Jumatatu, 10 Julai 2017

Hongereni sana wanaCCM na wale wote wapenda Amani

Mwenyekiti wa  Jumuiya ya wazazi Tanzania, Abdallah Bulembo amewataka wawakilishi, wabunge na madiwani wa majimbo ya Kusini Unguja  kuthamini kazi zinazotekelezwa na mabalozi wa nyumba kumi kwani wao ndio viongozi wanaolinda maslahi ya chama hicho kwa ngazi za chini.

Kauli hiyo ameitoa wakati akizungumza na viongozi na wanachama wa CCM wa Mkoa huo katika mwendelezo wa ziara  yake  ya kuimarisha uhai wa CCM Zanzibar, alisema  mabalozi wa nyumba kumi wanafanya kazi kubwa ya kutafuta wanachama hai  ambao ndio mtaji wa kisiasa wa kufanikisha ushindi wa chama hicho kwa kila uchaguzi.

Alieleza kuwa viongozi hao wa nyumba kumi ndio wanaowajua vizuri wanachama wenye uwezo na nia za kweli za kukisaidia chama hicho katika masuala mbali mbali za kisiasa hivyo wanatakiwa kuungwa mkono wakati wa utekelezaji wa majukumu yao.

Akizungumzia mabadiliko ya chama Bulembo alisema mabadiliko hayo  hayakufanyika  kwa kumkomoa  mtu bali yametokana na dhamira ya kukiimarisha chama kwa lengo la kuwapelekea wananchi wa mijini na vijijini maendeleo endelevu.

Alisema kutokana na mabadiliko yaliyofanywa ndani ya chama na kuweka utaratibu wa kugombea nafasi moja mtu mmoja ni moja ya mkakati wa kuhakikisha kila kiongozi anayepewa dhamana anatumikia nafasi yake kwa ufanisi .

“Wito wangu kwenu viongozi, watendaji na wanachama sote tushirikiane kufanya kazi za chama na jumuiya zetu kwa lengo la kutekeleza kwa vitendo dhana ya kuimarisha uchumi  ndani ya chama na kwa mwananchi mmoja mmojo”, alisema Bulembo.

 Aidha alifafanua kuwa malengo ya  CCM kupitia uchaguzi wa ndani ya chama unaoendelea hivi sasa ni kupata viongozi waadilifu watakaokuwa na uwezo wa kukemea vitendo vya rushwa na makundi yasiofaa ndani ya chama bila ya woga.

Bulembo ambaye ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, aliwasihi viongozi wa Chama hicho kutangaza mafaniko na fursa mbali mbali zilizofanywa na Chama Cha Mapinduzi kwa  kuimarisha  Sekta za elimu, afya na miundombinu ya usafiri wa anga, barabara na bandari za  kisasa..














































Hakuna maoni:

Chapisha Maoni