimbia na uchaguzi ukafanyika na huo pia wa 2020 utafanyika na hakuna wa kuzuia.

CCM tunawambia tutaendelea kuwaletea wananchi maendeleo na kulinda amani na utulivu wa Zanzibar kwa gharama yoyote na anayetaka kuhatarisha amani basi ajaribu na aone .”, amesisitiza Dk. Mabodi.

Naibu Katibu Mkuu huyo Dk.Mabodi aliwasihi wananchi kuendelea kuiunga mkono CCM kwani hakuna mtu yeyote wa kuzuia Serikali chini ya Chama Chama Mapinduzi isitekeleze wajibu wake wa kuleta maendeleo endelevu kwa wananchi wake.

Akizungumzia uzinduzi huo wa maji safi na salama, Dk. Mabodi aliwapongeza washirika wa maendeleo wa kampuni ya Direct AID kutoka nchini Kuwait kwa kuchimba kisima hicho kitakachotoa huduma ya maji kwa wananchi wa shehia ya magogoni na maeneo jirani.

Alieleza na kuongeza kuwa wadau wa maendeleo wanavutiwa kuwekeza katika miundombinu ambayo ni muhimu kwa maisha ya kila siku kwa wananchi kutokana na sera mazingira rafiki ya uwepo wa Amani na Utulivu wa kudumu unaoletwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Aliwataka wananchi wa Wadi ya Ijitimai na shehia zake kulinda na kukitunza kisima hicho kisiharibiwe na baadhi ya watu wanaohujumu maendeleo ya serikali kwa makusudi.

Dk.Mabodi aliahidi kuwa Ofisi Kuu ya CCM Zanzibar chini ya Makamu Mwenyekiti wa CCM Dk.Ali Mohamed Shein itachangia mipira ya kusambazia maji kutoka katika kisima hicho kwenda kwa wananchi.

Pamoja na hayo alisema serikali kupitia mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) inatekeleza mradi mkubwa wa maji safi na salama nchini ambao utakamilika kabla ya mwaka 2020 ili wananchi waendelee kupata huduma hiyo kwa uhakika. 

Dk.Mabodi amekemea tabia ya baadhi ya wananchi wanaochimba visima vya maji na kugawa maji hayo kwa misingi ya itikadi za kisiasa, jambo ambalo alidai kuwa sio utamaduni mzuri.

Alisema utekelezaji wa miradi mbali mbali inayofanywa na Serikali ya CCM ni moja ya malengo ya Mapinduzi ya mwaka 1964 yaliyokuwa na dhamira ya kuleta usawa, ustawi wa kijamii, maendeleo kwa wote na wananchi kujitawala kiuchumi na kijamii.

Kupitia  hafla hiyo pia Dk. Mabodi alitoa zawadi ya nguo mbali mbali kwa niaba ya shirika la Direct AID, zitakazowasaidia wananchi wa maeneo hayo.

Katika Risala ya wananchi wa shehia ya Magogoni, wameshukru wadau nwa maendeleo wa Direct AID kwa kushirikiana na serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuchimba kisima hicho kitakachopunguza  tatizo la ukosefu wa maji wananchi wa shehia hiyo na shehia jirani.

Kwa upande wake Diwani wa Wadi ya Ijitimai, Asha Hassan Juma alisema uchimbaji wa kisima hicho ni mwendelezo wa utekelezaji wa miradi mbali mbali ya kijamii inayotekelezwa katika wadi hiyo.

Naye Mkurugenzi wa shirika la Direct Aid kutoka nchini Kuwait, Ayman Mohamed alisema kisima hicho ni mwendelezo wa visima mbali mbali vilivyojengwa nchini kwa ajili ya kuondosha tatizo la maji kwa jamii.

Alisema kwamba shirika hilo litaendelea kushirikiana kwa karibu na serikali kutatua changamoto za kijamii zikiwemo kuchimba visima vya maji safi na salama ambavyo ni miongoni mwa sadaka ya kuendelea kwa wananchi wa makundi yote.

Kisima hicho kilichogharimu milioni 50 kinatarajia kuwahudumia wananchi zaidi ya 2000 wa maeneo mbali mbali ya wadi ya ijitimai na shehia zake.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni