Jumapili, 6 Mei 2018

DK.SHEIN-ATOA ONYO KALI KWA WASAKA URAIS WA Z'BAR.


NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.

 MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein akiwahutubia Mabalozi wa CCM Wilaya ya Kati Unguja, mkutano uliofanyika katika ukumbi wa Chuo Kikuu Cha Taifa Zanzibar (SUZA) kilichopo Tunguu Mkoa wa Kusini Unguja.

  MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein akipokea risala ya mabalozi wa CCM Wilaya ya Kati Unguj.

 BAADHI ya wajumbe wa NEC waliofuatana na Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar katika ziara yake ya kuzungumza na mabalozi wa CCM Wilaya ya Kaskazini Unguja.
 MWENYEKITI wa CCM Mkoa wa Kusini Unguja Ramadhani Abdallah Ali 'Kichupa' akizungumza na mabalozi wa CCM Wilaya ya kati , kabla ya kumkaribisha Naibu Katibu Mkuu wa CCM Dk.Mabodi katika ziara ya Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk.Shein kuzungumza na mabalozi.

 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdalla Jumsa Mabodi pamoja na viongozi mbali mbali wa CCM na junmuiya zake waliofutana na Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk.Ali Mohamed Shein wakiimba wimbo wa mashujaa wa Zanzibar katika ziara ya kuzungumza na mabalozi wa CCM Wilaya ya Kati.




      MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk.Ali Mohamed Shein amewaonya baadhi ya watu wanaofanya kampeni za kusaka Urais wa Zanzibar kabla ya muda wa kufanya hivyo kufika na kusisitiza  kuwa yeye bado ni Rais wa Zanzibar.

Amesema kuna baadhi ya viongozi wa Chama na Serikali tayari wameanza kupanga timu za Urais badala ya kushughulika na mambo ya msingi ya kufanya shughuli za Chama zitakazofanikisha kuiweka serikali madarakani katika uchaguzi mkuu ujao.

Onyo hilo amelitoa katika mwendelezo wa ziara zake za kuimarisha Chama Cha Mapinduzi kwa kuzungumza na mabalozi wa mashina katika Wilaya ya kati Unguja,iliyofanyika ukumbi wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar(SUZA) ulipo Tunguu Mkoa wa Kusini Unguja.

Amesema nafasi ya Urais ndani ya CCM haipatikani kwa kampeni na makundi yasiyokuwa halali bali inapatikana kwa utaratibu maalum kupitia vikao vya kikatiba ambavyo vipo kwa mujibu wa Katiba na miongozo na kanuni  mbali mbali za CCM.

Alibainisha kuwa kwa wakati tofauti amewatahadharisha baadhi ya viongozi na wanachama hao kuacha tabia hizo kwani zinaweza kuleta migogoro na mgawanyiko isiyokuwa ya lazima ndani ya CCM kabla ya uchaguzi mkuu ujao.

Amebainisha kuwa watu hao wanaosaka Urais kwa sasa wasipoacha tabia hiyo na kuvumilia mpaka 2020, atawachukulia hatua kali za kinidhamu zikiwemo kufikishwa katika vikao vya usalama na maadili vya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC) ili wahojiwe na kuchunguzwa dhidi ya mwenendo wao  juu ya mwenendo wao usiokuwa na manufaa kwa CCM.

Alisema viongozi, watendaji na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi wanatakiwa kuelekeza nguvu zao katika kutekeleza mipango mbali mbali ya kukisaidia Chama kushinda na sio kuangaika na urithi wa kiti cha Urais.

“Naheshimu Katiba ya nchi muda wangu ukifika naondoka madarakani kwani huo ndio utaratibu wa Chama chetu na kwa mujibu wa sheria za nchi, lakini sifurahishwi hata kidogo kuona baadhi yenu mnaanza kuangaika na Urais badala ya kufanya kazi za kuitafutia ushindi CCM mwaka 2020", alisisitiza Dk.Shein na kuwataka Mabalozi na viongozi wengine wa ngazi za mashina kukataa kuingizwa katika mitandao hiyo ya kampeni.

Akizungumzia umuhimu wa viongozi hao, Dk.Shein alisema CCM inathamini mchango mkubwa wa kuimarisha Chama unaofanywa na viongozi wa mashina ambao ndio jeshi la kisiasa la Chama Cha Mapinduzi.
Alisema Chama kitaendelea kuisimamia vizuri serikali ili itekeleze Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020 kama ilivyowaahidi wananchi katika kampeni za uchaguzi zilizopita.

Kupitia mkutano huo Dk.Shein aliwataka viongozi hao kujenga utamaduni wa kusoma Katiba ya CCM  ya mwaka 1977 toleo la 2017, ili wajue majukumu waliokuwa nayo kwa mujibu wa Katiba na kuyatekeleza ipasavyo.

Alisema katika hatua za kuzitafutia ufumbuzi changamoto zinazowakabili wananchi, serikali inaendelea na mikakati ya matengenezo ya barabara ya maeneo ya Mwanakwerekwe na kutengeneza daraja la kisasa katika eneo la Kibonde mzungu ili kuwaondoshea usumbufu wananchi wa Mkoa wa Kusini Unguja.

Aidha alisema kwa upande wa changamoto ya maji yanayotwaama katika eneo la Kibonde mzungu tayari serikali inaendelea na mikakati ya kuanza ujenzi wa daraja kubwa litakaloweza kumaliza tatizo hilo la maji katika maeneo hayo.

Pia aliwambia mabalozi hao kuwa hakuna wa kuzuia ushindi wa CCM katika uchaguzi mkuu ujao kwani Chama hicho kimejiandaa kushinda kwa nguvu za demokrasia, kwani kina wananchi wengi wanaokiamini na kukiunga mkono kutokana na utekelezaji mzuri wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015/2020.

Alisema Serikali inaendelea kutekeleza kwa vitendo dhamira ya ASP ya kuwapatia wananchi huduma bure za kijamii hasa elimu na Afya.
Akizungumza Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Mabodi, amesema mabalozi wa Chama Chama Mapinduzi wamekuwa mstari wa mbele kurejesha Chama kwa wananchi.

 Alisema Chama Cha Mapinduzi kwa sasa kinaendelea na mfumo wa uongozi shirikishi unaowashirikisha viongozi wa ngazi tofauti jambo ambalo Dk.Shein anaendeleza mfumo huo kwa kuzungumza na mabalozi hao kila mwaka.

 Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kusini Unguja, Ramadhan Abdalla Ali 'Kichupa', alipongeza Dk.Shein kwa juhudi zake za kuwaletea maendeleo wananchi wa Mkoa huo katika nyanja za kijamii,kiuchumi na kisiasa.

Mapema akisoma risala ya mabalozi, ndugu Mkombe Vuai Khamis alisema serikali ya awamu ya saba inayoongozwa na Dk.Shein wananchi wameshuhudia kuimarika kwa sekta mbali mbali nchini hasa suala zima la kuanzisha penchini ya kuwalipa  wazee ya shilingi 20,000 kwa kila mwezi.

Kupitia risala hiyo walimpongeza Dk.Shein kwa kuasisi na kuendeleza kwa vitendo hatua yake ya kutoa pencheni kwa wazee hatua ambayo ni ya kishujaa kwani imesaidia mamia ya wazee wengi kupata fedha za kujikimu kila mwezi.

Walisema wataendelea kulinda na kutetea maslahi na miongozo ya Chama Cha Mapinduzi kwa vitendo ili kishinde kwa ngazi zote katika uchaguzi mkuu ujao.




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni