Jumanne, 22 Machi 2016

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 UTANGULIZI.

Ndugu Waandishi wa Vyombo mbalimbali vya Habari.
ASSALAM ALEYKUM.

Awali ya yote, nachukua nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, Muumba Mbingu na Ardhi na Vyote viliyomo Ndani yake, kwa kutujaalia uzima na afya njema. Aidha, nachukua nafasi hii kwa mara nyengine tena kuwashukuru ninyi Waandishi wa Vyombo mbali mbali kwa kukubali wito wetu na kuhudhuria kikao hiki pamoja na majukumu kadhaa mliyonayo ya kulihabarisha Taifa.

Ndugu Wanahabari,
Bila ya kupoteza muda, lengo kuu la kukuiteni hapa leo hii si jengine bali ni kutoa salamu za pongezi kwa Rais Mteule wa Zanzibar Mhe. Daktari Ali Mohamed Shein, kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi na Wazanzibari hasa Wana CCM hapo tarehe 20 Machi, mwaka huu na hatimaye Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) Mhe. Jecha Salim Jecha, jana (21/03/2016) kumtangaza rasmi kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, kwa kipindi cha miaka mitano ijayo (2015 - 2020).

Kwa mnasaba huo basi, Chama Cha Mapinduzi kinampongeza kwa dhati kabisa aliyekuwa mgombea wa Chama chetu Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, kwa kupata kura halali 299,982  (91.4%). Hakika ni ushindi mkubwa ambao haujapata kutokea katika historia ya demokrasia ya vyama vingi kwa upande wa Zanzibar.

Pia ushindi huo umedhihirisha wazi kuwa bado wananchi wa Zanzibar wana imani kubwa na Chama cha Mapinduzi (CCM) kutokana na utekelezaji mzuri wa ilani ya chama hiki.

Aidha, CCM inampongeza kwa mara nyengine tena kwa hotuba nzuri aliyoitoa katika hafla ya kutangaza matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa Marudio, iliyofanyika jana, ambapo Mhe. Dkt. Shein aliwaahidi Wananchi kuendeleza suala zima la Amani na utulivu wa Taifa, ili kuwafanya watu  waweze kujiendeleza kimaisha.

Sambamba na hilo, Mhe. Rais Shein Mteule huyo, alielezea nia yake ya kusimamia kwa nguvu zote Utekelezaji wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu mwaka 2015 - 2020 na kuinua hali ya kiuchumi kutoka asilimia 7.0 (sasa) kufikia asilimia 10.

Ushindi huo, aliopata Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, haukuja hivi hivi tu, bali umetokana na juhudi na mashirikiano ya pamoja baina ya Viongozi na Wanachama wa CCM na Jumuiya zake wa ngazi zote Unguja na Pemba.

Kama hiyo haitoshi, Wazanzibari wameshawishika na maendeleo yaliyoletwa na CCM chini ya Uongozi uliotukuka wa Rais wa Zanzibar mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, ikiwa ni Utekelezaji wa kwa vitendo Ilani ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 - 2015.

Ndugu Wanahabari,
Chama Cha Mapinduzi kinachukua nafasi hii kuwapongeza pia wana CCM na wananchi wa Unguja na Pemba kwa kutumia kikamilifu haki yao ya demokrasia na hatimaye kufanya maamuzi sahihi na kukichagua Chama Cha Mapinduzi na hivyo kuipa ridhaa ya kuongoza dola Tanzania Bara na Zanzibar katika kipindi cha miaka 2015 - 2020.

CCM pia, inawapongeza Viongozi, Watendaji na Wanachama wa Chama hicho (ngazi zote) pamoja na wananchi kwa ujumla, kwa kujitokeza kwa wingi siku ya upigaji kura na hatimaye kufanya maamuzi sahihi katika Uchaguzi huo wa Marudio, uliofanyika machi 20, mwaka huu, nchini kote.

Sambamba na hilo, Chama Cha Mapinduzi Zanzibar, pia kinavipongeza kwa dhati Vyombo vya Ulinzi na Usalama kwa kusimamia kikamilifu suala la ulinzi katika Mikoa yote ya Zanzibar kabla na wakati wote wa zoezi la upigaji kura, hali iliyotoa fursa kwa wananchi kuweza kutekeleza haki yao hiyo ya kidemokrasia.

Mwisho, nawapongeza kwa dhati wadau mbali mbali waliofanikisha kwa namna moja ama nyingine  uchuguzi mkuu huo wa Marudio kwa  amani na utulivu.

‘KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI’

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni