Jumanne, 2 Oktoba 2018

CCM MKOA WA MAGHARIB YAFANYA ZIARA KATIKA SHAMBA LENYE MGOGORO.

 Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Magharibi Ndugu Mohamed Rajab Soud akizungumza na Wananchi wanaofanya shughuli za kilimo katika shamba lililopo Dole kwa Shabuta waliomwita kwa ajili ya kuwasilisha malalamiko yao ya kufukuzwa katika shamba hilo.

 MWAKILISHI wa Jimbo la Bububu Ndugu Masoud Abrahman Masoud akizungumza mbele ya wananchi hao.

 BAADHI ya wananchi hao wakimsikiliza kwa makini Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Magharibi Ndugu Mohamed Rajab Soud.

Shamba la Dole kwa Shabuta lenye ukubwa wa hekta 168 ambalo lina mgogoro kati ya wananchi na bi.Shafika Hamed Abdulla.



MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Magharibi Ndugu Mohamed Rajab Soud  amewataka wananchi wanaofanya shughuli za kilimo katika shamba lililopo Dole kwa Shabuta kuendelea kuwa wavumilivu wakisubiri maamuzi ya Vyombo vya kisheria kutatua mgogoro wa shamba hilo.

Rai hiyo ameitoa leo wakati alipotembelea shamba hilo lililopo Dole kwa Marehemu Mzee Shabuta lenye hekta zaidi ya 168 ambalo lina mgogoro baina ya wananchi wanaotumia eneo hilo kwa ajili ya shughuli za kilimo na Bi. Shafika Hamed Abdallah anayedaiwa kuwa mmiliki wa eneo hilo.

Alisema mgogoro huo tayari upo katika ngazi ya Mahakama ni vyema wananchi hao wakaendelea kutulia huku wakifanya shughuli zao za kujitafutia kipato mpaka mahakama itakapofanya maamuzi ya kisheria juu ya shauri hilo.

 Mwenyekiti huyo ndugu Rajab aliyefuatana na Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Magharib kwa lengo la kusikiliza malalamiko ya wananchi hao, na kusema kuwa CCM itafuatilia kwa kina ili  kutatua mgogoro huo kwa njia ya amani bila kutokea athari yoyote ya uvunjifu wa Sheria.

Alisema baada ya ziara hiyo atakaa na Kamati ya Siasa ya Mkoa huo pamoja na viongozi mbali mbali wa serikali kwa lengo la kujadiliana na kufikia maamuzi yatakayosaidia kusuluhisha mgogoro huo.

“Tumekutana na nyinyi wananchi na kusikia malalamiko yenu na tunaahidi kuyafanyika kazi lakini kwa kuwa jambo hili tayari lipo katika ngazi ya mahakama tutafuatilia kujua wapi limekwama ili tukwamue”.amesema Mwenyekiti huyo wa CCM.

Akizungumza Mwakilishi wa Jimbo la Bububu Masoud Abrahman Masoud, amesema ziara hiyo imefanyika baada ya wananchi hao kumuomba wakutane na uongozi wa CCM ngazi ya Mkoa ili wawasilishe malalamiko yao ya kuzuiliwa kufanya shughuli za kilimo katika shamba hilo wanalolitumia kwa miaka mingi kwa ajili ya kilimo.

Mwakilishi huyo Masoud, ameongeza kuwa kutokana na mgogoro huo kuwa wa muda mrefu huku pakizuka vurugu za mara kwa mara kuna umuhimu wa Serikali hasa taasisi zinazohusika na utatuzi wa migogoro ya ardhi kutafuta ufumbuzi wa haraka juu ya tatizo hilo.

Shamba hilo lenye ukubwa wa jumla ya hekta 168 linatumiwa kwa shughuli za kilimo na zaidi ya wananchi 200 wa vijiji mbali mbali vya Jimbo la Bububu  hasa kijiji cha Dole na vjijiji vya majimbo jirani.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni