Alhamisi, 2 Machi 2017

Vijana ruhusa kugombea nafasi za Uongozi




NA IS-HAKA OMAR,  ZANZIBAR.

NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar,  Nd. Vuai Ali Vuai amewasihi vijana wa Chama hicho kuwania nafasi za uongozi katika ngazi za mashina hasa Ubalozi wa Nyumba kumi ili kuongeza nguvu za kiutendaji katika ngazi hizo.

Amesema nafasi hizo kwa kiwango kikubwa zimekuwa zikishikiliwa na Wazee  ambao umri wao hauwaruhusu kuendelea kuhudumu katika uwanja wa mapambano ya kisiasa kwa sasa.

Akizungumza  Naibu Katibu Mkuu huyo na viongozi, Watendaji na Wanachama wa Jimbo la Jang’ombe katika mwendelezo wa ziara ya kuimarisha  uhai wa Chama iliyofanyika katika Tawi la CCM Matarumbeta Unguja.

Vuai alisema nguvu za taasisi hiyo zinaanzia katika ngazi za chini za uongozi zinazotakiwa kusimamiwa na viongozi vijana  wenye uwezo wa kupigania maslahi taasisi hiyo bila ya woga.

“ Kwa miaka mingi kila ukifika uchaguzi wa Chama na Jumuiya zake wanaojitokeza kuwania ngazi za ubalozi wa nyumba kumi ni Wazee na watu ambao umri wao unaelekea katika utu uzima, ambapo vijana mnazikimbia nafasi hizo na kugombea nafasi za juu wakati ngazi za chini hazina watu wenye nguvu wa kuzisimami”.alisisitiza Vuai na kuongeza kuwa mtaji wa kisiasa wa CCM ni wanachama hai wanaopatikana kupitia ngazi za Matawi na Mashina.

Alieleza kuwa Wazee kwa sasa wanatakiwa kupumzika huku wakipewa fursa za kushauri masuala mbali mbali ya kisiasa ndani ya taasisi hiyo, kwani wao ndio mashujaa wanaostahiki kupewa heshima kutokana na mshango wao wa kufanya mapinduzi ya mwaka 1964 yaliyoleta ukombozi wa kudumu kwa Wazanzibar.

Aliwashauri wanachama hao kuwachagua viongozi imara wenye uwezo wa kupanga na kusimamia mikakati endelevu ya kushinda katika Uchaguzi Mkuu wa Dola  mwaka 2020.

Sambamba na rai hizo alitoa tahadhari kwa viongozi, watendaji na wanachama wa chama hicho kuepuka mbinu na propaganda za wapinzani kwani historia ya siasa za Zanzibar zinathibitisha njama zinazofanyika hivi sasa kuiangamiza CCM zimewahi kutumika kuihujumu Afro Shiraz Party (ASP) mwaka 1959.

Hata hivyo alisema mipango ya kuimarisha CCM katika jimbo hilo iendane na dhana ya siasa na uchumi kwa kutekeleza miradi mbali mbali ya kimaendeleo itakayosaidia shughuli za kiutendaji.

Aidha aliwakumbusha wafuasi wa Chama hiocho kutokubali kuwapokea Watu wanaohamia katika Jimbo hilo kinyume na sheria za Uhamiaji kwani baadhi yao wanapandikizwa na vyama vya upinzani kwa nia ya kujiandisha kupata ZAN ID ili wajiorodheshe kwenye daftari la wapiga kura katika maeneo yasiyokuwa halali kwao kisheria.

Naye Kaimu Katibu wa Jimbo hilo Nd. Said Bakar akisoma risala ya maendeleo na hali ya kisiasa alisema toka kumalizika kwa uchaguzi wa marudio CCM imekuwa ikikubalika kwa wananchi kutokana na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015/2020  kwa wananchi wote.

Wakizungumza wafuasi hao kwa nyakati tofauti wameahidi kuzifanyia kazi kwa vitendo nasaha zilizotolewa na viongozi wa ngazi za juu za chama hicho.

Hata hivyo walielezea kukerwa na tabia za upotoshaji wa taarifa za viongozi wa umma katika mitandao ya kijamii na kuiomba CCM ishauri serikali iwatafute watu wanaomiliki mitandao hiyo ili wafikishwe katika vyombo vya kisheria.
                                                 MWISHO





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni