Jumapili, 21 Oktoba 2018

MTATIRO - ASEMA SERA NZURI ZA CCM NDIO CHIMBUKO LA MAENDELEO YA TANZANIA

 KADA wa CCM Julius Mtatiro akizungumza na Vyombo vya Habari vya Zanzibar kwa mara ya kwanza toka alipohama katika Chama cha CUF.

 BAADHI ya Waandishi wa Habari wakimsikiliza Kada wa CCM Julius Mtatiro katika Mkutano uliofanyika katika Ofisi Kuu ya CCM Kisiwandui Zanzibar.


KADA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Julius Mtatiro amesema viongozi mbali mbali wanahama katika  Vyama vya upinzani kutokana na taasisi hizo kushindwa kuwatumikia wananchi na badala yake ajenda zao zinatekelezwa na CCM.

Amesema mifumo imara ya kisiasa, kidemokrasia,uwazi, uwajibikaji, utendaji  na utawala bora iliyopo ndani ya CCM na Serikali zake mbili ya Zanzibar na  Jamhuri ya muungano ndio chanzo cha wanachama na viongozi kujiunga na Chama Cha Mapinduzi.

Kauli hiyo ameitoa leo wakati akizungumza na waandishi wa Habari huko Afisi Kuu ya CCM Zanzibar Kisiwandui, aliwambia wanachama mbali mbali wa vyama vya upinzani hasa CUF na CHADEMA kujiunga na CCM mapema ili wanufaike na demokrasia pamoja na siasa zenye sera halisi za maendeleo.

Kupitia mkutano huo, Mtatiro aliyewahi kushika nyadhifa za ngazi za juu ndani ya CUF na kwa sasa amehamia CCM, alisema amepoteza  miaka 10 akiwa kiongozi ndani ya CUF na UKAWA ambapo hana jambo lolote analoweza kujivunia zaidi ya kuwa muhanga  wa kutatua migogoro ndani ya taasisi hizo iliyotokana na uchu wa madaraka.

Ameeleza kwamba licha ya vyama vya upinzani kuwa mstari wa mbele kukosoa na kubeza kila jambo linalofanywa na Serikali lakini ukweli na kwamba ndani ya vyama hivyo kuna mifumo ya rushwa, ufisadi, ukandamizaji wa demokrasia, pamoja na ukiukaji wa haki za binadamu.

Akijibu baadhi ya hoja za waandishi wa habari , Mtatiro amesema kila mtu ana haki ya kuhama chama kimoja kwenda kingine na yeye amefanya hivyo baada ya kuvutiwa na mfumo imara wa kisiasa  ndani ya CCM chini ya Mwenyekiti wa Chama hicho Dkt. John Pombe Magufuli.

“ Kama niliweza kukaa ndani ya CUF miaka 10, basi hata CCM Mwenyezi Mungu akinipa uzima nitakaa zaidi ya miaka 60 kwani Chama hiki kimetekeleza mambo mengi mazuri kwa muda mfupi ambayo nilitamani yafanyike kwa Taifa letu”, alisema Mtatiro.

Amesema kuwa atabaki kuwa mwanasiasa mwenye msimamo na asiyeyumba katika kueleza ukweli na kuonyesha njia ya mafanikio kwa wananchi wenzake.

Akizungumzia hali ya maisha ya wananchi hasa wa Vijijini amesema yameimarika kwani huduma muhimu za kijamii na kiuchumi zimeboreshwa hasa Barabara Afya , Elimu , Umeme, Maji safi na salama.

Pia akizungumzia Sera ya Tanzania ya Viwanda Mtatiro, amesema mkakati huo ndio chimbuko la kukuza kwa kasi uchumi wa Taifa na kuongeza kuwa sera hiyo inatakiwa kwenda sambamba na kampeni uzalishaji mkubwa wa malighafi kupitia Sekta ya Kilimo.

Amesema Mataifa yaliyoendelea yamewekeza zaidi katika ujuzi na ufundi hasa kwa kundi la vijana ambalo ndio nguvu kazi ya uzalishaji katika Sekta mbali mbali za umma na binafsi.

Katika maelezo yake mtatiro, ameshauri CCM kupitia Serikali zake kuaulisha changamoto za ajira kwa vijana kupitia mfumo wa kujenga Vyuo vingi vya Ufundi na Ujasiriamali ili kuzalisha wataalamu wenye ujuzi wa kutengeneza bidhaa mbali mbali zitakazochangia kwa kiwango kikubwa katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

“ Nazishauri Serikali zetu badala  ya kutumia fedha nyingi kuwasomesha vijana Vyuo Vikuu pia waangazie katika ujenzi wa Vyuo vya Ufundi na Ujasiriamali kila Kata na Shehia ili tupate vijana wengi wenye ujuzi ambao wataweza pia kujiajiri wenyewe kwani mataifa mengi yaliyoendelea kiuchumi kama China,Marekani  na India wametumia mfumo huo na wameweza kufika mbali kiuchumi.”, ameshaSEuri Mtatiro.

Mwanasiasa huyo ambaye pia ni mchambuzi, mtafiti na mwandishi wa makala mbali mbali za Kisiasa nchini amezungumza na Vyombo vya Habari  vya Zanzibar kwa mara ya kwanza toka alipohama CUF na kujiunga na CCM mnamo  Desema 11, mwaka 2018.


Maoni 1 :