Jumanne, 23 Juni 2020

MWANAMICHEZO HASHIM SALUM ACHUKUA FOMU YA KUWANIA URAIS WA ZANZIBAR.





KADA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Hashim Salum Hashim leo amechukua fomu ya kuomba ridhaa ya kugombea Urais wa Zanzibar kupitia CCM.

Kada huyo amewasili katika Ofisi za Afisi Kuu ya Chama Cha Mapinduzi Kisiwandui Zanzibar majira ya saa 6:10 mchana na kupokelewa na maafisa wandamizi wanaoshughulikia mapokezi ya makada hao.

Hashim alikabidhiwa fomu hiyo na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC, Idara ya Organazesheni CCM Zanzibar Cassian Gallas Nyimbo, na kumtaka atafute wadhamini 250 wa Chama Cha Mapinduzi.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kukabidhiwa fomu hizo Hashim, amesema endapo atapewa ridhaa na Chama atahakikisha kipaumbele chake ni kuimarisha sekta ya michezo nchini.

Amesema yeye ni mwanamichezo na amehudumu katika sekta hiyo kwa muda mrefu hivyo atahakikisha serikali inatoa  udhamini wa ligi kuu ya soka Zanzibar  kwa asilimia 100.

Amefafanua kuwa ligi hiyo inaendeshwa bila udhamini kwa muda mrefu toka kampuni ya Grand Malta isitishe udhamini wake mwaka 2013.

Ameongeza kwamba mbali na michezo pia ataendeleza maendeleo yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 10 ya Serikali ya awamu ya saba chini ya uongozi wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein.

“Nampongeza Rais wetu Dk.Shein kwa kasi yake ya kuwaletea wananchi wa Zanzibar maendeleo endelevu hasa katika sekta za afya,elimu, miundombinu ya umeme na barabara, maji safi na salama pamoja na sekta mbali mbali za kiuchumi na kijamii”,amesema.

Pamoja na hayo kada huyo ambaye ni mtumishi wa SMZ katika Idara ya Mazingira amesema ataimarisha maendeleo katika Nyanja za kiuchumi na kijamii kwa manufaa ya wananchi wote.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni