Jumamosi, 10 Machi 2018

HIMAHIMA YAFANYA USAFI PANGAWE


NA EMMANUEL MOHAMED,ZANZIBAR

TAASISI isiyokuwa ya kiserikali ya Hima Hima,imefanya usafi katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Mjini, visiwani humu ambapo ni sehemu ya kuzuia maambukizi ya magonjwa ya milipuko.

Akizungumza baada ya kufanya usafi huo,Katibu wa Uhusiano wa Taasisi hiyo,Othman Kibwana alisema taasisi hiyo inatarajia kufanya usafi endelevu kwenye majimbo yote ya mjini ambayo yako kwenye hali isio nzuri.

Katibu huyo aliongeza kuwa hatua hiyo itasaidia kutoa fursa kwa vijana ya kujiajiri kwenye ubebaji taka kama ilivyo agizwa na Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar(SMZ).

"Tumeamua kufanya hivi kutokana kuwa kipindi kinachokuja ni cha mvua hivyo mazingira ya yanapaswa kuwa safi ili kutotokea kwa magonjwa ya milipuko kama kipindipindu hivyo moja ya mipango yetu ni kufanya usafi kwenye maeneo hayo ya majimbo yasiokuwa safi,"alisema Katibu huyo.

Aliongeza kuwa Taasisi hiyo imeanzia kufanya usafi kwenye maeneo ya Pangawe kutokana na kuwa taasisi hiyo ya Hima Hima imefanya tafiti na kubaini kuwa sehemu hiyo ndio ina mazingira ya sio kuwa safi.

"Kuna maeneo ambayo yana taka nyingi lakini kutokana na sababu zisizotatulika ikiwemo kukosa vitendea kazi, magari ya kubebea taka ambapo taka nyingi zinakaa kwa muda mrefu hivyo leo tumeamua kuanzia hapa na kwengine ni Magogoni pamoja na sehemu ambazo milipuko ikija inakuwa ya mwanza kutokea,"alisema

Kwa upande wake Mwakilishi wa jimbo la Pangawe, Khamis Juma Mwalim,alisema hatua hiyo ya taasisi hiyo kufanya usafi kwenye maeneo hayo ya Pangawe itasaidia kutatua changamoto ambazo zilikuwa zikichochea kuwa na mazingira machafu.

Alisema kipindi hichi katika maeneo hayo ya Pangawe kumekuwa na wingi wa taka pamoja na vijana kujaribu kuzizoa na kwamba hatua hiyo ya taasisi hiyo itasaidia kuziondoa kwa uwepesi.

"Taka hizi zitaondoka kwa haraka kutokana na kuwa vifaa vya kubebea viko vingi ikiwemo magari ya taka na nguvu kazi ya kubebea taka hizo wako wengi hivyo usafi wa mazingira kwenye eneo la Pangawe litakuwa limekwisha,"alisema.  

Naye Mjumbe wa Taasisi hiyo ya Hima Hima,Nadra Juma Mohamed, alisema ufanyaji usafi huo ni moja ya hamasa katika kusafisha maeneo ya mbalimbali ya Zanzibar ili kuepuka na magonjwa hayo ya milipuko.

"Wananchi wanatakiwa kuhakikisha wanakuwa na tabia ya kufanya usafi na kwamba wasiingize na itikadi yeyote hivyo ni lazima tupende mazingira yetu yenyewe,"alisema

Mjumbe huyo alisena ufanyaji usafi ni moja ya fursa ya ajira kwa vijana na kwamba watu wakiwa wanatoa gharama za kulipia ili kubebewa taka wanapata kuwa na ajira ya uhakika hivyo kundi hilo linapaswa kuona umuhimu huo.





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni