Jumamosi, 27 Oktoba 2018

RAMADHAN CHANDE - AIBUKA MSHINDI UCHAGUZI WA JANG'OMBE KWA ASILIMIA 90.5

MSHINDI wa Uwakilishi tiketi ya CCM Uchaguzi Mdogo wa Jang'ombe Ndugu Ramadhan Hamza Chande. 


MGOMBEA Uwakilishi katika Uchaguzi Mdogo wa Jimbo la Jang'ombe Zanzibar  kupitia Chama cha Mapinduzi Ndg Ramadhan Hamza Chande  ameibuka mshinda katika uchaguzi huo kwa ushindi wa Kura 6,581 sawa na asilimia 90.5 ya kura zote halali zilizopigwa ambazo ni 7,274.

Akitangaza matokeo hayo  Msimamizi Mkuu wa Uchaguzi Jimbo hilo ambaye pia ni Afisa wa Tume ya Uchaguzi Wilaya ya Mjini Unguja, Mwanapili Khamis Mohamed amesema kufuatia matokeo hayo Ramadhan Hamza ameshinda Ujumbe wa Baraza la Wawakilishi wa Jimbo la Jang'ombe.

Afisa huyo amemtangaza mshindi wa pili kuwa ni Mgombea wa Chama Cha CUF ndugu Mtumwa Ambari Abdalla aliyepata kura 172 sawa na asilimia 2.4.

Aidha ametaja kura za vyama vingine vilivyoshiriki katika mchakato huo wa Uchaguzi ambazo ni ADA-TADEA 131, AFP 58, CCK 72, DP 73, TLP 71, SAU 53 pamoja na NRA 62.
Akizungumza mara baada ya matokeo hayo Mwakilishi wa Mgombea wa chama cha ADA-TADEA Halma Abdalla amesema Uchaguzi huo ulikuwa huru na wa haki hivyo mgombea wa CCM ameshinda kihalali.

Naye Mshindi wa Kiti cha Uwakilishi tiketi ya CCM Jimbo la Jang'ombe ndugu Ramadhan Hamza Chande amewashukuru wananchi wote waliojitokeza kupiga kura hasa wale waliomwamini na kumpa ridhaa ya kuwa Mwakilishi wa kuliongoza Jimbo hilo.

Ameahidi kutekeleza vipaumbele vyake alivyoahidi kupitia katika mikutano mbali mbali ya kampeni za Uchaguzi kwa mujibu wa maelekezo yaliyomo katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020.

Uchaguzi huo uliofanyika leo Octoba 27, mwaka 2018 umefanyika kutokana na aliyekuwa Mwakilishi wa Jimbo hilo ndugu Abdalla Diwani kuvuliwa uanachama kwa makosa ya ukiukaji wa maadili ndani ya taasisi hiyo.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni