NA IS-HAKA
OMAR, ZANZIBAR.
NAIBU Katibu Mkuu wa
CCM Zanzibar, Nd. Vuai Ali Vuai amewasihi vijana wa Chama hicho kuwania
nafasi za uongozi katika ngazi za mashina hasa Ubalozi wa Nyumba kumi ili
kuongeza nguvu za kiutendaji katika ngazi hizo.
Amesema nafasi hizo
kwa kiwango kikubwa zimekuwa zikishikiliwa na Wazee ambao umri wao
hauwaruhusu kuendelea kuhudumu katika uwanja wa mapambano ya kisiasa kwa sasa.
Akizungumza
Naibu Katibu Mkuu huyo na viongozi, Watendaji na Wanachama wa Jimbo la Jang’ombe
katika mwendelezo wa ziara ya kuimarisha uhai wa Chama iliyofanyika
katika Tawi la CCM Matarumbeta Unguja.
Vuai alisema nguvu
za taasisi hiyo zinaanzia katika ngazi za chini za uongozi zinazotakiwa
kusimamiwa na viongozi vijana wenye uwezo wa kupigania maslahi taasisi
hiyo bila ya woga.
“ Kwa miaka mingi
kila ukifika uchaguzi wa Chama na Jumuiya zake wanaojitokeza kuwania ngazi za
ubalozi wa nyumba kumi ni Wazee na watu ambao umri wao unaelekea katika utu
uzima, ambapo vijana mnazikimbia nafasi hizo na kugombea nafasi za juu wakati
ngazi za chini hazina watu wenye nguvu wa kuzisimami”.alisisitiza Vuai na
kuongeza kuwa mtaji wa kisiasa wa CCM ni wanachama hai wanaopatikana kupitia
ngazi za Matawi na Mashina.
Alieleza kuwa Wazee
kwa sasa wanatakiwa kupumzika huku wakipewa fursa za kushauri masuala mbali
mbali ya kisiasa ndani ya taasisi hiyo, kwani wao ndio mashujaa wanaostahiki
kupewa heshima kutokana na mshango wao wa kufanya mapinduzi ya mwaka 1964
yaliyoleta ukombozi wa kudumu kwa Wazanzibar.
Aliwashauri
wanachama hao kuwachagua viongozi imara wenye uwezo wa kupanga na kusimamia
mikakati endelevu ya kushinda katika Uchaguzi Mkuu wa Dola mwaka 2020.
Sambamba na rai hizo
alitoa tahadhari kwa viongozi, watendaji na wanachama wa chama hicho kuepuka
mbinu na propaganda za wapinzani kwani historia ya siasa za Zanzibar
zinathibitisha njama zinazofanyika hivi sasa kuiangamiza CCM zimewahi kutumika
kuihujumu Afro Shiraz Party (ASP) mwaka 1959.
Hata hivyo alisema
mipango ya kuimarisha CCM katika jimbo hilo iendane na dhana ya siasa na uchumi
kwa kutekeleza miradi mbali mbali ya kimaendeleo itakayosaidia shughuli za
kiutendaji.
Aidha aliwakumbusha
wafuasi wa Chama hiocho kutokubali kuwapokea Watu wanaohamia katika Jimbo hilo
kinyume na sheria za Uhamiaji kwani baadhi yao wanapandikizwa na vyama vya
upinzani kwa nia ya kujiandisha kupata ZAN ID ili wajiorodheshe kwenye daftari
la wapiga kura katika maeneo yasiyokuwa halali kwao kisheria.
Naye Kaimu Katibu wa
Jimbo hilo Nd. Said Bakar akisoma risala ya maendeleo na hali ya kisiasa
alisema toka kumalizika kwa uchaguzi wa marudio CCM imekuwa ikikubalika kwa
wananchi kutokana na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015/2020
kwa wananchi wote.
Wakizungumza wafuasi
hao kwa nyakati tofauti wameahidi kuzifanyia kazi kwa vitendo nasaha
zilizotolewa na viongozi wa ngazi za juu za chama hicho.
Hata hivyo
walielezea kukerwa na tabia za upotoshaji wa taarifa za viongozi wa umma katika
mitandao ya kijamii na kuiomba CCM ishauri serikali iwatafute watu wanaomiliki
mitandao hiyo ili wafikishwe katika vyombo vya kisheria.
MWISHO
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni