Jumamosi, 27 Oktoba 2018

MWANAPILI-ASEMA ZOEZI LA KUPIGA KURA LINAENDELEA VIZURI JANG'OMBE.

 MGOMBEA wa nafasi ya Uwakilishi tiketi ya CCM Jimbo la Jang'ombe Ramadhan Hamza Chande akipiga kura katika Kituo cha Kupigia kura kilichopo Shule ya Jang'ombe Jimbo la Jang'ombe Wilaya ya Mjini Zanzibar.


 BAADHI ya Wananchi wakiangalia majina yao kwa ajili ya kupiga kura katika Kituo cha kupiga kura kilichopo Kidongochekundu zanzibar katika zoezi la uchaguzi jimbo la Jang'ombe linaloendelea katika maeneo mbali mbali ya Jimbo hilo.


NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.

ZOEZI la Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Jang’ombe wa kumchagua Mwakilishi wa Jimbo hilo unaendelea vizuri bila ya kuwepo na matukio ya vurugu na uvunjifu wa amani katika vituo vya kupigia kura.

 Akizungumza Msimamizi Mkuu wa Uchaguzi Jimbo hilo ambaye pia ni Afisa wa Tume ya Uchaguzi Wilaya ya Mjini Unguja, Mwanapili Khamis Mohamed, amedhibitisha kuwa zoezi hilo linaendelea vizuri.  

Amesema wananchi wamejitokeza toka saa 1:30 asubuhi walikuwa tayari washafika katika vituo vya kupiga kura na vituo vilipofunguliwa wamepiga kura kwa utulivu na bado wanaendelea kujitokeza.

Afisa huyo wa Tume ya Uchaguzi Wilaya ya Mjini, amewasihi wananchi wenye sifa za kupiga kura kisheria kuendelea kujitokeza kwa wingi kwa lengo la kutekeleza haki yao ya Kidemokrasia.

Aidha amesema mpaka hivi sasa bado hapajatokea changamoto yoyote kwani Tume hiyo imejipanga vizuri hasa katika suala zima la kuweka mazingira rafiki ya upatikanaji wa  vifaa pamoja na huduma za msingi za maafisa na wadau mbali mbali walioshiriki katika kufanikisha zoezi hilo.

Akizungumza wakati wa kutembelea Vituo  vya kupigia kura  Mgombea Uwakilishi wa Tiketi ya CCM wa Jimbo la Jang’ombe Ndugu Ramadhan Hamza Chande, ameelezea kuridhishwa kwake na hali ya utulivu katika Vituo vya kupigia kura.

Amewasisitiza wananchi wa Jimbo hilo bila ya kujali tofauti zao za kisiasa wajitokeze  kwa wingi kuchagua mgombea watakayeona ana sifa na vigezo vya kuwaletea maendeleo.

Kwa upande wake mgombea wa nafasi ya Uwakilishi wa Chama cha ADA-TADEA, Sabry Ramadhan Mzee ‘China’ , amewataka wananchi wa Jimbo la Jang’ombe kuendeleza utamaduni wa ustaarabu na utulivu wakati wote wa zoezi hilo la Uchaguzi.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi RC-Ayoub Mohamed Mahmoud, amesema Vyombo vya Ulinzi vimejipanga vizuri kukabiliana na changamoto yoyote inayohusu masuala ya ulinzi na usalama ndani ya Jimbo hilo.

Amewasihi wananchi wakimaliza kupiga kura warudi majumbani kwa lengo la kuendendelea na shughuli zao za kujitafutia kipato huku wakisikiliza vyombo vya habari kwa ajili ya kupata matokeo ya Uchaguzi huo.

Uchaguzi huo unaofanyika leo Octoba 27, mwaka 2018 unafanyika kwa lengo la kumpata Mgombea Uwakilishi wa Jimbo la Jang’ombe kufuatilia aliyekuwa kiongozi wa nafasi hiyo kuvuliwa uanachama na CCM kutokana na kukiuka maadili ya taasisi hiyo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni