Jumamosi, 17 Juni 2017

DKT. MABODI: ASEMA CCM ITAENDELEA KUENZI SIASA ZA USHINDANI WA KISERA.

Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar , Dkt. Abdulla Juma Saadalla “Mabodi” akisalimiana na Mbunge wa Viti Maalum  Wanawake (CCM)  (MNEC) Bi. Khadija Hassan Aboud pamoja  na  viongozi  mbali mbali wa UWT Mkoa wa Mjini  Zanzibar mara baada ya kuwasili katika Ukumbi wa Mikutano wa Mkoa wa Mjini CCM uliopo Amani Unguja.

Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar , Dkt. Abdulla Juma Saadalla “Mabodi” akiwahutubia  mamia  ya wanachama na viongozi  wa UWT Mkoa wa Mjini  Unguja, mara baada ya kufungua mafunzo ya Wanawake na Uongozi katika siasa huko  Ukumbi wa Mikutano wa Mkoa wa Mjini CCM uliopo Amani Unguja. 

 Baadhi ya Viongozi na wanachama wa UWT walioudhuria katika mafunzo hayo wakifuatilia kwa umakini nasaha za mgeni rasmi  Dkt. Abdulla Juma Saadalla “Mabodi”  wakati  akizungumza mara baada ya kufungua  mafunzo hayo.

Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Mjini, Bi. Waridi Juma Othman akizungumza  na viongozi na wanachama  hao kabla ya kumkaribisha mgeni  rasmi afungue  mafunzo hayo  Ukumbi wa Mikutan    o wa Mkoa wa Mjini CCM uliopo Amani Unguja. 

 Mbunge wa Viti Maalum  Wanawake (CCM)  (MNEC) Bi. Khadija Hassan Aboud akitoa maneno ya shukrani kwa mgeni rasmi  Dkt. Abdulla Juma Saadalla “ Mabodi”  kabla ya kuanza mafunzo hayo.

 Katibu wa NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi  Bi. Waride  Bakar  Jabu  akiwapungia na kuwasalimia  washiriki wa mafunzo hayo  ambao ni viongozi na wanachama wa UWT Mkoa wa Mjini Unguja.

 Mkufunzi  wa Mafunzo  hayo  Bi. Emiley Nelson Fwambo  akizungumza na washiriki wa mafunzo  ya Wanawake  na Uongozi  katika siasa.

NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar , Abdulla Juma Saadalla “ Mabodi” amesema  CCM itaendelea kufanya ushindani wa sera za maendeleo kisiasa  zitakazowanufaisha wananchi wa makundi yote mijini na vijijini.

Kauli hiyo ameitoa wakati akifungua Mafunzo ya Wanawake na Uongozi kwa wanachama na viongozi wa UWT Mkoa wa Mjini huko Amani Zanzibar, Dkt. Mabodi amesema  wananchi wa visiwa vya Zanzibar kwa sasa wanachohitaji ni siasa za ushindani wa Sera za maendeleo na sio sera za vurugu na migogoro.

Dkt. Mabodi ameeleza kuwa  taifa lolote linalotamani kuendelea kiuchumi ni lazima wananchi wake wakubali kwa vitendo dhana ya siasa za ustaarabu katika kudumisha amani na utulivu wa nchi ili kufanya kazi za kujiongezea kipato katika hali ya  Amani na utulivu.

Aidha  Naibu Katibu Mkuu huyo amesema  ushindi wa CCM katika chaguzi mbali mbali za dola unatokana na nguvu za Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi  katika kuunga mkono harakati mbali mbali za kisiasa hadi kuhakikisha chama kinaingia madarakani.

“ kila mtu ndani ya Chama Chetu anajua na kutambua mchango wa Wanawake katika medali za kisiasa, wao ndio wamekuwa mstari wa mbele kwa kila kitu ikiwemo kujitokeza kwa wingi kupiga kura halali za kuiletea ushindi CCM.

Pia naahidi kuwa nitakuwa nanyi bega kwa bega kwa lengo la kuimarisha chama na jumuiza zake sambamba na kusimamia vyema serikali itekeleze Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020 ili wananchi mpate maendeleo ya kudumu.”, amesema Dkt. Mabodi.

Kupitia Mkutano huo Dkt. Mabodi amewasihi  viongozi na watendaji wa  Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) kushuka ngazi za chini kiutendaji hasa matawi na mashina kwa lengo la kuratibu changamoto zinazowakabili  wananchi ili zitafutiwe ufumbuzi wa kudumu na serikali.

Amewapongeza  viongozi wa UWT waliojitolea kuanzisha mafunzo ya uongozi kwa wanawake wenzao ili wapate ujuzi wa kufanya siasa za maendeleo zitakazowajengea ujasiri wa kujenga hoja imara zinazokubalika katika ulimwengu wa siasa za ushindani.

Sambamba na hayo aliwapongeza Mwenyekiti wa CCM Taifa ambaye pia ni Rais wa Zanzibar Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar  ambaye pia ni Rais wa  Zanzibar  na Mwenyekiti wa baraza la Mapinduzi kwa kutekeleza ipasavyo ilani ya Chama hicho hasa katika juhudi za kulinda rasilimali za nchi zisihujumiwe na baadhi ya watu wanaotanguliza mbele maslahi binafsi.

Akizungumzia Uchaguzi wa ngazi ya Wadi unaoendelea hivi sasa katika Chama na Jumuiya  Ameziagiza  kamati zinazosimamia zoezi hilo zifanye kazi ya ziada ya kuhakikisha wanapatikana viongozi safi wasiokuwa na sifa za usaliti.

Mapema akizungumza katika Mkutano huo Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Mjini, Bi. Waridi  Juma Othman aliahidi kuwa wanawake hao watatumia vizuri mafunzo ya uongozi katika siasa kama muongozo wa kufanya kazi za kisiasa kwa ufanisi mkubwa.

Akitoa neno la shukrani  Mbunge wa Viti Maalum wanawake( MNEC), Khadija Hassan Aboud alisema lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo wanawake wa CCM ili waweze kuzitumika vizuri fursa za uongozi zinazopatikana ndani ya chama na serikali kwa ujumla.

Mafunzo hayo ya siku moja  yameandaliwa na Mbunge wa Viti Maalum wanawake( MNEC), Khadija Hassan Aboud kwa kushirikiana na Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mjini, Faharia Shomari Shomari Khamis  kwa lengo la kuwajengea uwezo wanawake wa UWT ili wapate ukomavu wa kisiasa utakaosaidia CCM kushinda katika uchaguzi wa mwaka 2020.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni