Jumatano, 15 Julai 2020

MAELFU YA WANA CCM WAMPOKEA DK.HUSSEIN MWINYI ZANZIBAR.


 MGOMBEA Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM Dk.Hussein Ali Hassan Mwinyi akiongozwa na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar  Dk.Abdullah Juma Saadalla Mabodi mara baada ya kuwasili Zanzibar kwa mara ya kwanza toka achaguliwe kuwa Mgombea wa CCM.

 MAELFU ya Wana CCM wakiwa katika msafara wa mapokezi ya Mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM Dk.Hussein Ali Hassan Mwinyi kutoka uwanja wa ndege wa kimataifa wa Zanzibar.

 Mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM Dk.Hussein Ali Hassan Mwinyi ,akizungumza na Wanachama wa CCM na wananchi kwa ujumla katika mapokezi yake hafla iliyofanyika Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui Zanzibar. 

 MAKAMU Mwenyekiti wa CCM Zanzibar ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akizungumzav na Wana CCM katika mapokezi ya Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia CCM Dk.Hussein Ali Hassan Mwinyi, hafla iliyofanyika Kisiwandui Zanzibar.





MAELFU ya Wanachama wa Chama Cha Mapinduzi na Wananchi kwa ujumla kisiwani wamejitokeza kumpokea Mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM Dkt.Hussein Ali Hassan Mwinyi,aliyewasili nchini kwa mara ya kwanza toka achaguliwe kushika nafasi hiyo.

Dkt.Hussein amewasili katika Kisiwa cha Unguja leo majira ya saa 3:43 kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume na kupokelewa na viongozi na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi.

Baada ya kupokelewa makundi mbali mbali ya wanachama yakiwemo ya sanaa pamoja na vijana wa CCM wakiongozwa na kikundi cha pikipiki maalum waliongoza msafara wa kuelekea katika Ofisi Kuu ya CCM Kisiwanduzi Zanzibar, ambapo hafla ya mapokezi ndipo ilipofanyika.

Alipofika katika viunga vya Ofisi hiyo alipokelewa na vijana maalum wa chipukizi na kumvisha sikafu kwa ajili ya kumkaribisha na baada ya hapo alikabidhiwa vifaa mbali mbali na Wazee wa Chama Cha Mapinduzi na akazuru kaburi la Rais wa kwanza wa Zanzibar marehemu Abeid Amani Karume.

Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein akizungumza katika hafla hiyo amesema baadhi ya watu wanadai kuwa Dkt.Hussein sio mzawa wa Zanzibar wanapotosha kwani kiongozi huyo kwa mujibu wa sheria za nchi ni mzaliwa wa Zanzibar na wazazi wake wote wapo.

"Kuna watu tayari wameanza siasa chafu za kuchafuana eti Dkt.Hussein sio mzawa je wao wamezaliwa wapi, wakati sote tunamjua kiongozi huyu kuwa hapa ndio kwao",. amehoji Dk.Shein.

Amesema sifa alizonazo Dkt.Hussein ni nyingi sana zikiwemo upole,uadilifu,utiifu na kuheshimu kila mtu kwa nafasi yake mambo ambayo ni sifa za msingi za kiongozi bora.

Amesema kuchaguliwa kwa Dkt.Hussein kupeperusha bendera ya CCM katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu ndio maendeleo ya CCM ya sasa na yajayo yatakayoendelea kuipaisha nchi kiuchumi.

Pamoja na hayo ameeleza wazi kuwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu utafanyika kwa fedha za ndani za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ),mara Tume ya Uchaguzi Zanzibar(ZEC) itakapotangaza muda rasmi wa kuanza mchakato wa uchaguzi.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Saadalla Mabodi, akizungumza katika mapokezi hayo alisema CCM itaendelea kuwa kinara wa Demokrasia.

Naye Mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM Dkt.Hussein Ali Hassan Mwinyi, amewahakikishia wananchi kuwa endapo atapata ridhaa ya kuwa Rais wa Zanzibar ataendelea kulinda Amani na Utulivu wa Zanzibar kwani ndio msingi wa maendeleo yote.

Amesema atalinda na kuenzi tunu za taifa zikiwemo Muungano na Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964.

Amesema uchaguzi ndani ya CCM tayari umeisha na makundi yote yameisha na kwa sasa limebaki kundi moja la kuiletea ushindi CCM katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.

" Nitahakikisha suala la upemba,uunguja,ukaskazini na ukusini havipewi nafasi kwani vinaweza kukwambisha kasi ya maendeleo yetu", amesema Dk.Hussein.

Amesema nia ya kuwania Urais huo ni kuwatumikia Wananchi wote bila ya ubaguzi kwa kuhakikisha ya wananchi yakuwa bora.

Ameahidi kuwa katika safari ya maendeleo hayo hatovumilia vitendo vya rushwa,ufisadi,wahujumu wa mali za umma na viongozi watakaoshindwa kutekeleza majukumu yao.

Wakizungumza kwa wakati tofauti baadhi ya makada wa CCM walioshiriki katika kuchukua fomu ya kuomba ridhaa ya  kuchaguliwa Urais wa Zanzibar kupitia CCM,walisema kuwa mchakato wa kumpata mgombea huyo umefanyika kwa ufanisi mkubwa na watamuunga mkono.

Akizungumza Shamsi Vuai Nahodha, ambaye ni miongoni mwa makada walioshiriki mchakato wa kuomba ridhaa ya Urais kupitia Chama alisema atamuunga mkono mgombea huyo hadi ashinde na kuwa Rais wa Zanzibar.

Kwa upande wake Dkt.Khalid Salum Mohamed, ambaye ni miongoni mwa makada walioshiriki mchakato wa kuomba ridhaa ya Urais kupitia Chama, amesema ushindi alioupata Dk.Hussein ni ushindi wa Wana CCM wote hivyo kazi iliyobaki ni kuhakikisha anashinda.

Naye Prof.Makame Mnyaa mbawara, amewaomba wananchi visiwani humo kutambua kuwa wamepata bahati ya kuwa na mgombea mwenye sifa za kuwa kiongozi bora.

Katika mchakato wa uchaguzi ndani ya Chama, Dk. Hussein, ambaye ni mtoto wa rais wa awamu ya pili Al-Hajji Ali Hassan Mwinyi, aliwashinda wagombea wengine waliofika katika mchujo wa mwisho, ambao ni waziri kiongozi wa zamani Shamsi Vuai Nahodha na Khalid Salum Mohamed.

Katika mchakato wa ndani wa uchaguzi, Dk.Hussein alipata jumla ya kura 129, ambazo ni sawa na asilimia 78.65, dhidi ya kura 16 za Nahodha na 19 za Khalid Mohamed.

Awali, kamati Maalum ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Zanzibar, ilipendekeza  majina matano na kuyawasilisha kwa kamati Kuu. Pamoja na watatu waliofika duru ya mwisho, wengine walikuwa Makame Mbarawa na Khamis Mussa Omar.  
  

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni