Jumatatu, 3 Desemba 2018

DK.MABODI: AWATAKA WATENDAJI WA SERIKALI ZA MITAA KUSHUKA KWA WANANCHI.


 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Mabodi akiwa na wananchi wa Shehia ya Mbuyu Tende katika ziara yake ya kukagua utekelezaji wa ilani ya CCM  juu ya shughuli zilizotekelezwa na Halmashauri chini ya mfumo wa ugatuzi.
  NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Mabodi  akionyeshwa kisima cha maji Safi na Salama.



  NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Mabodi akipewa maelezo na Katibu wa Kikundi cha ushirika chenye mashine ya kisasa aina ya G-20 ya kukoboa mpunga huko Kisongoni.

 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM  Zanzibar  Dk. Abdulla Juma Mabodi akiwaonyesha moja ya ripoti ya ukaguzi wa miradi watendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini 'A'  Unguja(hawapo pichani)



NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.

WATENDAJI wa Serikali za Mitaa nchini wametakiwa kujenga utamaduni wa kufanya ziara za kiutendaji kwa wananchi wa ngazi zote ili kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu changamoto zinazowakabili wananchi.

Rai hiyo ameitoa Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Saadalla Mabodi katika mwendelezo wa ziara zake za kukagua utekelezaji wa Ilani katika Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini 'A' Unguja.

Amesema lazima watendaji na viongozi waliopewa dhamana ya kusimamia mfumo wa ugatuzi washuke kwa wananchi kwa lengo la kufuatilia masuala mbali mbali yatakayosaidia kumaliza changamoto zinazowakabili wananchi katika ngazi za serikali za mitaa.

"Lengo la Serikali Kuu kushusha madaraka katika Serikali za Mitaa kupitia dhana ya ugatuzi ni kuongeza ufasini wa uimarishaji wa huduma za kijamii kwa wananchi, hivyo watendaji nyote mlioaminiwa na kupewa dhamana ya kuwahudumia wananchi lazima muwe katibu na jamii", amesisitiza Dk.Mabodi.

Katika maelezo yake Naibu Katibu Mkuu huyo, amewataka wamewasihi watendaji hao kuwa wabunifu katika kuibua miradi mbali mbali ya kijamii inayoweza kuongeza ufanisi wa kutoa huduma bora kwa wananchi.

Pia Dk. Mabodi kupitia ziara yake hiyo ameelezea kuridhishwa kwake na utendaji mzuri wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini 'A' katika kutekeleza vizuri miradi inayotekelezwa kupitia ugatuzi.

Dk. Mabodi aliwasihi wananchi kuendelea kuthamini na kuamini juhudi kubwa za kimaendeleo zinazofanywa na Serikali ya awamu ya Saba ya Zanzibar inayoongozwa na Dk. Ali Mohamed Shein, kwa utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM ya mwaka 2015/2020.

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini 'A' Mussa Ali Makame, amesema katika ukusanyaji wa mapato katika mwaka 2018/2019 wamekisia kukusanya shilingi milioni 869,300,000 hadi Novemba wamekusanya kiasi cha shilingi milioni 157,697,081 sawa na asilimia 18.

Amesema Halmashauri hiyo imetoa mafunzo kwa wakulima 144 ili kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula cha biashara.

Aidha ameeleza kuwa wametoa mafunzo kwa wafugaji 1,027 wa ng'ombe na mbuzi kwa lengo la kuwajengea uelewa wa matumizi ya huduma ya chanjo.

Mussa amesema jumla ya Shule 32 za Wilaya ya Kaskazini 'A' Unguja ambapo wanafunzi 6,158 wa maandalizi wamepatiwa huduma ya lishe kwa mwaka wa fedha kwa mwaka wa fedha wa 2017/2018 pamoja na 2018/2019.

Akizungumza Mjumbe wa Kamati Maalum ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Zanzibar Amini Salmin Amour, amewataka wataalamu wa fani mbali mbali waliopelekwa katika mfumo wa ugatuzi kutumia ujuzi wao kuwaelimisha wananchi juu ya masuala ya kilimo bora, ufugaji, uvuvi sambamba na kuhakikisha miradi yote inayotekelezwa inawanufaisha watu husika.

Naye Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja Idd Ali Ame, amempongeza Naibu Katibu Mkuu huyo Dk.Mabodi kwa ziara yake hiyo ambayo ameitaja kuwa imeongeza ari na kasi ya watendaji kutatua kero za wananchi kwa wakati.

Kwa upande wake Mkaazi wa Kijiji cha Mbuyu Tende Ramadhan Ali Mcha ameeleza kuwa mfumo wa ugatuzi umewasaidia wananchi kupata huduma muhimu za kijamii.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni