Jumatano, 7 Juni 2017

DR.SHEIN AMEUNGANA NA MAMIA YA WANANCHI KATIKA MAZISHI YA PROF. ISHAU


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr. Ali Mohamed Shein Akisalimiana na baadhi ya viongozi walioudhuria katika mazishi ya Marehemu Prof. Ishau  Abdulla Khamis huko Donge Wilaya ya Kaskazini "B" Unguja.
 Viongozi mbali mbali wa Serikali na Chama akiwemo Rais wa Zanzibar Dkt. Ali Mohamed Shein , Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar  Balozi Seif Ali Idd, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Abdulla Juma Saadalla” Mabodi”  wakiongozwa na Katibu wa Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar, Sheikh Fadhil Suleiman Soraga wakati wa kuswalia maiti katika msikiti wa Donge Wilaya ya Kaskazini "B"Kaskazini Unguja.
 Baadhi ya wananchi wamebeba jeneza la maiti wakielekea katika eneo la mazishi huko Donge Wilaya  ya Kaskazini  "B"  Unguja.
 Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Abdulla Juma Saadalla” Mabodi”  akishiriki katika mazishi ya Marehemu Prof. Ishau kwa kuweka udongo katika kaburi huko Wilaya ya Kaskazini "B" Donge.



RAIS wa Zanzibar  na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein leo ameungana na mamia ya wananchi katika mazishi ya aliyewahi kuwa Mjumbe  wa Halmashauri Kuu na Afisa Mwandamizi (Mstaafu) wa Idara ya Organaizesheni CCM Zanzibar , Prof. Ishau  Abdullah Khamis huko kijijini kwao  Donge  Wilaya ya Kaskazini "B" Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Marehemu Prof. Ishau amefariki  jana katika Hospitali ya Taifa Muhimbili alipokuwa akipatiwa matibabu baada ya kuuguwa kwa muda mrefu maradhi ya figo.

Katika mazishi hayo Dkt. Shein ameambatana na viongozi mbali mbali wa chama na serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar  wakiwemo Makamo wa  pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dkt. Abdulla Juma  Saadalla “Mabodi”
,Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Vuai Mwinyi Mohamed, Naibu Kadhi Mkuu wa Zanzibar Sheikh Hassan Othman Ngwali, Katibu wa Mufti Sheikh Fadhil Suleiman Soraga.

Prof.Ishau amepata elimu yake ya  msingi  katika  Shule ya msingi Donge  na kusoma elimu ya Chuo Kikuu Makerere Uganda na baadae kwenda nchini Hungry alikopata kiwango cha elimu ya Uprofesa na kurudi nchini kwa ajili ya kufanya kazi za umma.

Aidha  Marehemu Prof. Ishau enzi za  uhai wake aliwahi kushika nyadhifa mbali mbali katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ikiwemo Mkuu wa Wilaya, Mkuu wa Mkoa, Ubunge,  Mwalimu katika Chuo cha Uchumi (Dar), Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi na  Waziri wa Utalii na Misitu.

Pia  Prof.Ishau hadi kufariki kwake alikuwa ni Mwenyekiti wa Bodi ya Ofisi ya Takwimu Zanzibar  nafasi  ambayo ameteuliwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein.

Kwa upande wa Chama marehemu aliwahi kuwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu, Katibu wa Fedha, uendeshaji na Miradi ya Chama, Mkuu wa Kitengo cha Uchaguzi katika Idara ya Organaizesheni - Afisi Kuu ya CCM Zanzibar, cheo alichoshikilia hadi mwaka 2014, alipostaafu Utumishi wa Chama.

Chama Cha Mapinduzi kinaungana na wanafamilia, ndugu na marafiki wa marehemu Tunamuomba Mwenyezi Mungu muumba Mbingu na Ardhi na Vyote viliomo ndani aiweke roho ya marehemu mahali pema Peponi amin.

Marehemu amefariki akiwa na umri wa miaka 75  na ameacha  watoto Sita. 




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni