Jumatatu, 22 Aprili 2019

DK.MABODI-ASEMA CCM IMEJIZATITI KUTATUA CHANGAMOTO ZA WANANCHI NA KUSIMAMIA DEMOKRASIA.

 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Saadalla Mabodi akiwahutubia Wanachama wa CCM na Wananchi  katika ziara yake ya kukagua Utekelezaji wa Ilani katika Maskani ya CCM ya Kisonge, iliyopo Shehia ya Mzuri Jimbo la Makunduchi Wilaya ya Kusini Unguja.



NAIBU Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dk.Abdulla Juma Saadalla ‘Mabodi’ amesema Chama hicho kimejizatiti kutatua changamoto za Wananchi pamoja na kusimamia Demokrasia kwa kukemea vitendo viovu vinavyohatarisha Amani na Utulivu wa Nchi.

Kauli hiyo ameitoa katika ziara yake ya kukagua Uhai wa Chama na Utekelezaji wa Ilani ya CCM katika Jimbo la Makunduchi Wilaya ya Kusini Unguja, amesema vipaumbele vya CCM ni kutekeleza kwa kasi ahadi zilizotolewa na Taasisi hiyo kwa wananchi kupitia Uchaguzi Mkuu uliopita.

Amesema Chama Cha Mapinduzi kinaendelea kuaminiwa,kupendwa na kuthaminiwa na Mamilioni ya Watanzania kutokana na usimamizi mzuri wa utekelezaji wa Sera zake, kwa kutatua changamoto za kijamii kwa wakati mwafaka.

Aidha amesema katika kusimamia dhana ya Demokrasia CCM haitosita kukemea vitendo viovu vinavyoashiria kuvunja Sheria za Nchi, hasa vinavyotekelezwa na baadhi ya Vyama vya upinzani.

“Tumekubali kuingia katika mfumo wa Vyama vingi ili tushindane kwa Sera na sio kushindana kwa vituko na vurugu ni muhimu kila mwanasiasa kujitathimini juu ya mwenendo wake kwa jamii anayoiongoza.”, ameeleza Dk.Mabodi.

Amesema katika zama za CCM mpya imekuwa imekuwa ni kimbilio la wananchi wanaoamini katika siasa za maendeleo ambao wametelekezwa na Vyama vyao na kupokelewa  vizuri ndani ya CCM ili wanufaike na Demokrasia iliyotukuka.

Amewataka Viongozi na Watendaji wa CCM kutowawekea vikwazo Wananchi wanaotaka  kujiunga na Chama na badala yake wapewe fursa hiyo bila masharti magumu sambamba na kuwasomesha miongozo na itikadi za kitaasisi.

Amewaagiza Wabunge,Wawakilishi na Madiwani kufanya mikutano katika maeneo yao ya kuwaeleza Wananchi mafanikio yaliyofikiwa katika utekelezaji wa Ilani ili wananchi hao wawe Mabalozi wa kufikisha taarifa hizo kwa jamii.

Amewambia wananchi kuwa CCM imesimamia kwa ufanisi miradi ya maendeleo ukiwemo wa TASAF ambao upo katika Ilani ya CCM ya mwaka 2015/2020, ambao umewaondosha wananchi katika wimbi la umasikini na kuwa na kipato cha kati.  

Akizungumza wakati wa kukabidhi vifaa mbali mbali vikiwemo Runinga (Television) pamoja na Fedha kwa vikundi 11 vya Saccos ya Shehia ya Mzuri katika Maskani ya CCM ya Kisonge Makunduchi Dk.Mabodi amesisitiza kuwa uhai wa Taasisi hiyo ya kisiasa unaanza kuimarishwa kuanzia ngazi ya mashina.

Naye Mwakilishi wa Jimbo la Makunduchi Mhe.Haroun Ali Suleiman amesema tayari Ilani ya CCM ndani ya Jimbo hilo imetekelezwa kwa asilimia 90, na kwa sasa wanaendelea kutatua baadhi ya changamoto ili kuzimaliza kabla ya 2020.

Mhe.Haroun amesema kwa kushirikiana na Kamati ya Siasa ya Jimbo hilo wamefanya ziara katika Shehia 13 za Jimbo kwa kuratibu changamoto zinazowakabili wananchi na nyingi zimetatuliwa sambamba na kueleza fursa na miradi ya maendeleo iliyotekelezwa na Serikali.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo hilo Mhe. Ameir Haji Timbe ameeleza kuwa maendeleo yaliyopatikana katika Jimbo hilo yametokana na ushirikiano mkubwa uliopo baina ya viongozi na wananchi.

Akizungumza Mwenyekiti wa Maskani ya CCM ya Kisonge iliyopo Makunduchi Abdallah Hassan Haji amesema wanaendelea kuvuna wanachama wapya kutoka vyama vya upinzani huku wakijipanga kufuta masalia ya upinzania ndani ya Jimbo hilo.

Naye Mwenyekiti wa Maskani ya CCM ya Hapa Kazi Tu Yussuf Abeid Haji, akizungumza katika uzinduzi wa Maskani hiyo amefafanua kuwa eneo la maskani yao litatumika kuwa chachu ya kujenga umoja,mshikamano pamoja na kuwa kituo mbadala cha kubuni miradi mbali mbali ya maendeleo kwa maslahi ya Wana CCM.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni