Jumatatu, 15 Juni 2015

TAMKO LA PAMOJA LA VIONGOZI


TAMKO LA PAMOJA LA VIONGOZI, WATENDAJI WA CHAMA CHA MAPINDUZI NA JUMUIYA ZAKE  WA MIKOA SITA YA KICHAMA YA ZANZIBAR LA KUKUOMBA MAKAMU MWENYEKITI WA CCM NA RAIS WA ZANZIBAR MHE. DKT. ALI MOHAMED SHEIN KUCHUKUA FOMU YA KUOMBA KUTEULIWA KUGOMBEA KITI CHA RAIS WA ZANZIBAR KUPITIA CHAMA CHA MAPINDUZI KATIKA UCHAGUZI MKUU WA MWAKA 2015


Kwa niaba ya Viongozi, Watendaji wa Chama na Jumuiya zake wa Mikoa sita ya Kichama ya Zanzibar,  tunayo heshima kubwa leo kusimama hapa kwa niaba yenu ili kuwasilisha tamko letu hili lenye nia na madhumuni ya kumuomba kiongozi wetu mpendwa Makamu Mwenyekiti wa CCM, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, kwenda kuchukua Fomu ya kuomba kuteuliwa kugombea nafasi ya kiti cha Rais wa Zanzibar, katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.

Awali ya yote ninapenda kutumia fursa hii kumshukuru Mola wetu mtukufu mwingi wa rehema na muumba mbingu na ardhi pamoja na vyote viliyomo, kwa kutujaalia afya njema na kutuwezesha kukusanyika hapa leo hii kwa salama na amani.

Kwa niaba ya wanachama wa CCM, Jumuiya   pamoja na wananchi wote wapenda amani, umoja na mshikamano wa kitaifa wa Mikoa na Wilaya zote za Zanzibar, sisi Viongozi wa Chama, Jumuiya pamoja na Watendaji  wa CCM kutoka Mikoa sita ya kichama ya Unguja na Pemba, leo hii tarehe 14 Juni 2015, tumekutana hapa kwenye ukumbi wa Nyumba za Wazee Sebleni Unguja, ili kutafakari na kujenga mustakabali wa uhai wa Chama chetu.

Kama tunavyofahamu kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, mwaka huu wa 2015 tunakabiliwa na Uchaguzi Mkuu wa kumchagua Rais wa Zanzibar, Wabunge, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi pamoja na Madiwani.  Huu ni uchaguzi mkuu wa tano (5) tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa hapa Tanzania hapo mwaka 1992. 

Aidha, Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) tayari imeshatangaza ratiba ya uchaguzi huo ambao utafanyika tarehe 25 Oktoba 2015.  Vile vile hivi karibuni CCM imetangaza ratiba ya mchakato wa uteuzi wa mgombea wake katika uchaguzi huo pamoja na ule wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  Ratiba hiyo imeanza tarehe 3 Juni 2015 hadi tarehe 2/7/2015.

Hadi kufikia jana tarehe 13 Juni 2015, wakati idadi ya wanachama wa CCM waliochukua fomu za kuomba kuteuliwa kugombea nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imefikia 32, hakuna mwanachama wa CCM hata mmoja aliyejitokeza kuchukua fomu ya kuomba kuteuliwa kugombea nafasi ya Rais wa Zanzibar, hali ambayo inathibitisha kwamba, wana CCM wote hapa Zanzibar bado tunaridhika na uongozi wa Mhe. Dkt. Shein.  Hivyo sisi viongozi wa CCM wa Mikoa na Wilaya kwa kushirikiana na Jumuiya zetu pamoja na wazee wetu tumeona tunao wajibu wa kukutana ili kutafakari hali hiyo na kuipatia majibu.


Kwa kuzingatia historia ya Chama chetu na uzito wa changamoto iliyo mbele yetu tumeamua kukutana pahala hapa (Nyumba za Wazee Sebleni) ili kujikumbusha wajibu wetu kama viongozi wa Chama Cha Mapinduzi, walinzi na watetezi wa Mapinduzi matukufu ya Zanzibar ya tarehe 12 Januari 1964 ambayo ndio chimbuko la majengo haya.

Baada ya kutafakari kwa kina na kupima kazi iliopo mbele yetu katika kusimamia maendeleo ya wananchi, kudumisha umoja, amani, Muungano wa Tanganyika na Zanzibar pamoja na Mapinduzi yetu matukufu ya tarehe 12 Januari 1964, kwa kauli moja tumekubaliana kumuomba kiongozi wetu mpendwa Makamu Mwenyekiti wa CCM, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, kwa mara nyingine tena ajitokeze kwenda kuchukua fomu ya kuomba kuteuliwa kugombea nafasi ya Rais wa Zanzibar kupitia Chama Cha Mapinduzi.

Kwa hakika tunazo sababu nyingi za kumuomba afanye hivyo, lakini kwa ajili ya kuokoa muda ninaomba nizitaje chache kwa umuhimu wake, nazo ni kama zifuatazo:-
    a)    Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein bado anakidhi vigezo na sifa zote zinazohitajika kwa mujibu wa Katiba na sharia za uchaguzi.

   b)   Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita ameonesha uwezo mkubwa wa kuongoza nchi yetu na kusimamia kwa ufanisi mkubwa utekelezaji wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 – 2015.

    c)    Anao uwezo mkubwa wa kuwaunganisha Wazanzibari na kudumisha umoja, amani, na Muungano wetu wa Tanganyika na Zanzibar.
  
    d)   Ameiongoza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yenye mfumo wa umoja wa kitaifa kwa weledi mkubwa na kuwa mfano bora wa kuigwa na Mataifa mengine duniani.

    e)    Ana tabia ya upole, uadilifu, uaminifu na unyenyekevu kwa wananchi wa rika na jinsia zote.

   f)     Hana makuu wala ubaguzi wa aina yoyote.  Ni mpenda maendeleo na mwanamapinduzi wa kweli.

    g)    Ni mwenye msimamo thabiti.  Katika masuala ya msingi yanayohusu nchi na wananchi hayumbi na wala hayumbishwi.

   h)   Kuanzia tarehe 17/11/2014 hadi tarehe 4/12/2014, Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, alitembelea Mikoa na Wilaya zote za Kichama hapa Zanzibar.  Katika ziara hizo alikutana na kuzungumza na viongozi wa mashina (Mabalozi) na Maskani zote za CCM Unguja na Pemba.  Kwa kupitia mikutano hio viongozi hao ambao ni kundi kubwa la wana CCM walimuomba Dkt. Ali Mohamed Shein, afikirie kugombea tena nafasi hii ya Rais wa Zanzibar katika Uchaguzi Mkuu wa 2015.

Kama nilivyoeleza hapo juu, kwa hakika sababu ni nyingi inatosha tu kusema kwamba, kwa maoni yetu Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, bado ni jembe la kujivunia na tunaimani kubwa ya kwamba, katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 ataendelea kutuvusha na hakuna mbadala wake kwa sasa.

Hivyo kwa heshima na unyenyekevu mkubwa tunamuomba atukubalie ombi letu hili na kwa mara nyingine tena akachukue Fomu ya kuomba kuteuliwa kugombea kiti cha Rais wa Zanzibar kupitia CCM!

KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni