Jumatano, 24 Juni 2020

HASNA ATTAI ACHUKUA FOMU YA URAIS ZANZIBAR

KADA wa CCM Hasna Attai Masoud aliyechukua fomu ya kuomba ridhaa ya kugombea Urais wa Zanzibar kupitia CCM akionyesha mkoba wenye fomu za kuwania Urais wa Zanzibar, mara baada ya kukabidhiwa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC,Idara ya Organazesheni CCM Zanzibar Cassian Gallos Nyimbo, hafla hiyo imefanyika Afisi Kuu ya CCM Kisiwsandui,Zanzibar.




MBIO za kusaka Urais wa Zanzibar zimeendelea leo Juni 24,2020 kada wa CCM Hasna Attai Masoud(40), amechukua fomu ya kuomba ridhaa ya kugombea Urais wa Zanzibar kupitia Chama Cha Mapinduzi.

Hasna, akiwa ni mwanamke wa pili kujitokeza katika kinyang’anyiro hicho amewasili katika Ofisi za Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui Zanzibar majira ya 4:00 asubuhi na kukabidhiwa fomu hiyo na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC,Idara ya Organazesheni CCM Zanzibar Cassian Gallos Nyimbo.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kukabidhiwa fomu hiyo, amempongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein kwa kuwaamini na kuwapatia fursa mbali mbali za uongozi na utendaji wanawake nchini.

Amesema Dk.Shein, amekuwa ni kiongozi wa kuigwa katika kuthamini kundi la wanawake ambao kwa miaka mingi walikuwa hawana uwakilishi mkubwa katika nafasi mbali mbali za uongozi kama ilivyo hivi sasa.

“ Serikali ya awamu ya saba chini ya uongozi wa Rais wetu mpendwa Dk.Shein imewaona wanawake na kuwapatia nafasi kubwa ya kuongoza katika vyombo vya kufanya maamuzi, hivyo nasi tumehamasika sana nasi kuingia katika ushindani wa kuwania nafasi mbali mbali za uongozi”, amesema.


Kada huyo ambaye ni msomi wa shahada ya pili ya masuala ya usimamizi wa biashara, anakuwa ni wa 25 kuchukua fomu hiyo ya kuomba ridhaa ya kugombea Urais wa Zanzibar kupitia CCM.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni