Ijumaa, 4 Mei 2018

DK.SHEIN ASEMA USHINDI WA CCM 2020 UKO PALE PALE

 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi pia Makamo Mwenyekiti wa CCM Dk.Ali Mohamed Shein  akizungumza nao katika Ukumbi wa Skuli ya Sekondari Mohamed Juma Pindua Mkanyageni Mkoa wa Kusini Pemba akiwa katika ziara ya kuimarisha Chama cha Mapinduzi.

MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa kazi kubwa ya viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuanzia Shina hadi Taifa ni kuhakikisha chama hicho kinashinda uchaguzi Mkuu na ule wa Serikali za Mitaa na hatimae kukamata Dola kwa Zanzibar na Tanzania Bara.

Dk. Shein ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi aliyasema hayo leo wakati alipokuwa akizungumza na Mabalozi wa Wilaya ya Kusini Pemba huko katika ukumbi wa Skuli ya Sekondari ya Mohammed Juma Pindua Mkanyageni katika mkutano wake wa kukutana na Mabalozi wa Wilaya zote za Zanzibar ulioanza katika Wilaya hiyo.

Kuchaguliwa kwao ni kwa lengo la kukitumikia chama cha CCM ili kushinda uchaguzi na kuongoza dola kwani CCM ni chama kinachopendwa na wananchi wenyewe na chenye wafuasi wengi sana na hayo ni maelekezo ya Katiba ya CCM kuwa chama hicho ni lazima kishinde chaguzi zake zote.

Alisema kuwa CCM ni chama halisi cha Watanzania halisi na Wazanzibari halisi wanayoipenda nchi yao na hakina mbadala kwa Tanzania huku akisisitiza kuwa suala la ushindi katika uchaguzi ni lazima kwani ni maelekezo ya Katiba na Kanuni ya Chama hicho na kuzingatia historia ya TANU na ASP, CCM ni lazima ishike Dola kwa Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Aliongeza kuwa kazi kubwa ya siasa ni kutafuta na kuikamata Dola na hatimae kuikabidhi Serikali ambapo pia, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwapongeza Mabalozi wote waliochaguliwa na waliokuwa kura zao hazikutosha.

Alieleza kuwa kazi kubwa ya viongozi wa CCM ni kusimamia Ilani ya Uchaguzi ya Chama hicho na Mabalozi pamoja na viongozi wengine wa ngazi mbali mbali ni kuhakikisha inatekelezwa kwa vitendo.

Alieleza kuwa CCM ni chama chenye mtandao mkubwa sana wa utumishi na uongozi na kusisitiza haja ya kila kiongozi kutekeleza wajibu wake na kuwa makini katika utekelezaji wa majukumu yake na ndio maana mambo yake yamekuwa yakienda kwa kasi kutokana na mtandao huo.

Alisisitiza haja ya kuwa makini na kutekeleza vyema majukumu yao na kukiimaraisha chama cha Mapinduzi na kutumia fursa hiyo kueleza wajibu wa Mabalozi kwani ni watu wakubwa sana ndani ya chama hicho.

Alieleza kuwa wao ni walinzi namba moja wa Mapinduzi ya Zanzibar ya Januari 12, 1964 kwani wao ndio wa mwanzo wa kuyalinda, kuyadumisha na kuyatetea na viongozi wote wa ngazi za juu wataendeleaa kuwaunga mkono.Aidha, alisisitiza haja ya kujengwa kwa majengo ya chama, na kueleza umuhimu wa Mashina na kusisitiza kuwa Mabalozi ndio muhimili mkuu wa chama kwani wao ndio wawakilishi wa CCM katika nyumba zao wanazoziongoza.

Alieleza kuwa hakuna mkataba kuliko hati za Muungano ambayo ndio makubaliano makubwa waliyosainiwa kati ya Marehemu Mzee Ameid Karume na Mwalimu Julius Nyerere na kuwataka Mabalozi wasisikilize mambo yatakayowapotezea mwelekeo.

Alisema kuwa wanaCCM wapo macho na wapo hadhiri katika kuulinda na kuutetea Muungano wa Tanganyika na Zanzibar pamoja na Mapinduzi ya Januari 12, 1964.Aliongeza kuwa maadili ni ungozi wa chama hicho kwani yapo mambo ambayo viongozi wa CCM hawatakiwi kufanya katika uongozi wao huku akisisitiza kuwa rushwa ni adui wa haki na ni aibu kwa mwanaCCM kutoa na kupokea rushwa.

Aliwataka viongozi hao kutoogopa kusema wala kuwataja watoaji na wapokeaji wa rushwa na wala wasinungunike pembeni kwani hata vitabu vyote vya dini vinakataza rushwa na lazima Mabalozi washirikiane na viongozi wa CCM wa Jimbo, Wilaya na hatimae viongozi wa ngazi za juu katika kuwataja watoaji na wapokeaji rushwa.

Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar alieleza kuwa tayari ameshatangaza kuwa elimu ya Msingi bure na ikifika Julai katika Bajeti ya mwaka huu 2018/2019, elimu ya Sekondari itakuwa bure kwani pesa sio tatizo na kusisitiza kuwa atakaetoza fedha kuanzia muda huo Serikali itapambana nae.Kwa upande wa afya, Dk. Shein alisema kuwa Serikali inauwezo mkubwa wa kutekeleza huduma za afya bure kwa wananchi kwa kutekeleza azma ya Marehemu Mzee Karume katika sekta hiyo.

Alieleza kuwa hakuna mwananchi hata mmoja anaebaguliwa kwa jinsia yake, rangi yake, dini yake, kabila yake huku akieleza kuwa hakuna haja ya kuleta lugha ya istizai katika maendeleo yanayofanywa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Dk. Shein aliwataka viongozi wote wa CCM kuyatangaza mafanikio ya Serikali pamoja na kwenda kuwaeleza watu mafanikio yaliofikiwa “Na nyie mnajua kuwa wengine uongo imekuwa kama jadi yao”,alisema Dk. Shein.

Alisikitishwa na uongo wa baadhi ya wanasiasa wanaosema kuwa kuna walimu wamepelekwa skuli ya Chokocho wakati hakuna mwalimu hata mmoja aliepelekwa katika skuli hiyo. Pia, alitumia fursa hiyo kuwataka Mabalozi kushirikiana katika mapambano ya unyanyasaji wa kijinsia.

Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Abdalla Juma Mabodi alieleza umuhimu wa Mabalozi na mchango wao mkubwa katika kuimarisha chama na kueleza haja ya kutekeleza majukumu yao ipasavyo huku akitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa rais Dk. Shein kwa kutekeleza vyema Ilani ya Uchaguzi.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kusini Pemba, Yussuf Ali Juma kwa upande wake alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa juhudi zake katika kutekeleza Ilani pamoja na uongozi wake madhibuti katika Serikali anayoiongoza.Katika risala yao, Nao Mabalozi walimpongeza Rais Dk. Shein kwa kuendelea kuwajali na kumpongeza kwa kuwajali wazee wanaopata pencheni huku wakieleza jinsi wanavyofaidika na miradi ya TASAF ambayo imekuwa mkombozi katika maisha yao.

Mwajuma Hassan Kaduara akisoma risala ya Mabalozi, alieleza kuwa kuwepo kwa baadhi ya watumishi serikalini ambao hawatoi huduma vyema kwa wananchi hali ambayo inapelekea kuipaka matope Serikali inayoongozwa na CCM.

Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba Hemed Suleiman alitumia fursa hiyo kueleza ukweli juu ya suala zima la ajira lilivyofanyika katika mkoa huo na kueleza kuwa Skuli ya Chokocho hakuna mwalimu hata mmoja aliyopelekwa na maneno yanayovumisha na baadhi ya wanasiasa si ya kweli kama skuli hiyo wamepelekwa walimu wanane na kueleza kuwa ajira zilikuwa zinazingatia Wizaya zote, na kuwataka wale wote wanaovumisha hivyo kuutafuta ukweli. 

Alhamisi, 3 Mei 2018

DK.SHEIN ATANGAZA VITA DAWA ZA KULEVYA Z'BAR.

NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.
MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk.Ali Mohamed Shein akiwa na viongozi mbali mbali wa Chama na Jumuiya zake katika ziara ya kuimarisha Chama ya kuzungumza na mabalozi wa mashina wa CCM Wilaya ya Micheweni Pemba.

MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk.Ali Mohamed Shein amesema hatokubali Zanzibar kugeuzwa uchochoro wa kupitisha, kuuza na kusambaza dawa za kulevya.

Msimamo huo ameutoa leo wakati akihutubia mabalozi na viongozi wa ngazi za mashina wa Wilaya ya micheweni Pemba, amesema haiwezekani dawa za kulevya kuthibitiwa Tanzania bara na kituo cha kuuza dawa hizo kikahamia visiwani Zanzibar.

Ameliagiza Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na vikosi vya Idara maalum za SMZ kuongeza ulinzi na kuhakikisha watu wote wanaojihusisha na vitendo hivyo wanakamatwa na kufikishwa katika vyombo vya kisheria.

“Haiwezekani Zanzibar kuwa kituo cha kufanya biashara za dawa za kulevya na kuangamiza nguvu kazi ya nchi, vyombo vya ulinzi hakikisheni kila muhusika anakamatwa kisheria hata akiwa ni Mwana CCM ama mtu yeyote ndani ya Chama na serikali.

Zanzibar haikuwa na vitendo hivyo vya kihalifu vinavyofanywa na watu wachache kwa tama za kupata fedha za haraka huku wakiangamiza vizazi vya sasa na nguvu kazi ya baadae.

Kupitia mkutano huo Dk.Shein amewataka mabalozi kutoa taarifa sahihi juu ya matukio mbali mbali ya kuhatarisha amani ya nchi yanayotoikea katika jamii kwani wao wapo karibu zaidi za wananchi wa ngazi za chini.

Makamo Mwenyekiti huyo amesema anatambua na kuthamini mchango wa viongozi wa CCM ngazi za mashina wakiwemo mabalozi kuwa wanafanya kazi kubwa ya kuimarisha Chama Cha Mapinduzi.

Dk.Shein amewasihi viongozi hao kwamba ili watekeleze majukumu yao kwa ufanisi ni lazima wasome na kuchambua kwa kina majukumu yao yaliyotajwa katika Katiba ya CCM ya mwaka 1977 toleo la mwaka 2017.

Pamoja na hayo Dk.Shein ambaye ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi amewakumbusha mabalozi hao kwamba licha ya kukabiliwa na majukumu mbali mbali bado wanatakiwa kuendeleza na mikakati ya kukiletea ushindi Chama Cha Mapinduzi(CCM),katika uchaguzi Mkuu ujao.

Pia Dk.Shein ameahidi kuzitafutia ufumbuzi  changamoto zinazoikabili wilaya hiyo zikiwemo kumaliza tatizo la ukosefu wa nishati ya umeme katika kijiji cha Kijongwani, ujenzi wa barabara ya kutoka kijiji cha Kiuyu kwenda Micheweni pamoja na ujenzi wa daharia katika skuli ya sekondari ya Chwaka chumbe katika Wilaya ya Micheweni.

Akizungumza Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Mabodi amesema Chama Cha Mapinduzi kimesimamia vizuri utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2018 katika Wilaya ya micheweni na kuwatoa wananchi katika kiwango cha umasikini uliokithiri na kufikia kiwango cha uchumi wa kati.

Alisema kupitia sera imara za CCM zinazotekelezwa na serikali ya awamu ya saba chini ya uongozi wa Rais wa Zanzibar Dk.Ali Mohamed Shein, wataendelea kuimarisha huduma muhimu za kijamii ili kila mwananchi anufaike na maendeleo hayo.

Aidha Dk. Mabodi ameeleza kwamba Chama Cha Mapinduzi kinaendelea kuimarika kisiasa, kijamii na kiuchumi kutokana na kuwa karibu na wananchi wa makundi yote sambamba na kutekeleza kwa wakati ahadi zinazokidhi mahitaji yao.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini Pemba, Mbwerwa Hamad Mberwa ameipongeza serikali kwa utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM katika Nyanja mbali mbali na kueleza kuwa hatua hiyo imekijengea heshima kubwa Chama mbele ya wananchi.

Katika risala yao mabalozi wa Wilaya hiyo wamesema CCM ni Chama chenye nia ya dhati ya kumaliza changamoto za wananchi wa makundi yote bila ya ubaguzi.

Wamesema katika jitihada za kuimarisha uhai wa Chama Cha Mapinduzi viongozi na watendaji wa ngazi hizo wameendelea kuwafariji wananchama ili waendelee kushikamana licha ya kukabiliwa na vitendo vya hujuma kutoka kwa wapinzani.

Wameeleza kuwa katika kipindi cha mwezi januari hadi april mwaka 2018 Chama ngazi ya wilaya na jumuiya zake kimefanya ziara ya kutembelea ngazi za mashina kwa lengo la kuimarisha Chama Cha Mapinduzi kwa ngazi hiyo.

Wameomba kupatiwa mafunzo kwa lengo la kuongeza uelewa na ufahamu mzuri wa masuala mbali mbali ya kisiasa, kwa lengo la kuiletea ushindi CCM kwa kila uchaguzi.

Hata hivyo wameeleza kwamba wataendelea kulinda amani na utulivu wa nchi, ili serikali iweze kutekeleza kwa ufanisi Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020.