Jumanne, 16 Aprili 2019

MKOA WA MAGHARIB CCM YAANZA ZIARA KATIKA MAJIMBO YA MKOA HUO.

KAMATI ya Siasa ya CCM Mkoa wa Magharibi Unguja wakikagua mradi wa maji katika jimbo la Chukwani Unguja katika ziara ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa na mifuko ya Jimbo ya Mwakilishi na Mbunge wa Jimbo hilo.

 VIONGOZI mbali mbali wa Kamati ya Siasa wakikagua na kupima afya katika  Kituo cha Afya cha Shehia ya Shakani ambacho kipo katika jimbo la Chukwani ambacho ni miongoni mwa Vituo vinavyosaidiwa vifaa mbali mbali kutoka mfuko wa maendeleo ya Jimbo hilo la Chukwani.


 KAMATI ya Siasa ya CCM Mkoa wa Magharib Unguja wakikagua miradi mbali mbali inayotekelezwa na mfuko wa maendeleo ya Jimbo la Chukwani katika Skuli ya Msingi na Sekondari ya Chukwani Unguja.



NA IS-HAKA OMAR,ZANZIBAR.

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Magharibi Unguja kimesema kigezo cha kuwapatia nafasi za uongozi kwa awamu nyingine kupitia uchaguzi ujao wa mwaka 2020 Wabunge, Wawakilishi na Madiwani ni utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM utakaokidhi mahitaji ya wananchi.

Msimamo huo umetolewa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa huo Mohamed Rajab Soud katika ziara ya kukagua na kutathimini utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika Jimbo la Chukwani Unguja.

Amesema viongozi wa Majimbo waliopewa dhamana ya kuongoza  majimbo kupitia ridhaa za wananchi ndani ya Mkoa huo wanatakiwa kufanya kazi kwa kasi ili  kukamilisha ahadi zao kwa sasa kabla ya 2020.

Ameeleza kwamba tiketi ya pekee ya kuwarejesha madarakani viongozi hao ni kuyatekeleza kwa ufanisi yale waliowaahidi wananchi  na atakayeshindwa kutekeleza masharti hayo asitarajie utetezi wa CCM.

Mohamed amesema lengo la ziara hiyo ni kutathimini,kuchambua na kujiridhisha juu ya ripoti za utekelezaji wa Ilani ya CCM zinazoandikwa na viongozi wa majimbo hasa thamani ya fedha zilizoainishwa matumizi yake kama zinalingana na miradi iliyotekelezwa.

Amesema ziara hiyo itafanyika katika majimbo yote 13 ya Mkoa huo kwa kukagua miradi mbali mbali ikiwemo ya maji, afya, elimu, kilimo, ufugaji, miundombinu ya barabara, umeme na vikundi mbali mbali vya ujasiriamali iliyotekelezwa na viongozi hao wa majimbo.

Akizungumzia jimbo la Chukwani Mwenyekiti huyo Mohamed, amesema licha ya viongozi wa jimbo hilo kutekeleza vizuri baadhi ya miradi bado kuna miradi muhimu ya kijamii haijatekelezwa vizuri hasa katika masuala ya vikundi vya ujasiriamali na  kilimo.

Pamoja na hayo alitaka baadhi ya miradi ya kijamii hasa ya maji safi na salama iwekewe mazingira rafiki ya kutumiwa na wananchi wengi kuliko kuwanufaisha watu wachache.

"Tumeanza ziara ya kukagua miradi ya maendeleo unayotekelezwa na wabunge, wawakilishi na madiwani kwa kila jimbo tutafika kila pembe kuona mambo yote aambayo viongoza wetu wanayaandika katika taarifa zao kuwa wametekeleza sasa tunataka tuyaone badala ya kuambiwa tu.

Kupitia ziara hii hatutowaonea wala kuwapendelea viongozi awa kila mtu tutampa maelekezo kwa mujibu alivyotekeleza Ilani ya CCM ya mwaka 2015/2020,kwani huu ndio muda mwafaka wa kumalizia kazi za kutekeleza ahadi za wananchi. "alieleza Mwenyekiti huyo na kuongeza kuwa CCM itaendelea kuwa karibu na wananchi kwa kutatua kwa kutatua kero zao kwa wakati.

Naye Mwakilishi wa Jimbo hilo Mhe. Mwanaasha Khamis Juma amesema ametekeleza miradi mbali mbali katika sekta za Elimu, Afya, Maji na miundombinu ya barabara ili kumaliza changamoto sugu zinazowakabili wananchi wa jimbo hilo.

Amesema katika mradi wa utengenezaji wa barabara ya kutoka shehia ya Kisauni,shakani,buyu hadi Chukwani yenye urefu wa kilomita 8.5 iliyojengwa kwa kiwango cha kifusi ametumia zaidi ya shilingi milioni 24 Mbunge shilingi milioni 10 na Madiwani shilingi milioni 10 na mililioni 68 zimetolewa na Manispaa ya Magharibi ‘B’ ambapo zimetumika jumla ya shilingi milioni 112 katika mradi huo.

Kupitia maelezo yake Mwakilishi huyo ameiomba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar  kuharakisha mipango yake ya kujenga barabara hiyo kwa awamu ya pili ya kiwango cha lami ili kuepusha hasara ya fedha ambazo kwa awamu ya mwanzo.

Mwanaasha ameahidi kuyafanyia kazi maagizo mbali mbali yaliyotolewa na CCM Mkoa wa Magharib ili kukamilisha baadhi ya ahadi alizozitoa katika kampeni za uchaguzi uliopita.

Katika ziara hiyo amefuatana na viongozi mbali mbali wa CCM na Jumuiya zake wanaounda kamati ya Siasa ya Mkoa huo wakiwemo Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa pamoja na Wajumbe wa Mabaraza mbali mbali ya Jumuiya kwa ngazi ya Mkoa na Taifa.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni