Jumapili, 11 Juni 2017

UWT ZANZIBAR YAPIGA MSASA VIONGOZI WAPYA WA MATAWI YA MAJIMBO YA MKWAJUNI NA CHAANI UNGUJA


 Naibu Katibu Mkuu wa UWT Zanzibar, Bi.Salama Aboud Talib akiwahutubia viongozi wapya wa Matawi ya Majimbo ya Chaani na Mkwajuni Kaskazini “A” kichama Unguja.
 Katibu wa Idara ya Organazesheni wa UWT Zanzibar, Tunu Juma Kondo akizungumza na viongozi hao kabla ya kumkaribisha Katibu Mkuu wa UWT Zanzibar, Bi.Salama Aboud Talib huko  Gamba Ofisi ya Wilaya Kaskazini “A” Gamba Unguja.
Mmoja wa Viongozi wa Tawi la Chaani Mcheza Shauri Jimbo la Chaani Bi. Fatma akitoa akizungumza katika Mkutano huo. 
Naibu Katibu Mkuu huyo Bi. Salama Aboud akitoa sadaka ya fedha kwa Akina Mama wa UWT kwa ajili ya futari  ya Mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Mwakilishi wa Viti Maalum Mkoa wa Kaskazini Unguja 
 Bi. Mtumwa Suleiman akimuunga  mkono  Naibu Katibu Mkuu wa UWT Z'bar Bi. Salama kwa kuongeza sadaka ya fedha kwa Akina Mama wa UWT kwa ajili ya futari  ya Mwezi mtukufu wa ramadhani.
Baadhi ya viongozi mbali mbali UWT wa ngazi za matawi wa Majimbo ya Chaani na Mkwajuni  Wilaya ya Kaskazini “A” wakifuatilia kwa makini nasaha zinazotolewa na viongozi wakuu wa UWT katika Mkutano huo.



      UMOJA wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi Tanzania (UWT), umewataka viongozi waliochaguliwa kwa ngazi za matawi ya umoja huo na chama kwa ujumla kuongeza idadi ya wanachama hai watakaoiwezesha CCM kushinda katika uchaguzi mkuu ujao.  

Wito huo umetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa UWT  Zanzibar, Bi. Salama Aboud Talib katika ziara ya kuwapongeza na kuwahamasisha  viongozi wapya wa ngazi za matawi waliochaguliwa hivi karibuni katika Majimbo ya Chaani na Mkwajuni Wilaya ya Kaskazini “A” kichama Unguja.

Amewataka  viongozi hao kujua idadi kamili ya wanachama na kubaini ni wanachama wangapi wamefariki ili watolewe katika orodha ya wanachama hai kwa lengo la kupata idadi ya uhakika ya  wanachama watakaoendelea kuibeba CCM katika  michakato mbali mbali ya kisiasa.

Amesema   viongozi waliochaguliwa wameaminiwa hivyo wanatakiwa kuwatumikia na kuwaongoza vizuri  wanachama waliowachagua kwa kutetea maslahi ya CCM kwa vitendo.

Aidha  Bi. Salama Aliwataka wanawake hao kuwa na masimamo imara wa kuendelea kuwachagua viongozi wenye sifa na uwezo wa kuzitumikia chama na jumuiya kwa uadilifu badala ya kuwatumikia watu wachache wenye nguvu za kisiasa na uwezo wa kifedha.

Hata hivyo kupitia ziara hiyo, Naibu Katibu Mkuu huyo amesisitiza kudumishwa dhana ya umoja ndani ya jumuiya hiyo ili wasimamie ipasavyo matakwa ya Katiba ya CCM na Jumuiya waweze kufanikisha majukumu mbali mbali ya kuendelezwa kwa dhana ya umoja na mshikamano ndani ya jumuiya hiyo .

Mapema Katibu wa Idara ya Organazesheni wa UWT Zanzibar,  Bi. Tunu Juma Kondo, akimkaribisha  Naibu Katibu Mkuu huyo ameeleza kuwa matarajio ya CCM na UWT kutoka kwa viongozi wapya wa umoja huo wa ngazi za matawi ni kuona mabadiliko ya haraka ya kiutendaji yatakayoongeza ufanisi ndani ya taasisi hiyo.

Naye Bi.Fatma Khamis mussa kutoka Tawi la Chaani, amewasihi viongozi wa ngazi za juu wa umoja huo pamoja na chama kufanya ziara za mara kwa mara katika ngazi za Matawi ili kuongeza hamasa ushirikiano kwa wanachama na viongozi wa ngazi hizo.

Pamoja na hayo katika  mkutano huo Naibu Katibu Mkuu huyo Bi. Salama Aboud kwa kushirikiana na Mwakilishi wa Viti Maalum Mkoa wa Kaskazini Unguja  Bi. Mtumwa Suleiman wametoa sadaka ya fedha kwa akina Mama wa UWT kwa ajili ya futari  ya Mwezi mtukufu wa ramadhani.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni