Jumapili, 19 Agosti 2018

DK.BASHIRU ASEMA CCM INAZIDI KUIMARIKA

 


NA IS-HAKA, ZANZIBAR.

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Dk.Bashiru Ally amesema CCM inaendelea kuimarika na hakuna Chama chochote cha kisiasa nchini kinachoweza kushindana na taasisi hiyo katika uringo wa siasa za ushindani wa sera za maendeleo kwa wananchi.

Kauli hiyo aliitoa mara baada ya kuwasili kisiwani Pemba katika mwendelezo wa ziara yake ya kujitambulisha ambapo amezungumza na wanachama mbalimbali katika ukumbi wa Skuli ya Sekondari ya Fidel Castro Wilaya ya Chake Chake Mkoa wa Kaskazini Pemba.

Amesema kutokana na uimara huo hakuna chama kingine mbadala wa Chama Cha Mapinduzi kinachoweza kushuka kwa wananchi nyumba kwa nyumba na kutatua changamoto za wananchi.  

Dk.Bashiru amewahakikishia wanachama na viuongozi hao kuwa CCM bado ipo imara na itapata ushindi wa kihistoria mwaka 2020 kwa nchini nzima kuliko ushindi unaopatikana kwa sasa katika uchaguzi mdogo unaoendelea katika maeneo mbalimbali nchini.

Ameongeza kwamba sababu za Chama Cha Mapinduzi kushinda kwa kishindo kwa kila uchaguzi huku vyama vya upinzani vikisambaratika na kukosa muelekeo wa uhalali wa kuitumikia jamii.

Kupitia mkutano huo aliwambia wanachama wa vyama vya upinzania kisiwani Pemba kwamba huu ndio wakati wao wa kujitawala kifikra kwa kujiunga na CCM kwani Chama Cha CUF hakina tena mvuto kwa jamii kutokana na tabia ya unafiki na uongo unaofanywa na viongozi wakuu wa CUF.

 Dk.Bashiru kupitia mkutano huo alitangaza rasmi kuwa Chama Cha Mapinduzi kitaendelea kuvunja ngome zote za upinzani kabla ya mwaka 2020, ambapo mamlaka hayo yanatokana na usimamizi mzuri wa utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi wa CCM ya mwaka 2015/2020.

Kupitia mkutano huo pia Dk.Bashiru aliwapokea wanachama wapya 62 waliotoka chama cha CUF na kujiunga na CCM kisiwani Pemba.

Aliwapongeza wanachama wajumbe wote wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kwa kumuamini kasha kupendekeza ateuliwe kushika nafasi ya Katibu Mkuu wa CCM Tanzania, na akaahidi kuwa atatumia nafasi yake kuleta mageuzi makubwa ya kiutendaji ndani na nje ya Chama Cha Mapinduzi.

Akizungumza Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Saadalla (Mabodi), amesema kazi kubwa ya Chama cha mapinduzi kwa zama za sasa ni kutekeleza kwa vitendo dhana ya CCM mpya na Tanzania mpya kwa maendeleo ya jamii.

Amefafanua kuwa miradi mbali mbali ya maendeleo iliyotekelezwa kwa ufanisi kisiwani Pemba ikiwemo mfuko wa maendeleo wa TASAF na kuongeza bei ya zao la karafuu ni kutokana na utekelezaji mzuri wa sera za CCM.

Naye Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kusini Pemba Ndugu Yussuf Ali Juma amesema ndani ya Mkoa huo wanaendelea na mikakati ya kuhakikisha CCM inashinda kwa ngazi zote katika uchaguzi Mkuu ujao.

Katika ziara hiyo Dk. Bashiru alifuatana na viongozi mbali wa Chama na Jumuiya wakiwemo wajumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa, wajumbe wa halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Makamu Wenyeviti wa Jumuiya pamoja na viongozi mbali mbali wa Chama na Serikali Zanzibar.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni