Ijumaa, 30 Juni 2017

WABUNGE NA WAWAKILISHI PEMBA WATAKIWA KUWEKEZA KATIKA ELIMU





Chama cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar kimewataka Wabunge na Wawakilishi kisiwani Pemba kuwekeza katika sekta ya elimu ili kuwasaidia vijana wanaosoma kwenye shule na vyuo vya elimu ya juu vilivyopo katika kisiwa hicho.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Dkt. Abdulla Juma Saadalla “Mabodi” katika mwendelezo wa ziara yake Pemba wakati akikagua ujenzi wa shule ya Msingi na Sekondari ya Kwale Mkoa wa Kusini Pemba.

Amesema viongozi hao wanatakiwa kubuni miradi itakayosaidia kuinua viwango vya elimu kwa vijana mbali mbali waliopo katika majimbo hayo ili waweze kupata taaluma zinakazowasaidia kujiajiri wenyewe.

Ameeleza kuwa  endapo kila jimbo litakuwa na wataalamu mbali mbali waliosomeshwa na viongozi wa majimbo hatua hiyo itaongeza kasi ya maendeleo kwa kupata wataalamu wa fani mbali mbali watakaohudumu kwenye sekta za umma na binafsi katika majimbo hayo.

Sambamba na hayo aliwaagiza Wabunge na wawakilishi hao kuongeza kasi katika kutatua kero zinazowakabili wananchi  ili kwenda sambamba na matakwa ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. 

Dkt.Mabodi alisema viongozi hao wanatakiwa kuwa wa kwanza kuratibu changamoto zinazowakabili wananchi kwa lengo la kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu kama walivyowaahidi wananchi hao katika kampeni za uchaguzi mkuu uliopita.

Pamoja na hayo amewapongeza wananchi wa shehia ya Kwale Kisiwani Pemba kwa uzalendo wao wa kushiriki katika shughuli za kijamii zikiwemo ujenzi wa Skuli ya Kwale ambayo kwa sasa wanasoma watoto wa shehia hiyo na vitongoji vyake.

Kupitia ziara hiyo Dkt. Mabodi amechangia shilingi milioni tatu kwa lengo la kusaidia ujenzi wa madarasa ya shule ya Kwale.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni