Jumanne, 12 Juni 2018

UVCCM JIMBO LA MTONI WATOA SADAKA KWA WAGONJWA NA WAZEE WASIOJIWEZA

 MWENYEKITI wa UVCCM Jimbo la Mtoni Ibrahim Mtumwa Saleh akizungumza na wajumbe wa Kamati ya siasa ya umoja huo katika jimbo hilo katika kikao cha mipango ya utoaji wa sadaka za mchele na unga wa ngano kwa wagonjwa na wazee wasiojiweza katika shehia tano za jimbo la Mtoni Unguja.

 
KATIBU wa UVCCM Halima Khamis Ali akizungumza katika kikao hicho.

 
MWENYEKITI wa Jimbo hilo Ibrahim  akitoa maelezo juu ya sadaka hizo akiwa na viongozi wengine wa UVCCM na CCM.

 MWENYEKITI wa UVCCM Ibrahim Mtumwa na Katibu  wa UVCCM Jimbo la Mtoni Halima Khamis Ali (kushoto) wakimkabidhi sadaka hizo  Bi. Ghanima   Mohamed Omar  kwa niaba ya Mzee Msham Mbwana(kushoto).

 
BAADHI wa UVCCM na CCM walioshiriki katika zoezi hilo la utoaji wa sadaka kwa wagonjwa na wazee wasiojiweza.

 
NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.


UMOJA wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi ( UVCCM) Jimbo la Mtoni umesema utaendelea kuwasaidia watu wasiojiweza ambao ni wazee na wagonjwa wanaosumbuliwa na maradhi kwa muda mrefu ili waweze kujivua uwepo wa umoja huo katika jimbo hilo.

Kauli hiyo ameitoa Mwenyekiti wa UVCCM wa jimbo hilo Ibrahim Mtumwa Saleh wakati akiwakabidhi sadaka za mchele na unga wa ngano kwa ajili ya Mwezi Mtukufu wa ramadhani na siku kuu ya Idd Fitri wazee na wagonjwa wa shehia tano za Jimbo la Mtoni Unguja.

Amesema licha ya UVCCM kukabiliwa na majukumu ya kisiasa ya kusimamia miongozo ya kikanuni ya umoja huo na CCM hasa kwa rika la vijana bado  wana jukumu kubwa la kutatua changamoto zinazowakabili wazee.

Mwenyekiti huyo alieleza kwamba kundi hilo linahitaji msaada  msaada na uangalizi wa karibu, jambo ambayo imepelekea Umoja huo kuona kuna umuhimu wa kusaidia kundi hilo hasa kwa kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa ramadhani kama walivyo watu wengine katika jamii.

“ UVCCM chini ya ulezi wa CCM tunajali  na kuthamini mchango wa makundi yote katika jamii hasa wazee ambao walitumikia taifa hili kwa muda mrefu, hivyo sisi vijana ni wajibu wetu kuwasaidia mahitaji mbali mbali ambayo yapo ndani ya uwezo tu ili nao wajivunie uwepo wetu ndani ya jamii”, alisema Ibrahim.

Alisema utamaduni huo wa kutoa sadaka kwa makundi mbali mbali katika jamii hasa yenye mahitaji maalum  utakuwa endelevu, na kuwaomba viongozi mbali mbali wa Chama, Jumuiya, Serikali na watu wenye uwezo kuendeleza utaratibu huo.

 Amebainisha kuwa CCM na jumuiya zake ni taasisi bora ya kisiasa iliyokuwa karibu na wananchi wa makundi yote kuliko chama chochote cha kisiasa toka kuanzishwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992.

Naye Katibu wa CCM wa Jimbo hilo Khamis Omar Khamis, alipongeza juhudi za uchapakazi na ubunifu unaofanywa na UVCCM jimbo hilo kwa kuendeleza kwa vitendo harakati na vugu vugu za kujitolea zilizowahi kufanywa na vijana wa enzi za ASP.

Alisema vijana ndio nguzo ya CCM hivyo wanatakiwa kuwa mfano bora wa kutenda na kutekeleza mambo mema yanayoenda sambamba na matakwa ya kanuni, miongozo na sera Chama Cha Mapinduzi katika kutekeleza falsafa ya siasa za maendeleo kwa wote.

Akitoa shukrani zake Bi. Ghanima  Mohamed kwa niaba ya Mzee Msham Mbwana Saleh ambaye ni mgonjwa kwa muda mrefu, alisema sadaka hiyo itatumiwa vizuri ili imsaidie mgonjwa huyo.

 Sadaka hizo  zimetolewa na umoja huo kwa lengo la kuwasaidia wagonjwa na wazee wenye mahitaji maalum wa shehia tano za jimbo la Mtoni.

Ijumaa, 8 Juni 2018

KATIBU MKUU MPYA WA UWT MWL. QUEEN MLOZI AZUNGUMZA NA WENYEVITI NA MAKATIBU WA UWT Z'BAR

 KATIBU Mkuu wa UWT Taifa Ndugu Queen Mlozi akizungumza na viongozi na watendaji wa Umoja huo ngazi za Mikoa na Wilaya Zanzibar, Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui Zanzibar  katika ziara yake ya kujitambulisha.

 BAADHI ya Wenyeviti na Makatibu wa UWT wa Mikoa na Wilaya wakisikiliza hotuba ya Katibu Mkuu wa Umoja huo Taifa.

 VIONGOZI wakuu wa UWT Taifa wakiomba dua katika kaburi la Mwasisi wa Mapinduzi ya mwaka 1964 ambaye pia alikuwa ni Rais wa kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Marehemu Abeid Amani Karume.

 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Mabodi akizungumza na viongozi wakuu wa UWT Taifa waliofika Ofisini kwake, Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui Zanzibar.

 NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Mabodi akielezea historia ya eneo alilouawa na wapinga maendeleo aliyekuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar Mzee Abeid Aman Karume.

 

  SPIKA  wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar Mhe. Zubeir Ali Maulid(kushoto) akizungumza na Mwenyekiti wa UWT Taifa Bi. Gaudencia Kabaka(kulia) alipofika katika Baraza hilo kwa lengo la kujitambulisha na kuzungumza na Wawakilishi wanawake katika Baraza hilo.

  NAIBU Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar Mhe. Mgeni Hassan Juma (kulia) akimkabidhi Katiba ya Jumuiya ya wawakilishi wanawake katika Baraza hilo Katibu Mkuu wa UWT Taifa, Bi. Queen Mlozi (kushoto).



KATIBU Mkuu wa Umoja wa wanawake Tanzania (UWT)Taifa, Ndugu Queen Mlozi ameahidi kufanya kazi kwa weledi, uaminifu na uzalendo uliotukuka ili CCM ishinde katika uchaguzi mkuu wa dola mwaka 2020.

Hayo ameyasema wakati akizungumza na viongozi na watendaji wa ngazi mbali mbali za UWT Zanzibar  hapo Afisi Kuu CCM Kisiwandui  katika ziara yake ya kwanza kujitambulisha kwa viongozi na watendaji  hao.

Alisema atatekeleza majukumu yake kwa ufanisi kwa lengo la kuimarisha  taasisi hiyo ili kwenda sambamba na kasi ya maendeleo ndani ya Umoja huo na Chama kwa ujumla.

Ameeleza kwamba wanawake wa UWT wanatakiwa kuelekeza nguvu zao katika kulinda maslahi ya CCM ili ishinde kwa ngazi zote kwa upande wa Tanzania bara na Zanzibar katika uchaguzi Mkuu ujao.

Katibu Mkuu huyo amewashukuru viongozi viongozi wote wa Chama Cha Mapinduzi waliomuamini na kumteuwa kushika nafasi hiyo ya ngazi ya juu ya kiutendaji kupitia Kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC) kilichofanyika hivi karibuni Jijini Dar es saalam.

“ Viongozi na wanachama wote nakuahidini kwamba nitatumia weledi na uzoefu wangu wote kwa kuhakikisha UWT inaendelea kuwa imara na mkombozi na mtetezi mkubwa wa maslahi ya wanawake wote nchini”, alisema Queen.

Akizungumza Mwenyekiti wa UWT Taifa, Ndugu Gaudencia Kabaka alisema ushirikiano anaoupata kutoka kwa viongozi mbali mbali wa Umoja huo na Chama unampa nguvu na imani ya kusimamia maslahi ya taasisi hiyo bila hofu.

Naye Makamu Mwenyekiti wa UWT Taifa, ndugu Thuwayba Kisasi alisema lengo la ziara hiyo ni Katibu Mkuu huyo mpya  ujitambulisha kwa viongozi wa umoja huo pamoja na kuzungumza na Wawakilishi wanawake wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar.

Kwa Naibu Katibu mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Mabodi alizungumza na msafara wa viongozi hao wa UWT Taifa aliwaeleza kuwa CCM Zanzibar inajivunia uwepo wa umoja huo kwani unafanya kazi kubwa ya kusimamia na kutekeleza kikamilifu sera za Chama kwa makundi yote yaliyopo katika jamii.

Viongozi hao walitembelea Baraza la Wawakilishi Zanzibar  wakazungumza na viongozi mbali mbali wakiwemo Spika wa Baraza hilo Mhe. Zubeir Ali Maulid pamoja na Naibu Spika Mhe. Mgeni Hassan Juma na wakaelezwa masuala mbali mbali ya kiutendaji yanayofanyika katika Baraza hilo.